Na Deborah Munisi, Dodoma
Wito huo umetolewa na waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu)Mhe. Prof. Joyce L. Ndalichako katika mkutano wa waandishi wa habari leo Sep21 2022 jijini dodoma ambapo ametanabaisha kuwa Tanzania itashiriki Maonesho ya 22 ya Wajasiriamali Wadogo na wa Kati wa Jumuiya ya Afrika Mashariki tarehe 8n hadi 18 mwezi Decemba 2022.
“Tanzania itashiriki maonyesho ya 22 ya wajasiriamali wadogo na wakati wa jumuiya ya Afrika Mashariki maarufu kama Nguvu Kazi au Jua Kali yatakayofanyika Jijini Kampala, Uganda kuanzia tarehe 8 hadi 18 mwezi Desemba 2022. Wajasiriamali wapatao 1,000 kutoka Burundi, Kenya, Rwanda, Uganda, Sudan ya Kusini, Jamhuri ya Demokrasia ya Congo na Jamhuri ya Muungano wa Tanzania watashiriki maonesho hayo”

Prof. Ndalichako amesema maonyesho hayo yanalenga kuwainua vijana wajasiriamali wa kati na wadogo waliopo katika sekta isiyo rasmi ili kurasimisha shughuli zao kwa kuwapatia fursa ya kutangaza bidhaa zao.
“Maonesho haya hujulikana kama Maonesho ya Nguvu Kazi au Jua Kali kwasababu yanawalenga vijana wajasiriamali wa kati na wadogo waliopo katika sekta isiyo rasmi. Lengo kubwa la maonesho haya ni kuwawezesha vijana wajasiriamali kurasimisha shughuli zao kwa kuwapatia fursa ya kutangaza bidhaa zao, kubadilishana taarifa, kukuza ujuzi, kukuza masoko ya bidhaa na kukuza teknolojia ya utengenezaji wa bidhaa na hatimaye kuongeza fursa za ajira za staha kwa vijana.”

Ameendelea kubainisha fursa ambazo wajasiriamali hao watakazo nufaika nazo ikiwa ni pamoja na kuwajengea uwezo kuhusu masoko na kujifunza mbinu za kutengeneza bidhaa, sambamba na kutafuta masoko kutoka kwa nchi zingine za wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki.
“Maonesho haya hufanyika sambamba na mafunzo ya kuwajengea uwezo Wajasiriamali kuhusu masoko; Ubora wa bidhaa; Urasimishaji biashara; na Kuongeza thamani ya bidhaa. Kwa vijana wajasiriamali wa Tanzania, maonesho haya ni fursa ya pekee kujifunza mbinu za kutengeneza bidhaa na kutafuta masoko kutoka kwa wenzetu wa nchi wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki. Maonesho haya ni ya kipekee na yanaratibiwa na Ofisi ya Waziri Mkuu Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu kutokana na ukweli kwamba ofisi hii ndiyo inahusika katika kuendeleza vijana, kukuza fursa za ajira hususan kwa vijana wajasiriamali wa makundi yote wakiwemo wenye ulemavu.”

Kama ilivyodesturi kila kituu kina chimbuko lake, maonyesho haya yalifanyika kwa mara ya kwanza ya kwanza mwezi Desemba, 1999 Jijini Arusha, Tanzania sambamba na Sherehe za Utiaji Saini wa Mkataba wa Uanzishwaji wa Jumuiya ya Afrika Mashariki uliofanyika tarehe 30 Novemba, 1999 zikiwepo nchi za Kenya, Uganda na Tanzania na kuja na suluhu kuwa maonesho haya yaendelee kufanyika kila mwaka kwa mzunguko katika kila nchi wanachama.
“Maonesho haya yalifanyika kwa mara ya kwanza mwezi Desemba, 1999 Jijini Arusha, Tanzania sambamba na Sherehe za Utiaji Saini wa Mkataba wa Uanzishwaji wa Jumuiya ya Afrika Mashariki uliofanyika tarehe 30 Novemba, 1999 zikiwepo nchi za Kenya, Uganda na Tanzania. Maonesho haya yalihudhuriwa na Wakuu wa Nchi Wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki. Wakuu hao wa nchi waliagiza maonesho haya yaendelee kufanyika kila mwaka kwa mzunguko katika kila nchi wanachama. Hivyo, maonesho haya hufanyika kila mwaka wiki ya kwanza na ya pili ya mwezi wa Desemba kama sehemu ya kumbukumbu ya kuanzishwa tena Jumuiya ya Afrika Mashariki. Tanzania imekua mwenyeji wa maonesho haya mara sita (mwaka 1999 Arusha, Dar es Salaam mwaka 2003, 2006, 2009, 2015 na mwaka 2021 Jijini Mwanza). ” Amesema Ndalichako.

Aidha amesema kongamano hilo piah linalenga kuibua vijana wajasiriamali mahiri wakiwemo watu wenye ulemavu watakao wakilisha Tanzania katika maonyesho hayo hivyo amewataka kujitokeza kwa wiingi huku akielekeza mamlaka zinazohusika kuhakikisha zinawaibua vijana wajasiriamali ili kuweza kushiriki maonyesho kikamilifu.
“Ofisi ya Waziri Mkuu Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu kwa kushirikiana na Ofisi ya Rais – Kazi, Uchumi na Uwezeshaji – Zanzibar, Wizara, Taasisi nyingine za Serikali na Shirikisho la Vyama vya Wajasiriamali – (CISO) imejipanga kukahikisha inaibua vijana wajasiriamali mahiri wakiwemo watu wenye ulemavu watakaoiwakilisha Tanzania katika maonesho haya.”
“Hivyo, nichukue fursa hii kuelekeza Mamlaka zote zinazohusika kuhakikisha zinawaibua vijana wajasiriamali wakiwemo wenye ulemavu ili washiriki maonesho haya kikamilifu. Aidha, ninazielekeza Mamlaka za Serikali za Mitaa kuhakikisha kuwa vijana wajasiriamali watakaoshiriki maonesho haya wanapeleka bidhaa za asili za Mikoa au Wilaya wanazotoka.

Amesema washiriki wanaokusudia kushiriki maonyesho hayo zinapatikana katika tovuti ya Ofisi ya Wakurugenzi wa Halmashauri za Wilaya na Manispaa kote nchini kuanzia tarehe 26 Septemba 2022.
“Fomu za maombi pamoja na maelekezo kwa Wajasiriamali wanaokusudia kushiriki maonesho haya zitapatikana kuanzia tarehe 26 Septemba, 2022 katika Ofisi za Wakurugenzi wa Halmashauri za Wilaya na Manispaa kote nchini na pia katika tovuti ya Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu: www.kazi.go.tz. Aidha, fomu hizo pia zitapatikana kupitia Shirikisho la Vyama vya Wajasiriamali Wadogo (CISO (T) ila zote zitapaswa kurudishwa kupitia Ofisi za Wakurugenzi wa Halmashauri za Wilaya, Miji na Manispaa. Mwisho wa kurudisha fomu kupitia Halmashauri husika ni tarehe 17 Oktoba, 2022 ili kutoa muda wa kutosha kuchagua Wajasiriamali watakaokidhi vigezo. Ninapenda kusisitiza kwa wahusika wote kuhakikisha wanawaibua na kuwateua vijana wajasiriamali kwa kuzingatia vigezo vilivyowekwa.” Amesema waziri Ndalichako.

Aidha ameeleza vigezo wanavyotakiwa kuzingatia washiriki wa kongamano hilo ikiwa ni pamoja na kutumia ubunifu, cheti cha uasili wa bidhaa na kupeleka bidha iliyoalishiwa hapa nchini kulingana na mkoa husika.
“Mshiriki mwenye kuzalisha bidhaa zenye ubora na kukidhi viwango vinavyokubalika kibiashara na watakaotoa sura halisi ya bidhaa zinazotengenezwa Tanzania hususan katika Mkoa husika”
“Mshiriki awe na vipeperushi na kadi ya utambulisho wa bidhaa (business cards) kama nyenzo muhimu ya kutangaza bidhaa na kutafuta masoko”
“Mshiriki awe na bidhaa za ubunifu wa hali ya juu, kipaumbele kikiwa ni bidhaa zinazotokana na ngozi na mazao ya ngozi, nguo pamoja na bidhaa za kilimo zilizosindikwa, mifugo, mazao ya misitu, bahari, viungo (spices) na urembo”

“Mshiriki awe na cheti cha uasili wa bidhaa (Certificate of Origin) kinachotolewa na TCCIA na ZCCIA kwa upande wa Zanzibar;”
“Mshiriki awe na vifungashio vizuri vya bidhaa yake vinavyokubalika kimazingira; Mshiriki awe tayari kujaza dodoso la taarifa za maendeleo ya biashara yake wakati wa Maonesho kama itakavyotakiwa na kurejesha dodoso kwa waratibu wa maonesho, Mshiriki awe na uwezo wa kujihudumia na kujigharamia kwa muda wote wa maonesho,Idadi ya watu walioajiriwa na Biashara au huduma ya mhusika.”
Amewatoa hofu washiriki watakao shiriki maonyesho hayo huko nchini Uganda kwa kuwahakikishia wajasiriamali usalama wa bidhaa zao na kuwasisitiza kuandaa bidhaa zitakazokidhi vigezo.
“Majukumu mingine ya Serikali ni pamoja na kuhakikisha uwepo wa usalama wa wajasiriamali na mali zao kipindi chote cha safari na maonesho pamoja na kuratibu upatikanaji wa mafunzo mbalimbali kabla na wakati wa maonesho yatakayotolewa na taasisi kama vile TBS, TRA, TMDA, BRELA, SIDO, GS-1, OSHA, WCF, NSSF, TANTRADE, NHIF na TWCC, wajasiriamali wa Tanzania kujitokeza kushiriki maonesho haya bila wasiwasi wowote kwa kuwa tumejipanga kuhakikisha mnashiriki maonesho haya ipasavyo” amesema Prof. Ndalichako

“Pia naomba taasisi za huduma za biashara kwa wajasiriamali kuendelea kuwaandaa ili kukidhi vigezo vya kuweza kushindana kibiashara ndani na nje ya nchi.”
kwa upande wake Bw. Josephat Rweyemamu, ambaye ni Mwenyekiti wa Shirikisho la Vyama Vya Wajasiriamali Wadogo Tanzania (CISO) amewataka wajasiriamali ambao watashiriki kwenye maonyesho hayo kutumia bidhaa zinazozalishwa hapa nchini ili kuzidi kukuza utamaduni wa nchi.
Maonyesho ya mwaka huu yataenda sambamba na kauli mbiu ya Bidhaa au Huduma za Afrika Mashariki ili Kuijenga Afrika Mashariki kwa Ustahimilivu na Maendeleo Endelevu (Buy East African to Build East Africa for Resilience and Sustainable Development).
