
Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inayoongozwa na Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan imetenga zaidi ya Shilingi billioni tano kwa ajili ya kujenga mradi mkubwa wa maji kwa ajili ya kutatua changamoto za maji katika Jiji la Mbeya, ambao utasaidia kusambaza maji katika maeneo mbalimbali ikiwemo Kata za Mwansekwa na Iganzo ikiwemo mitaa ya Iganzo na Igodima. Mradi huo unatarajiwa kukamilika ndani ya mwaka wa fedha wa 2022/23.

Hayo yamesemwa na Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambaye pia ni Mbunge wa Mbeya Mjini, Mhe. Dkt. Tulia Ackson wakati alipofanya ziara katika kata ya Iganzo na kujionea changamoto ya maji wanayokumbana nayo Wananchi wake.
“Niwahakikishie ndugu zangu kwamba Serikali imetutengea zaidi ya bilioni tano kwa ajili ya ujenzi wa mradi mkubwa wa maji ambao utajengwa Kata ya Itagano kwa ajili ya kusambaza maji katika maeneo mbalimbali ikiwemo maeneo yote yanayozunguka Kata hiyo ikiwemo Iganzo na Igodima” amesema Dkt. Tulia
Kuhusu changamoto ya barabara, Mhe. Dkt. Tulia amesema kuwa tayari Serikali imeshaanza mchakato wa kuziboresha barabara kuu za Jiji hilo ikiwa ni pamoja na za mitaa ambayo zitajengwa kwa viwango vya lami.