
[2:10 AM, 6/16/2022] Msombe Bro: MTENDAJI Mkuu Dawasa, Mhandisi Cyprian Luhemeja, amesema kisima kirefu chenye kuzalisha maji lita 450,000 kwa saa ambayo ni sawa na lita 10,800,000 kwa siku kilichopo Kigamboni kimeanza kufanya kazi leo.
Luhemeja ameyasema hayo leo Juni 15, 2022 katika mkutano wa Uwekezaji na Maendeleo ya Sekta ya Maji ya chini ya Serikali ya Awamu ya sita uliofanyika kwa njia ya Zoom.
Amesema Dawasa ambayo imefika asilimia 95 ya kusambaza maji nyumbani, inazalisha lita 520 kwa siku na kwamba kuanza kwa kisima hicho cha Kigamboni kitamaliza tatizo la maji kwa wakazi wa Kigamboni na maeneo mengine ya Temeke.
Hadi sasa jumla ya visima 14 vimechimbwa vyenye urefu wa mita 400 hadi mita 600.

Amesema kukamilika kwa visima saba vya Kimbiji kumetoa kipaumbele kwa mradi wa maji Kigamboni kutekelezwa kwa awamu tatu na kukamilika kwa kisima hicho kirefu kuliko vyote, wananchi wa Kigamboni watapata huduma ya maji ya uhakika.
Luhemeja amesema ajenda kubwa kwa sasa ni uboreshaji wa huduma ya usafi wa mazingira kwa kuboresha miundombinu ya usafi wa mazingira kwa kununua magari makubwa 15 ya kubeba majitaka, ambayo yamesaidia wananchi kupata huduma kwa urahisi na kwamba huduma hiyo inapatikana pia mtandaoni.
“Tumeboresha miundombinu ya majitaka ikiwemo ukarabati wa mabwawa ya kupokea majitaka yaliyopo Mikocheni, Mabibo, Kurasini na Airwing, ” amesema Luhemeja.