
Maafisa na Askari wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji wapatao nane (08) Siku ya Jumatano tarehe 21 Septemba, 2022 walifanikiwa kufika katika Kilele cha Mlima Kilimanjaro (Uhuru Peak) huku wakipeperusha vyema Bendera ya Jeshi hilo kwa furaha.
Hii ni awamu ya tatu kwa Baadhi ya Maafisa na Askari wa Jeshi hilo ambao safari hii waliongozwa na Mrakibu Msaidizi wa Zimamoto (ASF) Shomari Salla kufanikiwa kupanda katika kilele cha Mlima huo, ambapo awamu ya Kwanza iliongozwa na Aliyekuwa Kamishna Jenerali wa Jeshi hilo ambaye kwa sasa ni Mkuu wa Mkoa wa Kigoma Mhe. Thobias Andengenye.
Hii imekuwa ni kama desturi ya Jeshi hilo kuendelea kutangaza na kuhamasisha Utalii wa Ndani kama ambavyo Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania alivyoamua kutangaza Utalii kwa kuandaa Filamu ya Uhamasishaji ijulikanayo kama THE ROYAL TOUR inayoendelea kuvutia watalii wengi kutoka Mataifa mbalimbali Ulimwenguni.