OR – TAMISEMI

Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, Mhe. Innocent Bashungwa amelipongeza Jeshi la Zimamoto na Uokoaji kwa kufanikiwa kuudhibiti moto uliotokea tarehe 21 Juni katika Ofisi za TAMISEMI jengo la Sokoine Jijini Dodoma kwa kushirikiana na kampumi ya ulinzi ya Mputa Security Guard.
Ametoa pongezi hizo Juni 23, 2022 Jijini Dodoma wakati alipokutana na watumishi wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji pamoja na kampuni ya ulinzi ya Mputa Security Guard walioshirikiana kwa pamoja kudhibiti moto uliotokea katika ofisi za wizara hiyo.

“Juzi tulipata janga la moto lakini kwa kudra za Mwenyezi Mungu kupitia Jeshi la Zimamoto mliweza kudhibiti moto huo, kwahiyo niliomba tukutane hapa kuwashukuru kwa jitihada kubwa kwa kitendo cha ujasiri na uzalendo mlioufanya kwa kuweza kudhibiti moto uliotokea hapa Ofisi ya Rais – TAMISEMI” amesema Bashungwa
Bashungwa amesema, tunamshukuru Mungu moto huo haukusababisha madhara kwa mtumishi yeyote wala hakuna nyaraka yoyote muhimu iliyoteketea katika tukio hilo tofauti na mtumishi wa Zimamoto aliyeumia mkono wakati akitekeleza majukumu yake.

Aidha, Bashungwa ametoa wito kwa Watanzania kuendelea kutoa ushirikiano kwa Jeshi la zimamoto wakati kunapotokea majanga ya moto au majanga mengine katika maeneo yanayowazunguka.


