
Sekta za Mifugo za Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania (SMT) na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar (SMZ) kupitia Makatibu wake wakuu wamekutana na kupitia utekelezaji wa maazimo yaliyowekwa ili kuendeleza sekta hiyo.
Akifungua kikao hicho leo (13.06.2022) Kaimu Katibu Mkuu Sekta ya Mifugo (SMT), Dkt. Charles Mhina kwenye ukumbi wa Ofisi ya Jeshi la Zimamoto Jijini Dodoma amesema kuwa serikali ina lengo la kuhakikisha sekta ya mifugo inakua na kuongeza mchango wake kwenye pato la taifa.

Dkt. Mhina amesema kuwa katika kikao kilichopita yapo maazimio yaliyowekwa ambayo yanapitiwa utekelezaji wake, lengo likiwa ni kuhakikisha sekta ya mifugo inawanufaisha wafugaji na wadau walio kwenye mnyororo wa thamani na kuongeza mchango wa sekta kwenye pato la taifa.
“Vikao hivyo vya ushirikiano wa kuendeleza Sekta ya Mifugo vinajadili maendeleo ya sekta katika udhibiti wa magonjwa yanayovuka mipaka, uboreshaji wa kosaafu za mifugo, masoko ya mifugo na mazao yake na kuona ni changamoto zipi zinazoikabili sekta ya mifugo katika pande zote mbili za Muungano ili kuzitatua,” alisema
Dkt. Mhina amesema kuwa kikao hicho kimepitia utekelezaji wa maazimio yaliyowekwa kwenye kikao kilichopita na kuona utekelezaji uliofanyika kwenye baadhi ya maeneo, lakini pia yapo maeneo mapya ambayo wamebaini kuwepo kwa changamoto nyingine ambazo pia tayari wameshaziwekea maazimio ya utekelezaji, lengo kuu ni kuhakikisha sekta inakua kwa pande zote mbili za SMT na SMZ.
Kwa upande wake mwakilishi wa Katibu Mkuu wa Wizara ya Kilimo, Umwagiliaji, Maliasili na Mifugo (SMZ), Bi. Asha Zahran amesema kuwa kupitia vikao hivyo tayari wameshaanza kuona mafanikio yake kwani wapo wataalam kutoka Zanzibar ambao wamepata mafunzo ya kuhimilisha Ng’ombe kupitia kituo cha NIC, mbegu bora za ng’ombe, kilimo cha malisho pamoja na masuala ya udhibiti wa magonjwa kutoka SMT. Hivyo ushirikiano huu ukiendelea utawezesha sekta ya mifugo kuimarika kwa pande zote za Muungano.
Naye mwakilishi kutoka Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira, Bw. Allan Bendera alisema kuwa Wizara inaendelea kuhakikisha changamoto zinazohusu Muungano zinatatuliwa ili kudumisha muungano kwa maendeleo ya taifa kwa ujumla. Hivyo kwa upande wa Sekta ya Mifugo changamoto zilizojitokeza zitaendelea kufanyiwa kazi kwa pande zote za Muungano lengo likiwa ni kuwasaidia wafugaji waweze kuongeza kipato na kuongeza kipato cha Sekta ya Mifugo kwenye pato la Taifa.
