
Kamishna Jenerali wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji John Masunga, leo Machi 27, 2023 amefungua Semina ya Utekelezaji wa Miradi ya Ujenzi ya Jeshi la Zimamoto na Uokoaji kwa mwaka 2022/2023.
Akizungumza wakati wa Ufunguzi wa Semina hiyo katika Ukumbi wa Makao Makuu ya Jeshi hilo Jijini Dodoma, Kamishna Jenerali amewataka wote wanaohusika na Miradi hiyo kufuata taratibu zilizowekwa katika kuendesha Miradi hiyo ya Ujenzi itakayotumia mfumo wa Force Account.
Wiki iliyopita, Kamishna Jenerali Masunga alisema tayari wameshapokea fedha kutoka kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt Samia Suluhu Hassan kwa ajili ya Miradi ya Ujenzi wa Vituo katika Mikoa saba (07) iliyokuwa haina vituo vya Zimamoto na Uokoaji (Manyara, Simiyu, Songwe, Katavi, Kagera, Geita na Njombe) pamoja na kuendeleza Miundombinu ya Chuo cha Zimamoto na Uokoaji, Handeni Tanga.

Semina hiyo itakayofanyika kwa siku nne (04) hadi siku ya Alhamisi tarehe 30 Machi, 2023 itaendeshwa na watoa mada mbalimbali wakiwemo Kamishna wa Utawala na Fedha wa Zimamoto na Uokoaji Mbaraka Semwanza pamoja na Mkurugenzi wa Manunuzi Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi Bw. Ole Mbille Kissioka.