Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam imetupilia mbali maombi ya zuio la kuvuliwa Ubunge yaliyowasilishwa na Wabunge 19 waliovuliwa uanachama na CHADEMA, wakiongozwa na Halima Mdee.
Mbali hilo, pia imetupilia mbali maombi ya Msingi ya kutaka kupewa kibali cha kufungua kesi ya kupinga kuvuliwa Uanachama.
Miongoni mwa sababu ya kutupiliwa mbali kwa maombi hayo ni kukosewa kwa jina la mjibu maombi namba moja ambaye ni Bodi ya Wadhamini ya CHADEMA iliyosajiliwa.
Uamuzi huo umetolewa leo na Jaji John Mgetta wakati akitoa uamuzi wa mapingamizi Sita yaliyowasisilishwa na Mawakili wa CHADEMA waliosema kwamba mahakama hiyo haina mamlaka ya kusikiliza maombi hayo yaliyoijumuisha Tume ya Uchanguzi (NEC) kwa madai kwamba tume hiyo haiwezi kuchunguzwa kwa maamuzi yoyote itakayokuwa imeyafanya.
Pia maombi hayo yalikuwa batili kwa sababu imeambatishwa na maelezo ya waombaji ambayo ni batili kutokana na kuingiza sahihi za Mawakili badala za waombaji.
Kutokana uamuzi huo, kinachosubiriwa ni tamko la Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dr.Tulia Ackson ya kwamba Mdee na wenzake sio wabunge.
Halima Mdee na wenzake walifungua maombi hayo mahakamani hapo kwa nia ya kuiomba mahakama itoe kibali cha wao kufungua kesi ya kupinga mchakato wa kuvuliwa uananachama wao.
Wengine waliofukuzwa ni Esther Matiko, Grace Tendega, Cecilia Pareso, Ester Bulaya, Agnes Lambart, Nusrat Hanje, Jesca Kishoa, Hawa Mwaifunga, Tunza Malapo, Asia Mohammed, Felister Njau, Naghenjwa Kaboyoka, Sophia Mwakagenda, Kunti Majala, Stella Flao, Anatropia Theonest, Salome Makamba na Conchesta Rwamlaza.