Na. Veronica Mwafisi-Dodoma

Kaimu Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma, Bi. Leila Mavika amewataka wadau kutoka katika taasisi za umma walioshiriki kikao kazi cha kujadili maeneo muhimu yenye uhitaji wa mafunzo kwa Watumishi wa Umma kuanisha maeneo hayo kwa kuzingatia mabadiliko ya kiutendaji, teknolojia na vipaumbele vya Serikali ili mafunzo yatakayotolewa yaboreshe utendaji kazi wa watumishi wa umma na kuwa na tija katika maendeleo ya taifa.
Bi. Leila Mavika ametoa wito huo kwa niaba ya Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma Bw. Juma Mkomi wakati akifungua kikao kazi cha wadau cha kujadili maeneo muhimu yenye uhitaji wa mafunzo kwa watumishi wa umma, kilichofanyika katika Ukumbi wa Ofisi ya Rais-UTUMISHI Mtumba jijini Dodoma.

Bi. Mavika amesema Serikali inatarajia kikao kazi hicho kitajadili na kuanisha maeneo muhimu ya mafunzo kwa ajili ya watumishi wa umma yatakayowezesha kufikia Dira ya Taifa na kutekeleza Mpango wa Maendeleo wa Taifa wa miaka mitano 2021/22-2025/26.
Bi. Mavika ameongeza kuwa, maeneo ya mafunzo yatakayoanishwa na wadau wa kikao kazi hicho yatawasilishwa kwa wadau wa maendeleo ambao wanashirikiana na Ofisi ya Rais-UTUMISHI ili waweze kutoa fursa za mafunzo ya muda mrefu na muda mfupi kwa watumishi wa umma zitakazoendana na mahitaji halisi na vipaumbele vya kitaifa.
Aidha, Bi. Mavika amewashukuru wadau walioshiriki kikao kazi hicho kwa mwitikio chanya na kuongeza kuwa ushiriki wao utakuwa na mchango mkubwa kwa ustawi wa taifa.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Idara ya Uendelezaji Rasilimaliwatu, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Dkt. Edith Rwiza amesema, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma
na Utawala Bora imedhamiria kuendelea kutoa mafunzo yenye tija kwa Viongozi na watumishi wa umma kupitia fursa za mafunzo zinazotolewa na wadau wa maendeleo, hivyo kikao kazi hicho kitaanisha aina ya mafunzo yatakayopewa kipaumbele na Serikali.
Dkt. Edith amesema kuwa, ili kutumia vizuri fursa za mafunzo zinazotolewa na wadau wa maendeleo, Serikali iliona ni vema kikao hicho cha wadau kifanyike kwa lengo la kuainisha mafunzo yanayohitajika kwa watumishi wa umma.
