HOTUBA YA MHESHIMIWA BALOZI LIBERATA RUTAGERUKA MULAMULA (MB). WAZIRI WA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI AKIWASILISHA BUNGENI MAKADIRIO YA MAPATO NA MATUMIZI KWA MWAKA WA FEDHA 2022/2023.

YALIYOMO
YALIYOMO………………………………………………………… i
ORODHA YA VIFUPISHO……………………………………. iv
1.0 UTANGULIZI……………………………………………… 5
2.0 TANZANIA NA UHUSIANO WA KIMATAIFA……….7
3.0 TAARIFA YA HALI YA SIASA, ULINZI NA
USALAMA DUNIANI……………………………………….8
3.1 Afrika………………………………………………………..8 3.2 Mashariki ya Kati………………………………………11 3.3 Ulaya na Amerika…………………………………….. 13
3.4 Asia na Australasia……………………………………14
4.0MAPITIO YA UTEKELEZAJI WA MPANGO NA
BAJETI YA WIZARA KWA MWAKA WA FEDHA
2021/2022………………………………………………..14
4.1 Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha
2021/2022…………………………………………….17
4.1.1 Mapato………………………………………………….17 4.1.2 Fedha Zilizoidhinishwa…………………………….18
4.1.3 Matumizi……………………………………………….18
4.2 Kusimamia na Kuratibu Masuala ya Uhusiano Baina ya Tanzania na Nchi Nyingine………….19
4.2.1 Ushirikiano wa Tanzania na Nchi za Afrika…20
4.2.2 Ushirikiano wa Tanzania na Nchi za Asia na
Australasia………………………………………………25
4.2.3 Ushirikiano wa Tanzania na Nchi za Mashariki
ya Kati…………………………………………………….31
4.2.4 Ushirikiano wa Tanzania na Nchi za Ulaya na
Amerika…………………………………………………. 37
4.3 Kuratibu Masuala ya Ushirikiano wa Kikanda na
Kimataifa………………………………………………….. 48
4.3.1 Jumuiya ya Afrika Mashariki……………………49
4.3.2 Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika
(SADC)…………………………………………………… 63
4.3.3 Umoja wa Afrika……………………………………..67
4.3.4 Jumuiya ya Nchi za Ukanda wa Maziwa Makuu
(ICGLR)………………………………………………….. 69
4.3.5 Ushirikiano wa Kimataifa…………………………69 4.4 Kufuatilia na Kusimamia Utekelezaji wa
Mikataba ya Kimataifa na Hati za Makubaliano za
Ushirikiano………………………………………………..74
4.5 Kuratibu Masuala ya Itifaki, Uwakilishi na
Huduma za Kikonseli…………………………………..75
4.6 Uratibu wa Watanzania Wanaoishi Nje ya Nchi
(Diaspora)…………………………………………………. 83
4.7 Elimu kwa Umma…………………………………….. 86
4.8 Utawala na Maendeleo ya Watumishi………….. 88 4.9 Kuratibu na Kusimamia Utekelezaji wa Miradi ya Maendeleo ya Wizara na Taasisi Zilizo Chini ya
Wizara……………………………………………………….91
4.10Taasisi Zilizo Chini ya Wizara……………………..94
4.10.1Kituo cha Kimataifa cha Mikutano Arusha
(AICC)……………………………………………………..95
4.10.2 Chuo cha Diplomasia…………………………….97
4.10.3 Mpango wa Hiari wa Afrika wa Kujitathmini katika Masuala ya Demokrasia na
Utawala Bora………………………………………… 100
5.0CHANGAMOTO NA HATUA ZILIZOCHUKULIWA 104
6.0SHUKRANI……………………………………………….104
7.0MALENGO YA WIZARA KWA MWAKA WA FEDHA
2022/2023………………………………………………108
8.0MALENGO YA TAASISI ZILIZO CHINI YA WIZARA
KWA MWAKA WA FEDHA 2022/2023……………109
9.0MAKADIRIO YA MAPATO NA MATUMIZI YA
WIZARA KWA MWAKA WA FEDHA 2022/2023.112
10.0 HITIMISHO……………………………………………113
ORODHA YA VIFUPISHO
AfCFTA – AfricanArea Continental Free Trade
AfDB – African Development Bank
AICC – ArushaCentre International Conference
APRM – African Peer Review Mechanism
BADEA – ArabDevelopmentBankin Africafor Economic
CFR – Centre for Foreign Relations
DRC – Democratic Republic of Congo
EAC – East African Community
Km – Kilometa
United Nations Multidimensional
MINUSCA – Intergrated Stabilization Mission in
the Central African Republic
United Nations Organization
MONUSCO – Stabilization Mission in the
Democratic Republic of Congo.
MW – Megawatt
OACPS – Organisationand Pacific Statesof African, Carribean
OSBP – One Stop Border Post
SADC | – SouthernCommunity African Development |
TEHAMA | – TeknolojiaMawasiliano ya Habari na |
UNESCO | United Nations Educational, – Scientific and Cultural Organisation |
UNDP | – UnitedProgrammeNations Development |
UNIDO | – UnitedDevelopmentNationsOrganisationIndustrial |
UNIFIL | – UnitedLebanonNations Interim Force in |
UVIKO-19 | – Ugonjwa wa Virusi vya Korona |
1.0 UTANGULIZI
- Mheshimiwa Spika, kufuatia taarifa iliyowasilishwa leo katika Bunge lako tukufu na Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama, ninaomba kutoa hoja kwamba Bunge lako tukufu likubali kupokea na kujadili taarifa ya utekelezaji wa Mpango na Bajeti ya Wizara ya Mambo ya Nje na
Ushirikiano wa Afrika Mashariki kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 na pia lijadili na kupitisha Mpango na Bajeti ya Wizara na Taasisi zilizo chini yake kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023.
- Mheshimiwa Spika, awali ya yote ninamshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema kwa kutujalia afya njema na kutuwezesha kukutana hapa leo kwa ajili ya kujadili Taarifa ya Mapitio ya Utekelezaji wa Mpango na Bajeti ya
Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023.
- Mheshimiwa Spika, ninaomba nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kutimiza mwaka mmoja wa kuiongoza nchi yetu. Ninawapongeza pia Mheshimiwa Dkt. Philip Isdor Mpango, Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; Mheshimiwa Dkt. Hussein Ali Mwinyi, Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi; na Mheshimiwa Kassim Majaliwa Majaliwa (Mb.), Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa utendaji wao mahiri na wa kizalendo.
- Mheshimiwa Spika, katika kipindi hiki tumeshuhudia mafanikio makubwa ya kimaendeleo katika Taifa letu ikiwemo kuimarika kwa diplomasia na uhusiano baina ya Tanzania na nchi nyingine na mashirika ya kimataifa. Ninaungana na Waheshimiwa Wabunge na Watanzania wenzangu kuendelea kuwaombea viongozi wetu Wakuu kwa Mwenyezi Mungu aendelee kuwapa nguvu, ulinzi, afya na kila lililo la heri katika kutekeleza majukumu ya kuliongoza Taifa ikiwemo kukuza na kuimarisha uhusiano wa kidiplomasia. Kazi Iendelee!
- Mheshimiwa Spika, ninakupongeza kwa kuchaguliwa kuwa Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Ninampongeza pia Mhe. Mussa Azzan Zungu (Mb.) kwa kuchaguliwa kuwa Naibu Spika wa Bunge. Aidha, ninawapongeza Mhe. Najma Murtaza Giga (Mb.) na Mhe. David Mwakiposa Kihenzile (Mb.) kwa kuendelea kukusaidia kutekeleza kikamilifu majukumu ya kuliongoza Bunge letu tukufu.
- Mheshimiwa Spika, ninapenda kumpongeza Mhe. Vita Rashid Kawawa, Mbunge wa Namtumbo kwa kuteuliwa kuwa Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama. Aidha, ninawapongeza na kuwashukuru wajumbe wote wa Kamati hii kwa kazi nzuri ya kuishauri Wizara na Serikali kwa ujumla. Naomba nikiri kuwa miongozo na ushauri wao katika masuala mbalimbali umekuwa na mchango mkubwa katika kufanikisha utekelezaji wa majukumu ya Wizara. Ninawapongeza pia Wenyeviti wa Kamati nyingine za Kudumu za Bunge kwa kuendelea kutekeleza majukumu yao kikamilifu.
- Mheshimiwa Spika, naomba nitumie fursa hii kuwapongeza Mhe. Dkt. Stergomena Lawrence Tax kwa kuteuliwa kuwa Mbunge na Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa; Mhe. Emmanuel Peter Cherehani kwa kuchaguliwa kuwa Mbunge wa Jimbo la Ushetu; Mhe. Emmanuel Lekishon Shangai kwa kuchaguliwa kuwa Mbunge wa Jimbo la Ngorongoro; na Mhe. Shamsi Vuai Nahodha kwa kuteuliwa kuwa Mbunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
- Mheshimiwa Spika, napenda kumshukuru Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuendelea kuniamini na viongozi wenzangu, Mheshimiwa Balozi Mbarouk Nassor Mbarouk,
Naibu Waziri; Balozi Joseph Edward Sokoine, Katibu Mkuu; na Balozi Fatma Mohammed Rajab Naibu Katibu Mkuu, kuiongoza Wizara hii. Naomba pia niwapongeze watumishi wote wa Wizara na Taasisi kwa mchango wao katika kufanikisha majukumu ya Wizara. Tunaahidi kuendelea kufanya kazi kwa weledi na utumishi uliotukuka ili kuleta maendeleo katika Taifa letu.
- Mheshimiwa Spika, kipekee ninapenda kumshukuru mume wangu mpendwa Mhandisi Dkt. George Steven Mulamula; watoto wangu pamoja na familia yangu kwa uvumilivu wao, na kuendelea kunipa moyo katika kutekeleza majukumu yangu ambayo mara nyingi yananilazimu kuwa mbali nao kwa muda mrefu. Mungu awabariki sana.
- Mheshimiwa Spika, ninapenda kutumia fursa hii kumpongeza Mheshimiwa Kassim Majaliwa Majaliwa (Mb.), Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa hotuba yake nzuri aliyowasilisha hapa Bungeni ambayo imetoa dira na mwongozo wa utekelezaji wa shughuli za Serikali kwa mwaka wa fedha 2022/2023. Nawapongeza pia Waheshimiwa Mawaziri wenzangu walionitangulia kuwasilisha hotuba zao katika Bunge hili la Bajeti.
- Mheshimiwa Spika, naomba kutoa pole kwako na Bunge lako tukufu kwa kuondokewa na wapendwa wetu, Mhe. Elias Kwandikwa, aliyekuwa Mbunge wa Jimbo la Ushetu na Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa; Mhe. William Tate Ole Nasha aliyekuwa Mbunge wa Jimbo la
Ngorongoro na Naibu Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Uwekezaji); na Mhe. Irene Ndyamkama aliyekuwa Mbunge wa Viti Maalum Mkoa wa Rukwa. Nitoe pia pole kwa familia, ndugu, jamaa, marafiki na Watanzania wenzangu kwa kuondokewa na wapendwa wetu.
- Mheshimiwa Spika, ninashukuru kwa salamu za rambirambi kutoka kwa Waheshimiwa Wabunge, Viongozi wa Serikali, Jumuiya ya
Wanadiplomasia hapa nchini na Washirika wa
Maendeleo kufuatia kifo cha Balozi Edwin
Rutageruka aliyekuwa Mkurugenzi wa Idara ya Diplomasia ya Uchumi Wizarani. Tunatambua na kuthamini upendo na faraja katika kipindi hicho kigumu.
- Mheshimiwa Spika, ninapenda kutoa salamu za pole kwa Mheshimiwa Uhuru Muigai Kenyatta, Rais wa Jamhuri ya Kenya, familia na Wakenya wote kwa kuondokewa na Mheshimiwa
Emilio Mwai Kibaki aliyekuwa Rais wa Awamu ya Tatu aliyefariki tarehe 22 Aprili 2022. Aidha, ninatoa salamu za pole kwa Mtukufu Sheikh Mohammed bin Zayed Al Nahyan, Rais wa Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE), familia na wananchi wote wa Umoja huo kwa kuondokewa na Mtukufu Sheikh Khalifa bin Zayed bin Sultan Al Nahyan aliyekuwa Rais wa Pili wa UAE aliyefariki tarehe 13 Mei 2022. Kadhalika, ninatoa salamu za pole kwa Mheshimiwa Yoweri Kaguta Museveni Rais wa Jamhuri ya Uganda, Spika wa Bunge la nchi hiyo, familia, ndugu na jamaa kwa kuondokewa Mhe. Jacob L’ Okori Oulanyah aliyekuwa Spika wa Bunge la Jamhuri ya Uganda. Tunaomba Mwenyezi Mungu azilaze roho zao mahali pema, Amina.
2.0 TANZANIA NA UHUSIANO WA KIMATAIFA
- Mheshimiwa Spika, Tanzania imeendelea kuwa na ushawishi katika Jumuiya ya Kimataifa na kusimamia misingi madhubuti iliyowekwa na Waasisi wa Taifa letu katika uhusiano wa kimataifa ambayo inapinga na kulaani vitendo vya uonevu na ukandamizaji popote duniani, kulinda uhuru na kujiamulia mambo yetu wenyewe; kulinda mipaka ya nchi yetu; kutetea haki; kuimarisha ujirani mwema; na kutekeleza sera ya kutofungamana na upande wowote kama dira na msimamo wetu kwenye uhusiano na nchi nyingine katika Jumuiya ya Kimataifa.
- Mheshimiwa Spika, ninapenda kulifahamisha Bunge lako kuwa Wizara imekamilisha mapendekezo ya Sera ya Mambo ya Nje ya Mwaka 2022 ambayo ipo katika hatua za kuridhiwa ndani ya Serikali. Mapendekezo ya Sera hiyo yamezingatia maslahi mapana ya Taifa ikiwa ni pamoja na misingi ya Taifa letu, ujirani mwema, diplomasia ya uchumi, uchumi wa buluu, masuala ya Diaspora, mabadiliko ya tabianchi na kubidhaisha Kiswahili. Mapendekezo ya Sera hii, yataendelea kuimarisha uchumi kupitia uhusiano na ushirikiano kati ya Tanzania na nchi nyingine, jumuiya za kikanda na kimataifa.
- Mheshimiwa Spika, pamoja na kutoa kipaumbele cha kujumuisha masuala ya Diaspora kwenye Sera mpya, na kwa kutambua ombi la Diaspora la muda mrefu la kutaka uraia pacha,
Wizara kwa kushirikiana na wadau mbalimbali imeandaa Andiko lenye mapendekezo yanayohusisha maoni mahsusi ya Diaspora. Andiko hilo litatoa mwongozo wa masuala ya Diaspora ikiwemo Hadhi Maalum.
3.0 HALI YA SIASA, ULINZI NA USALAMA
- Msheshimiwa Spika, hali ya siasa, ulinzi na usalama imeendelea kuimarika katika maeneo mengi duniani. Licha ya changamoto ya vita baina ya Urusi na Ukraine iliyosababisha mtikisiko wa uchumi duniani. Katika kipindi cha Mwaka wa Fedha 2021/2022, nchi mbalimbali zilifanya chaguzi kwa utulivu, uhuru na amani. Tunawapongeza viongozi waliochaguliwa na tunaahidi kuendelea kushirikiana na Serikali zao.
- Msheshimiwa Spika, ninaomba kutoa taarifa fupi kuhusu hali ya siasa, ulinzi na usalama kama ifuatavyo:
3.1Afrika
19. Mheshimiwa Spika, hali ya siasa, ulinzi na usalama imeendelea kuimarika barani Afrika, isipokuwa katika baadhi ya nchi zenye changamoto za kisiasa na kiusalama zilizosababishwa na uwepo wa makundi ya waasi, mashambulizi ya kigaidi na mapinduzi ya kijeshi. Baadhi ya nchi hizo ni:
Ethiopia
20. Mheshimiwa Spika, mapigano ya wenyewe kwa wenyewe nchini Ethiopia yameendelea kuzorotesha hali ya usalama nchini humo, ambapo vikosi vya Serikali ya Shirikisho la
Ethiopia vilikabiliana kijeshi na vikosi vya jeshi la Jimbo la Tigray. Tanzania inaunga mkono juhudi za jumuiya ya kimataifa katika kusitisha mapigano kwa njia ya mazungumzo ya amani kurejesha amani nchini humo.
Jamhuri ya Afrika ya Kati
21. Mheshimiwa Spika, kikundi cha waasi cha Seleka kimeendelea kufanya mashambulizi dhidi ya majeshi ya Serikali ya Jamhuri ya Afrika ya Kati hasa katika miji ya Bangui na Bassangoa. Tanzania inaendelea kuunga mkono juhudi zinazofanywa na jumuiya ya kimataifa katika kutafuta suluhu ya mgogoro huo ikiwemo kuimarisha ulinzi na usalama wa nchi hiyo kwa kuchangia vikosi vya kijeshi kwenye Misheni ya Umoja wa Mataifa ya Ulinzi wa Amani ya Afrika ya Kati (MINUSCA).
Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC)
22. Mheshimiwa Spika, hali ya usalama nchini DRC imeendelea kuwa tulivu katika maeneo mengi isipokuwa katika majimbo ya Kivu Kaskazini, Ituri na Kivu Kusini yaliyopo mashariki mwa nchi hiyo. Vikundi vya waasi vikiwemo M23, Cooperative for Development of Congo (CODECO) na Allied Democratic Forces (ADF) viliendelea kufanya mashambulizi ya kutumia silaha dhidi ya wananchi, majeshi ya Serikali na vikosi vya walinda amani. Tanzania inaendelea kuungana na jumuiya ya kimataifa katika kusaidiana kuleta amani nchini DRC kupitia SADC na kwa kuchangia vikosi vya kijeshi kwenye Misheni ya Umoja wa Mataifa ya Ulinzi wa Amani DRC (MONUSCO).
Msumbiji
- Mheshimiwa Spika, hali ya usalama nchini Msumbiji imeendelea kuwa tulivu katika maeneo mengi isipokuwa katika Jimbo la Cabo Delgado lililopo kaskazini mwa nchi hiyo. Jimbo hilo limeendelea kukabiliwa na changamoto ya kiusalama zinaosababishwa na mashambulizi ya kigaidi yanayofanywa na kikundi cha Ansaar AlSunna wal Jamaa. Tanzania imeendelea kushirikiana na nchi nyingine wanachama wa SADC kurejesha hali ya usalama na amani nchini Msumbiji kwa kuchangia vikosi vya walinda amani katika Misheni ya SADC nchini Msumbiji (SAMIM).
- Mheshimiwa Spika, aidha, mwezi Agosti 2021 Zambia ilifanya Uchaguzi Mkuu uliompa ushindi Mheshimiwa Hakainde Hichilema wa Chama cha United Party for National Development.
Ninatumia fursa hii kumpongeza Mheshimiwa Hichilema kwa ushindi alioupata pamoja na wananchi wa Zambia kwa kufanya uchaguzi huo kwa amani na utulivu. Serikali ya Tanzania itaendelea kushirikiana na Serikali yake katika kudumisha uhusiano kati ya nchi hizi mbili.
3.2Mashariki ya Kati
25. Mheshimiwa Spika, eneo la mashariki ya kati limeendelea kukabiliwa na migogoro ya kisiasa na mapigano katika baadhi ya mataifa hali ambayo imeendelea kudhoofisha usalama wa eneo hilo kama ifuatavyo:
Yemen
26. Mheshimiwa Spika, hali ya usalama nchini Yemen haijatengamaa kutokana na mapigano yanayoendelea kati ya jeshi la Serikali na kundi la wanamgambo wa Houthi. Tunapongeza usitishwaji wa mapigano katika kipindi cha mwezi Mtukufu wa Ramadhan, na ni matumaini yetu kuwa hatua hii itakuwa chachu ya kufikia amani ya kudumu kwa taifa hilo. Tanzania inaendelea kuunga mkono msimamo wa Umoja wa Mataifa unaozitaka pande zote zinazohasimiana kutafuta suluhu ya mgogoro huo kwa njia ya majadiliano.
Lebanon
27. Mheshimiwa Spika, Lebanon imeendelea kukabiliwa na changamoto za kisiasa, mdororo wa kiuchumi, ulinzi na usalama ambazo zimesababisha machafuko ya mara kwa mara nchini humo. Tanzania inaendelea kuunga mkono juhudi za jumuiya ya kimataifa katika kuleta amani na usalama Lebanon, ikiwemo kuchangia vikosi vya kijeshi katika misheni ya kulinda amani ya Umoja wa Mataifa nchini humo (UNIFIL).
Israel na Palestina
28. Mheshimiwa Spika, mgogoro kati ya Israel na Palestina umedumu kwa miongo mingi, ambapo mataifa hayo yameendelea kuwa na mapigano ya mara kwa mara yanayochangia kudhoofisha hali ya usalama katika eneo hilo. Tanzania inaendelea kuunga mkono maazimio ya
Umoja wa Mataifa na Umoja wa Afrika yanayozitaka pande husika kuheshimu makubaliano ya kuwepo kwa nchi mbili katika eneo hilo ambazo ni Palestina huru na Israel salama.
3.3Ulaya na Amerika
- Mheshimiwa Spika, kiujumla hali ya siasa, ulinzi na usalama katika ukanda wa Ulaya na Amerika imeendelea kuwa ya utulivu na amani isipokuwa vita kati ya Shirikisho la Urusi na Jamhuri ya Ukraine iliyoanza mwezi Februari 2022. Hatua hiyo imechangia kuzorota kwa hali ya usalama katika eneo la mashariki ya Ulaya. Vita hiyo imesababisha athari hasi katika uchumi wa dunia, ambapo nchi nyingi ikiwemo Tanzania zimeshuhudia kuongezeka kwa bei za bidhaa mbalimbali hususan bidhaa za nafaka, nishati ya mafuta na gesi. Hali hiyo, inatokana na nchi hizo kuwa miongoni mwa wazalishaji wakubwa wa bidhaa hizo duniani.
- Mheshimiwa Spika, Tanzania inaendelea kuunga mkono juhudi za jumuiya ya kimataifa za kutafuta suluhu ya mgogoro huo kwa njia ya majadiliano baina ya pande mbili zinazohasimiana kwa lengo la kurejesha amani na usalama.
- Mheshimiwa Spika, mwezi Aprili 2022,
Ufaransa ilifanya Uchaguzi Mkuu uliompa ushindi Mheshimiwa Emmanuel Macron kutoka Chama cha La République en Marche na kuendelea kushika kiti cha Urais kwa muhula wa pili.
Ninapenda kutumia fursa hii kumpongeza Mheshimiwa Macron kwa ushindi alioupata pamoja na wananchi wa Ufaransa kwa kufanya uchaguzi huo kwa amani na utulivu. Serikali ya Tanzania itaendelea kushirikiana na Serikali yake katika kudumisha uhusiano kati ya nchi hizi mbili.
3.4Asia na Australasia
- Mheshimiwa Spika, hali ya siasa, ulinzi na usalama katika ukanda wa Asia na Australasia iliendelea kuwa salama na tulivu licha ya uwepo wa mivutano ya kisiasa baina ya mataifa ya Pakistan na India; na Jamhuri ya Korea na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Watu wa Korea. Tanzania inaendelea kuzisihii pande zinazohasimiana kutafuta suluu ya migogoro hiyo kwa njia ya amani.
- Mheshimiwa Spika, baada ya kutoa maelezo ya utangulizi, misingi ya sera na hali ya dunia, ninaomba sasa kuwasilisha taarifa ya utekelezaji wa mpango na bajeti ya wizara kwa mwaka wa fedha 2021/2022 na makadirio ya mapato na matumizi kwa mwaka wa fedha 2022/2023.
4.0 MAPITIO YA UTEKELEZAJI WA MPANGO NA
BAJETI YA WIZARA KWA MWAKA WA
FEDHA 2021/2022
- Mheshimiwa Spika, kabla ya kueleza utekelezaji wa Mpango na Bajeti ya Wizara kwa mwaka wa fedha 2021/2022, naomba nitaje majukumu ya Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki kama yalivyoainishwa katika Muundo wa Wizara Toleo la tarehe 4 Februari, 2022 kama ifuatavyo:
- Kubuni na kusimamia utekelezaji wa Sera ya Nchi ya Mambo ya Nje;
- Kusimamia na kuratibu masuala ya uhusiano baina ya Tanzania na nchi
nyingine;
- Kusimamia na kuratibu masuala ya mikataba na makubaliano ya kimataifa;
- Kusimamia masuala yanayohusu kinga na haki za wanadiplomasia waliopo nchini;
- Kusimamia na kuratibu masuala ya itifaki na uwakilishi;
- Kuanzisha na kusimamia huduma za kikonseli;
- Kuratibu masuala ya ushirikiano wa kikanda na kimataifa;
- Kuratibu na kusimamia masuala ya watanzania wanaoishi ughaibuni;
- Kuratibu na kusimamia utekelezaji wa masuala ya Jumuiya ya Afrika Mashariki;
- Kuratibu biashara ya kimataifa na diplomasia uchumi;
- Kuratibu na kusimamia miradi ya
maendeleo ya taasisi zilizo chini ya Wizara; na
- Kusimamia utawala na maendeleo ya watumishi Wizarani na katika Balozi za Tanzania.
- Mheshimiwa Spika, utekelezaji wa majukumu ya Wizara ulizingatia sera, sheria na miongozo mbalimbali ya kitaifa, kikanda na kimataifa ikiwemo Dira ya Taifa ya Maendeleo ya mwaka 2025; Mpango wa Tatu wa Taifa wa Maendeleo wa Miaka Mitano (2021/22 – 2025/26); Ilani ya Chama cha Mapinduzi kwa Ajili ya Uchaguzi Mkuu wa Mwaka 2020; Sera ya Mambo ya Nje ya Mwaka 2001; Sheria ya Bajeti Na. 11 ya mwaka 2015; Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022; Ajenda ya 2030 ya Umoja wa Mataifa ya Malengo ya Maendeleo Endelevu; Ajenda ya 2063 ya Umoja wa Afrika; Mkataba wa
Uanzishwaji wa Jumuiya ya Afrika Mashariki wa mwaka 1999 na Itifaki zake; Mkataba wa Uanzishwaji wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) wa mwaka 1992 na Itifaki zake; Mkakati wa Maendeleo wa Jumuiya ya Afrika
Mashariki 2017/2018 – 2021/2022; na Mpango Mkakati Elekezi wa Maendeleo wa SADC 2020 –
2030.
- Mheshimiwa Spika, utekelezaji wa majukumu ulizingatia pia maoni na ushauri wa Waheshimiwa Wabunge wakati wa kujadili Mpango na Bajeti ya Wizara kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022; Mpango Mkakati wa Wizara wa mwaka 2021/2022 – 2025/2026; na maagizo yaliyotolewa kwa nyakati tofauti kwa Wizara na Viongozi wa Kitaifa, Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama na Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali.
4.1Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha
2021/2022
4.1.1 Mapato
- Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2021/2022, Wizara ilipanga kukusanya Shilingi
2,550,879,000. Kati ya kiasi hicho, Shilingi 47,240,000 ni makusanyo ya Makao Makuu ya Wizara na Shilingi 2,503,639,000 ni makusanyo kutoka Balozi za Tanzania nje. Vyanzo vya mapato hayo ni pamoja na uthibitisho wa nyaraka, pango la majengo ya Serikali nje ya nchi na mauzo ya zabuni.
- Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha Julai 2021 hadi Aprili 2022 Wizara imekusanya jumla ya Shilingi 854,335,191.66 sawa na asilimia 33 ya lengo lililopangwa kwa mwaka 2021/2022. Kupungua kwa mapato hayo kumetokana na kukosekana kwa wapangaji katika baadhi ya majengo ya Serikali kwenye Balozi za Tanzania nje ya nchi. Hali hii imesababishwa na uwepo wa janga la UVIKO-19 uliosababisha biashara nyingi katika nchi mbalimbali kufungwa. Fedha zote za maduhuli zilizokusanywa na wizara ziliingizwa moja kwa moja kwenye Mfuko Mkuu wa Serikali kama taratibu zinavyoelekeza.
4.1.2 Fedha Zilizoidhinishwa
39. Mheshimiwa Spika, katika kutekeleza malengo ya Wizara kwa mwaka wa fedha
2021/2022, kiasi cha Shilingi 192,265,438,000 kiliidhinishwa. Kati ya fedha hizo, Shilingi 178,765,438,000 ni kwa ajili ya matumizi ya kawaida na Shilingi 13,500,000,000 ni kwa ajili ya miradi ya maendeleo. Katika fedha zilizotengwa kwa matumizi ya kawaida, Shilingi 167,937,219,000 ni kwa ajili ya matumizi mengineyo na Shilingi 10,828,219,000 ni kwa ajili ya mishahara.
4.1.3 Matumizi
- Mheshimiwa Spika, hadi kufikia mwezi Aprili 2022 Wizara imepokea kutoka HAZINA kiasi cha Shilingi 174,640,751,594.47. Kiasi hicho cha fedha ni sawa na asilimia 90.8 ya fedha zote za bajeti zilizoidhinishwa katika mwaka wa fedha 2021/2022. Kati ya fedha hizo, Shilingi 163,186,284,122.63 ni kwa ajili ya matumizi mengineyo sawa na asilimia 97.2 na Shilingi 11,454,467,471.84 ni kwa ajili ya mishahara sawa na asilimia 105.8.
- Mheshimiwa Spika, hadi kufikia mwezi
Aprili 2022, Wizara ilitumia kiasi cha Shilingi 174,640,751,594.47. Kiasi hicho cha fedha ni sawa na asilimia 100 ya fedha zilizopokelewa. Kati ya fedha hizo, Shilingi 163,186,284,122.63 ni kwa ajili ya matumizi mengineyo na Shilingi 11,454,467,471.84 ni kwa ajili ya mishahara sawa na asilimia 105.8. Ongezeko hilo linatokana na watumishi waliohamishiwa Wizarani kutoka Wizara na taasisi nyingine za Serikali pamoja na kupandishwa vyeo kwa watumishi.
- Mheshimiwa Spika, baada ya kutaja majukumu ya Wizara, miongozo mbalimbali iliyozingatiwa katika utekelezaji wa majukumu pamoja na taarifa ya mapato na matumizi kwa mwaka wa fedha 2021/2022, ninaomba nitumie fursa hii kueleza kwa kifupi mapitio ya utekelezaji wa majukumu ya Wizara katika kipindi husika kama ifuatavyo:
4.2 Kusimamia na Kuratibu Masuala ya Uhusiano Baina ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Nchi Nyingine
43. Mheshimiwa Spika, Wizara iliratibu ushirikiano na uhusiano baina ya Tanzania na nchi nyingine duniani katika nyanja za kiuchumi, kisiasa na kijamii kama ifuatavyo:
4.2.1 Ushirikiano wa Tanzania na Nchi za Afrika
- Mheshimiwa Spika, mwezi Mei 2022, Wizara iliratibu na kufanikisha ziara rasmi ya Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania nchini Uganda kwa mwaliko wa Mheshimiwa Yoweri Kaguta Museveni, Rais wa Jamhuri ya Uganda. Wakati wa ziara hiyo nchi hizi mbili zilisaini hati mbili za makubaliano ya ushirikiano kuhusu ujenzi wa njia ya kusafirishia umeme wa kV 400 kutoka Masaka hadi Mwanza na masuala ya ulinzi na usalama. Vilevile, Tanzania na Uganda zilikubaliana kushirikiana katika uzalishaji wa chanjo na dawa za binadamu na mifugo.
- Mheshimiwa Spika, makubaliano mengine ni kufunguliwa upya kwa njia ya usafirishaji wa mizigo kutoka Mwanza hadi Port Bell Uganda kupitia ziwa Victoria ambayo itapunguza gharama za kufanya biashara ambapo idadi ya siku za kusafirisha mizigo itapungua kutoka wastani wa siku 9 hadi 4. Kupitia makubaliano hayo Tanzania itaanza kununua dawa za kufubaza Virusi vya UKIMWI (ARV) na Uganda imeahidi kutuma tani 10,000 za sukari ili kufidia upungufu wa bidhaa hiyo nchini. Wizara itaendelea kufuatilia utekelezaji wa hati hizo.
- Mheshimiwa Spika, mwezi Februari 2022, Wizara iliratibu na kufanikisha ushiriki wa Tanzania katika Mkutano wa Sita wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Afrika na Umoja wa Ulaya uliofanyika jijini Brussels, Ubelgiji. Katika mkutano huo, Umoja wa Ulaya uliahidi kutenga fedha kiasi cha Euro bilioni 150 kwa ajili ya kufadhili utekelezaji wa miradi ya maendeleo barani Afrika hususan sekta za nishati ya umeme, TEHAMA na uchukuzi ili kuchochea maendeleo ya bara hilo. Aidha, ufadhili huo unalenga kuchagiza utekelezaji wa Mkataba wa Eneo Huru la Biashara Barani Afrika (AfCFTA). Wizara inaendelea kufuatilia hatua zaidi za utekelezaji wa ahadi hiyo ya Umoja wa Ulaya.
- Mheshimiwa Spika, mwezi Januari, 2022 Wizara iliratibu na kufanikisha Mkutano wa Nne wa Tume ya Pamoja ya Kudumu ya Ushirikiano kati ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Jamhuri ya Uganda uliofanyika jijini Kampala, Uganda. Katika mkutano huo, Hati sita za Makubaliano ya ushirikiano katika maeneo ya habari; huduma za jamii, utamaduni na sanaa; mifugo na uvuvi; menejimenti ya utumishi wa umma; elimu na michezo; na afya zilijadiliwa. Majadiliano ya kukamilisha kusainiwa kwa hati hizo yanaendelea.
- Mheshimiwa Spika, mwezi Januari 2022, Wizara iliratibu na kufanikisha kusainiwa kwa
Hati ya Makubaliano ya ushirikiano baina ya Tanzania, Burundi na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) kuhusu ujenzi wa reli ya kisasa (SGR) kati ya Uvinza – Musongati – Gitega – Kindu.
Utekelezaji wa mradi huo utainufaisha nchi yetu kiuchumi kwa kuzingatia kuwa nchi za Burundi na DRC zinatumia Bandari ya Dar es Salaam kusafirisha sehemu kubwa ya shehena za mizigo. Ujenzi wa reli hiyo utarahisisha huduma ya uchukuzi na kukuza uhusiano wa kibiashara baina ya nchi hizo.
- Mheshimiwa Spika, mwezi Desemba 2021, Wizara iliratibu na kufanikisha ziara ya
Mheshimiwa Uhuru Muigai Kenyatta, Rais wa Jamhuri ya Kenya hapa nchini kufuatia mwaliko wa Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuwa mgeni rasmi katika maadhimisho ya miaka 60 ya uhuru wa Tanzania Bara. Aidha, kupitia ziara hiyo, nchi hizi mbili zimeendelea kuimarisha uhusiano na ushirikiano wa kiuchumi, kisiasa na kijamii.
- Mheshimiwa Spika, mwezi Novemba 2021, Wizara iliratibu na kufanikisha ziara ya
Mheshimiwa Yoweri Kaguta Museveni, Rais wa Jamhuri ya Uganda hapa nchini. Wakati wa ziara hiyo, nchi hizi mbili zilikubaliana kushirikiana katika kukuza na kuimarisha biashara na uwekezaji; kutengeneza chanjo ya kudhibiti UVIKO – 19; kukamilisha utekelezaji wa miradi ya pamoja katika sekta ya nishati na ujenzi wa miundombinu; na masuala ya ulinzi na usalama. Vilevile, Waheshimiwa Marais walishiriki katika kongamano la biashara kati ya Tanzania na
Uganda lililowakutanisha wafanyabiashara kutoka nchi hizi mbili. Kadhalika, akiwa hapa nchini, Mheshimiwa Rais Yoweri Museveni aliikabidhi Serikali shule ya awali na msingi iliyojengwa wilayani Chato, Geita kwa ufadhili wake.
- Mheshimiwa Spika, mwezi Novemba 2021, Wizara iliratibu na kufanikisha ziara ya Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania nchini Misri. Kupitia ziara hiyo, nchi hizi mbili zilisaini Hati za Makubaliano ya Ushirikiano katika elimu na michezo. Aidha, wakati wa ziara hiyo, Mheshimiwa Rais alifanya mazungumzo na wafanyabiashara wakubwa nchini Misri kwa lengo la kuwahamasisha kuwekeza Tanzania. Ninapenda kuliarifu Bunge lako tukufu kuwa, kufuatia ziara hiyo, mnamo mwezi Desemba 2021 ujumbe wa wafanyabiashara 100 kutoka Misri ulitembelea nchini na kushiriki ufunguzi wa kiwanda cha kutengeneza vifaa vya umeme kinachoitwa ElSewedy Electric Company chenye thamani ya Dola za Marekani milioni 35 kilichopo Kigamboni, Dar es Salaam. Kiwanda hicho kitachangia kukuza ajira, mauzo ya nje na kuongeza mapato ya
Serikali.
- Mheshimiwa Spika, mwezi Agosti 2021, Wizara iliratibu na kufanikisha Mkutano wa Nne wa Tume ya Pamoja ya Kudumu ya Ushirikiano kati ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na
Jamhuri ya Kenya uliofanyika jijini Nairobi, Kenya. Kupitia mkutano huo, nchi hizi mbili zilisaini Hati tatu za Makubaliano za Ushirikiano katika maeneo ya elimu ya juu, sayansi na teknolojia; mashauriano ya kisiasa na kidiplomasia; na uhakiki wa mipaka kati ya Tanzania na Kenya.
- Mheshimiwa Spika, mwezi Agosti 2021, Wizara iliratibu na kufanikisha ziara ya
Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania nchini
Rwanda. Ziara hiyo imechangia kuimarisha ujirani mwema kati ya nchi hizi mbili. Aidha, makubaliano yalifikiwa kuhusu kuimarisha ushirikiano katika sekta ya uchukuzi hususan uendelezaji wa miundombinu ya ushoroba wa kati kupitia ujenzi wa reli kutoka lsaka – Rusumo, Tanzania hadi Kigali, Rwanda. Vilevile, nchi hizo zilikubaliana kushirikiana katika kukuza matumizi ya lugha ya Kiswahili ili kuongeza fursa za ajira na biashara.
- Mheshimiwa Spika, vilevile, mwezi Agosti 2021, Wizara iliratibu na kufanikisha Mkutano wa 15 wa Tume ya Pamoja ya Kudumu ya Ushirikiano kati ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Jamhuri ya Rwanda uliofanyika jijini Dar es Salaam. Kupitia mkutano huo, nchi hizi mbili zilisaini Hati nne za Makubaliano ya Ushirikiano katika maeneo ya habari na TEHAMA; elimu; uhamiaji; na udhibiti wa vifaa tiba.
- Mheshimiwa Spika, mwezi Julai 2021, Wizara iliratibu na kufanikisha ziara ya Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania nchini
Burundi. Katika ziara hiyo, Marais wa Tanzania na Burundi walifanya mazungumzo na kushuhudia kusainiwa kwa Hati nane za Makubaliano za Ushirikiano kwenye maeneo ya mashauriano ya kisiasa na kidiplomasia, nishati, madini, uvuvi, ufundishaji wa lugha ya Kiswahili nchini Burundi na Kifaransa nchini Tanzania, kubadilishana wafungwa, kilimo na afya.
- Mheshimiwa Spika, sanjari na hayo, nchi hizi mbili zilikubaliana kuimarisha ushirikiano katika uendelezaji wa miundombinu ya usafiri na uchukuzi ikiwemo ujenzi wa reli kutoka Uvinza, Kigoma kwenda Musongati – Gitega, Burundi. Aidha, ilikubalika kuharakisha utekelezaji wa mradi wa umeme wa Rusumo wa Megawatt 80 unaotekelezwa na Tanzania, Burundi na Rwanda. Vilevile, nchi hizo zilikubaliana kushirikiana katika sekta ya mawasiliano hasa baada ya Burundi kuunganishwa na mtandao wa Mkongo wa Taifa wa Mawasiliano wenye uwezo wa
Gigabaiti 100.
4.2.2 Ushirikiano wa Tanzania na Nchi za Asia
na Australasia
- Mheshimiwa Spika, ninapenda kukufahamisha kuwa mwezi Aprili, 2022 nilifanya ziara ya kikazi nchini Jamhuri ya Korea kufuatia mwaliko rasmi wa Mhe. Chung Eui – Yong, aliyekuwa Waziri wa Mambo ya Nje wa Jamhuri ya Korea. Lengo la ziara hiyo lilikuwa ni kuadhimisha miaka 30 ya uhusiano wa kidiplomasia kati ya Tanzania na Korea ambao ulianzishwa rasmi tarehe 29 Aprili, 1992. Wakati wa ziara hiyo nilifanya mazungumzo na viongozi mbalimbali wa Serikali ya Korea pamoja na viongozi wa Shirika la Ushiriakiano wa Kimataifa la Maendeleo la Korea (KOICA) na benki ya Exim ya Korea. Kufuatia mazungumzo hayo Serikali ya Korea imeahidi kuendelea kutoa misaada yake kwa Tanzania kwa ajili ya kutekeleza miradi ya maendeleo kwa wakati.
- Mheshimiwa Spika, mwezi Februari 2022, Wizara iliratibu na kufanikisha kusainiwa kwa mkataba kati ya Tanzania na Japan wa mkopo wa masharti nafuu wenye thamani ya Yen za Japan bilioni 24.31 kwa ajili ya kutekeleza Mradi wa Uboreshaji wa Barabara ya Arusha-Holili; mkataba kati ya Tanzania na Japan wa mkopo wa masharti nafuu wenye thamani ya Yen za Japan bilioni 10.864 kwa ajili ya kutekeleza Mradi wa
Uboreshaji wa Miundombinu ya Usambazaji wa Maji Mjini Zanzibar; na mkataba kati ya Tanzania na Japan wa msaada wenye thamani ya Yen za Japan bilioni 2.726 kwa ajili ya kutekeleza Mradi wa Ukarabati wa Bandari ya Kigoma. Utekelezaji wa miradi hiyo utachochea maendeleo ya maeneo husika na kusogeza huduma kwa wananchi.
- Mheshimiwa Spika, Wizara iliratibu na kufanikisha upatikanaji wa fedha za ujenzi wa Shule ya Uongozi ya Julius Nyerere iliyopo Kibaha, Pwani. Shule hiyo iliyojengwa kwa ufadhili wa Chama cha Kikomunisti cha China kwa gharama ya Shilingi 101,000,000,000 ilifunguliwa rasmi na Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania mwezi
Februari 2022. Shule hiyo itatoa elimu ya uongozi kwa makada wa Chama cha Mapinduzi na vyama rafiki kutoka ukanda wa kusini mwa Afrika ikiwemo FRELIMO (Msumbiji), ANC (Afrika Kusini), SWAPO (Namibia), ZANU PF (Zimbabwe) na MPLA
(Angola).
- Mheshimiwa Spika, mwezi Novemba 2021, Wizara iliratibu na kufanikisha kusainiwa kwa
Hati ya Makubaliano ya Ushirikiano baina ya Taasisi ya Mifupa Muhimbili (MOI), Hospitali ya Tian Tan na Chama cha Madaktari China (CMA). Kupitia ushirikiano huo, MOI itanufaika na uhawilishaji wa maarifa na uzoefu katika masuala ya tiba kwa njia ya TEHAMA na uchunguzi wa magonjwa. Hatua hiyo itaongeza uwezo wa Tanzania wa kitabibu na kuipunguzia Serikali na watanzania kwa ujumla gharama za matibabu nje ya nchi. Aidha, kuimarika kwa huduma za kitabibu nchini ni kichocheo cha kukua kwa utalii wa tiba kwa kuwa raia kutoka nchi nyingine hususan nchi za jirani watakuja kupata huduma za tiba nchini.
- Mheshimiwa Spika, mwezi Novemba 2021, Wizara iliratibu na kufanikisha uwekezaji wa Kampuni ya Huaxin Cement kutoka nchini China katika kiwanda cha saruji cha Maweni Limestone Limited kilichopo mkoani Tanga. Kampuni ya Huaxin Cement ilinunua kiwanda hicho kutoka kampuni ya Arthi River Mining Group ya Kenya iliyokuwa ikizalisha saruji ya Rhino Cement. Uwekezaji huo umetoa ajira kwa watanzania, kuongeza uzalishaji wa saruji na mauzo ya nje pamoja na kupunguza nakisi ya bidhaa hiyo katika soko la ndani.
- Mheshimiwa Spika, mwezi Novemba 2021, Wizara iliratibu na kufanikisha ushiriki wa
Tanzania kwenye Mkutano wa Mawaziri wa
Jukwaa la Ushirikiano kati ya China na Afrika (FOCAC) uliofanyika Dakar, Senegal. Katika mkutano huo, China na Afrika kwa pamoja ziliandaa Dira ya Ushirikiano ya 2035, ambapo katika miaka mitatu ya mwanzo ya utekelezaji wa Dira hiyo, China itashirikiana na nchi za Afrika kutekeleza programu tisa ambazo ni, programu ya afya na utabibu; programu ya kupunguza umaskini na kuendeleza kilimo; programu ya kukuza biashara; programu ya kukuza uwekezaji; programu ya uvumbuzi wa kidijitali; programu ya mapinduzi ya kijani; programu ya kujenga uwezo; programu ya utamaduni na muingiliano wa watu; na programu ya ulinzi na usalama.
- Mheshimiwa Spika, ninapenda kulieleza Bunge lako tukufu kuwa, Wizara imeratibu na kufanikisha uwasilishaji wa mapendekezo ya awali ya miradi ya Tanzania kwa Serikali ya Jamhuri ya Watu wa China ili kupata ufadhili. Miradi iliyowasilishwa ni mradi wa kufua umeme wa Ruhudji na njia za kusafirishia umeme; mradi wa kufua umeme wa Rumakali na njia za kusafirishia umeme; mradi wa ujenzi wa vyuo saba vya ufundi katika mikoa ya Dodoma, Mwanza, Mbeya, Pwani, Mtwara, Tabora na Arusha; na mradi wa upanuzi wa Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete.
- Mheshimiwa Spika, miradi mingine ni ujenzi wa Chuo cha Taifa cha Usafirishaji; mradi wa ujenzi wa hospitali mkoani Dodoma; mradi wa ujenzi Geopark Ngorongoro – Lengai; na mradi wa uzalishaji wa malisho ya mifugo kwa kutumia teknolojia ya Juncao Tanzania Bara. Miradi mingine iliyowasilishwa ni mradi wa ujenzi wa Hospital ya Rufaa ya Binguni; mradi wa ujenzi wa kituo cha biashara, maonesho na mikutano; mradi wa ujenzi wa maeneo maalumu ya viwanda pamoja na ujenzi wa barabara zenye jumla ya kilometa 110.2 Zanzibar.
- Mheshimiwa Spika, mwezi Novemba 2021, pembezoni mwa Mkutano wa Mawaziri wa FOCAC, Serikali ya Jamhuri ya Watu wa China iliahidi kutoa msaada wa Yuan milioni 100 kwa ajili ya kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo nchini. Wizara inaendelea kufuatilia utekelezaji wa ahadi hiyo.
- Mheshimiwa Spika, mwezi Oktoba 2021, Wizara iliratibu na kufanikisha kusainiwa kwa Mkataba wa kutangaza bidhaa za Tanzania kwenye mtandao wa JD.COM wa China ambao hutembelewa na watu takriban milioni 700 kwa siku. Hatua hiyo, itasaidia kutangaza bidhaa za Tanzania katika soko la China na nchi nyingine ambazo wananchi wake wanautumia zaidi mtandao huo kufanya manunuzi ya bidhaa. Hadi sasa kampuni 57 kutoka Tanzania zimejisajili kwenye mtandao huo.
- Mheshimiwa Spika, mwezi Agosti 2021, Wizara iliratibu na kushiriki katika mkutano wa majadiliano ya kisera kati ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Jamhuri ya Korea uliofanyika jijini Dar es Salaam. Kupitia mkutano huo, Serikali ya Jamhuri ya Korea iliahidi kuipatia Tanzania mkopo wa masharti nafuu wa Dola za Marekani bilioni 1.3 kwa ajili ya kugharamia utekelezaji wa miradi 14 ya maendeleo nchini kwa kipindi cha miaka mitano kuanzia 2021 hadi 2025.
- Mheshimiwa Spika, baadhi ya miradi hiyo ni ujenzi wa makao makuu ya NIDA na ofisi 13 za mikoa za NIDA; mradi wa kuimarisha mipango ya ardhi kwa njia ya kidigitali; mradi wa maji safi na maji taka katika mkoa wa Iringa; mradi wa ujenzi wa chuo cha mafunzo ya reli; na mradi wa ujenzi wa hospitali ya rufaa Binguni na kituo cha mafunzo ya utabibu Zanzibar.
- Mheshimiwa Spika, sanjari na hayo,
ninapenda kulifahamisha Bunge lako tukufu kuwa, Wizara imeratibu na kufanikisha majadiliano kati ya Serikali ya Tanzania na Serikali ya China kuhusu kurejeshwa kwa safari za moja kwa moja za Shirika la Ndege la Tanzania (ATCL) kutoka Dar es Salaam hadi Guangzhou, China. Ninayo furaha kukufahamisha kuwa Serikali ya China imeridhia kurejeshwa kwa safari hizo ambapo ndege za ATCL zitaanza kufanya safari mara moja kwa wiki kati ya Dar es Salaam na Guangzhou.
4.2.3 Ushirikiano wa Tanzania na Nchi za
Mashariki ya Kati
- Mheshimiwa Spika, mwezi Aprili 2022, Wizara iliratibu na kufanikisha Mkutano wa Pili wa Tume ya Pamoja ya Kudumu ya Ushirikiano kati ya Tanzania na Umoja wa Falme za Kiarabu. Kupitia mkutano huo, nchi hizi mbili zilikubaliana kukuza ushirikiano katika masuala ya ulinzi na usalama, mashauriano ya kidiplomasia, misaada ya kibinadamu na maendeleo, biashara, nishati na madini, mawasiliano, uchukuzi, fedha na kilimo na chakula. Taratibu za kukamilisha Hati za Makubaliano katika maeneo ya ushirikiano zinaendelea.
- Mheshimiwa Spika, Wizara iliratibu na kufanikisha ushiriki wa Tanzania katika Maonesho ya Kimataifa ya Dubai (Dubai Expo 2020), yaliyofanyika kuanzia mwezi Oktoba 2021 hadi Machi 2022 Dubai, Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE), na ambayo yalishirikisha nchi 192. Kauli mbiu ya nchi yetu katika maonesho hayo ilikuwa “Tanzania is ready for take off”, ambayo ililenga kuhamasisha uhusiano wa kiuchumi kati ya Tanzania na mataifa mengine hususan katika biashara, uwekezaji, utalii na TEHAMA.
- Mheshimiwa Spika, ninapenda kulitaarifu Bunge lako tukufu kwamba, nchi yetu ilipewa heshima ya kuwa na siku maalum ya Tanzania katika maonesho hayo iliyoadhimishwa tarehe 26 Februari, 2022. Mheshimiwa Samia Suluhu
Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania alikuwa mgeni rasmi katika siku hiyo maalum, ambapo alihutubia viongozi wa serikali, wafanyabiashara, wawekezaji na washiriki wengine wa maonesho hayo. Hotuba hiyo ilirushwa mubashara na kutazamwa na nchi nyingi duniani na hivyo kutoa nafasi kwa nchi yetu kujitangaza vema katika jumuiya ya kimataifa.
- Mheshimiwa Spika, sanjari na maonesho hayo, Wizara iliratibu na kufanikisha kongamano la biashara na uwekezaji kati ya Tanzania na Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE). Kongamano hilo lilikutanisha kampuni kutoka sekta binafsi za nchi hizi mbili. Aidha, jumla ya Hati 37 za Makubaliano ya ushirikiano kati ya Tanzania na UAE zenye thamani ya Shilingi trilioni 18.5 zilisainiwa, ambazo utekelezaji wake utazalisha ajira zipatazo 246,785 katika sekta mbalimbali zikiwemo nishati (mafuta na gesi), kilimo, uzalishaji viwandani, uchukuzi, huduma, mawasiliano na utalii. Hati hizo za makubaliano zilizosainiwa zipo katika hatua mbalimbali za utekelezaji.
- Mheshimiwa Spika, mwezi Machi 2022,
Wizara iliratibu na kufanikisha ziara ya Mhe. Badr Bin Hamad Bin Hamood Al Busaidi, Waziri wa
Mambo ya Nje wa Oman na Mjumbe Maalum wa Mheshimiwa Mtukufu Sultan Haitham Bin Tarik, Mfalme wa Oman. Akiwa nchini Mjumbe huyo alikutana na kufanya mazungumzo na Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; na Mheshimiwa Dkt. Hussein Ali Mwinyi, Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi. Kufuatia mazungumzo hayo, nchi hizi mbili zimekubaliana kufanya Mkutano wa Pili wa Tume ya Pamoja ya Ushirikiano wa Kudumu kati ya Tanzania na Oman kabla ya kukamilika kwa mwaka huu wa fedha.
- Mheshimiwa Spika, mwezi Machi 2022, Wizara iliratibu na kufanikisha upatikanaji wa kibali cha kuuza nyama na bidhaa za nyama ya ng’ombe, mbuzi na kondoo kutoka Tanzania katika soko la Saudi Arabia. Hadi sasa kampuni ya Tanchoice ndiyo imekidhi vigezo na kupata ithibati ya Mamlaka ya Chakula na Dawa ya Saudi Arabia (SFDA) kuuza nyama na bidhaa za nyama nchini humo. Kampuni hiyo pia imepata ithibati ya kuuza nyama na bidhaa za nyama katika nchi ya Jordan. Aidha, kampuni ya Eliya Food inaendelea kufanyia kazi mapendekezo ya SFDA ili nayo iweze kupata ithibati. Hatua hiyo inatarajiwa kukuza mauzo ya nchi yetu nje, kuongeza mapato ya Serikali na kuinua kipato cha wafugaji nchini. Kadhalika, Saudi Arabia imeonesha nia ya kushiriki katika Maonesho ya 46 ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam mwezi Julai 2022.
- Mheshimiwa Spika, mwezi Machi 2022 nilifanya ziara ya kikazi nchini Saudi Arabia kwa mwaliko wa Mwana Mfalme Mtukufu Faisal bin Farhan Al Saud, Waziri wa Mambo ya Nje wa nchi hiyo. Ziara hiyo ililenga kukuza na kuimarisha uhusiano wa kidiplomasia kati ya Tanzania na Saudi Arabia. Katika ziara hiyo niliambatana na
Mhe. Mashimba Ndaki (Mb), Waziri wa Mifugo na Uvuvi na Mhe. Dkt. Damas Ndumbaro (Mb), wakati huo akiwa Waziri wa Maliasili na Utalii. Tukiwa nchini humo, tulifanya mikutano na
Waziri wa Mambo ya Nje, Waziri wa Biashara na
Naibu Waziri wa Kilimo pamoja na viongozi wa
Jumuiya ya Wafanyabiashara na Wenye Viwanda Saudi Arabia na kuelezea fursa za biashara na uwekezaji zilizopo nchini katika sekta za mifugo, uvuvi, kilimo, utalii na usafiri wa anga. Aidha, tuliwahamasisha wafanyabiashara wa Jumuiya hiyo kushiriki katika Maonesho ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam (Sabasaba) yanayofanyika mwezi Julai kila mwaka.
- Mheshimiwa Spika, mwezi Februari 2022, Wizara iliratibu na kufanikisha kikao cha pamoja kati ya Tanzania na Qatar kujadili utekelezaji wa mkataba wa ushirikiano kati ya nchi hizi mbili kuhusu ajira kwa watanzania nchini Qatar uliosainiwa mwaka 2014 kilichofanyika jijini Dar es Salaam. Kupitia kikao hicho, Tanzania na Qatar zilikubaliana kutatua changamoto zilizokuwa zinakwamisha utekelezaji wa mkataba huo zikiwemo masuala ya viza na usajili wa mawakala binafsi wa ajira.
- Mheshimiwa Spika, makubaliano hayo yamewezesha mawakala binafsi wa ajira kutoka Tanzania kwenda Qatar kufanya mazungumzo na mawakala binafsi wa ajira katika nchi hiyo kuhusu fursa za ajira kwa watanzania nchini Qatar hususan wakati huu ambapo nchi hiyo itakuwa mwenyeji wa mashindano ya kombe la dunia la mpira wa miguu yatakayofanyika mwezi Novemba na Desemba 2022. Serikali itaendelea kuweka mazingira mazuri kwa watanzania kupata fursa za ajira nje ya nchi na kuhakikisha kuwa ajira hizo zinakuwa rasmi na zenye staha ili kulinda maslahi yao.
- Mheshimiwa Spika, mwezi Januari 2022,
Wizara iliratibu ziara ya kikazi ya Mheshimiwa Dkt.
Hussein Ali Mwinyi, Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi katika Umoja wa Falme za Kiarabu. Katika ziara hiyo
Mheshimiwa Dkt. Mwinyi alishuhudia kusainiwa kwa makubaliano kati ya Serikali ya Mapinduzi Zanzibar na kampuni ya Eagle Hills Regional Properties ya Umoja wa Falme za Kiarabu kuhusu ujenzi wa hoteli ya nyota tano eneo la Kizingo, Zanzibar. Uwekezaji huo ni sehemu ya utekelezaji wa sera ya uchumi wa buluu inayolenga kukuza uchumi na kuinua kipato kwa wananchi.
- Mheshimiwa Spika, mwezi Desemba 2021, Wizara iliratibu na kufanikisha ziara ya ujumbe wa madaktari bingwa 27 wa moyo kutoka nchini Saudi Arabia waliotembelea nchini kwa lengo la kutoa huduma za upasuaji wa moyo kwa katika Taasisi ya Magonjwa ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI), jijini Dar es Salaam. Kufuatia ziara hiyo watoto wapatao 100 walifanyiwa vipimo vya maradhi ya moyo na watoto 34 kati yao walifanyiwa upasuaji.
- Mheshimiwa Spika, mwezi Oktoba 2021, Wizara iliratibu na kufanikisha ziara ya Dkt. Sidi Ould Tah, Mkurugenzi Mkuu wa Benki ya Kiarabu ya Maendeleo ya Uchumi Afrika (BADEA) hapa nchini. Kupitia ziara hiyo, BADEA iliidhinisha nyongeza ya mkopo wa masharti nafuu kiasi cha Dola za Marekani milioni 1.4 kwa ajili ya ujenzi wa barabara ya Wete – Chake yenye urefu wa kilomita 22.1; upanuzi na ukarabati wa Hospitali ya Rufaa ya Mnazi Mmoja; na ujenzi wa shule tatu za sekondari za ufundi. Kwa hatua hiyo, jumla ya mkopo uliotolewa na Benki hiyo kwa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar umefikia Dola za Marekani milioni 21.4.
- Mheshimiwa Spika, Wizara imeratibu na kufanikisha upatikanaji wa ajira 600 kwa vijana wa kitanzania katika Bandari ya Dubai (DP World) ambapo hadi sasa vijana 90 wamefaulu usaili na kuwasili Dubai, Umoja wa Falme za Kiarabu kwa ajili ya kuanza kazi. Vilevile, Wizara iliratibu na kufanikisha vijana 80 kwenda kushiriki mafunzo ya utarajali wa kilimo na mifugo nchini Israel. Vijana hao wanatarajiwa kukamilisha mafunzo hayo na kurejea nchini mwezi Septemba 2022.
- Mheshimiwa Spika, kati ya mwezi Agosti 2021 hadi Aprili, 2022 Wizara iliratibu na kufanikisha ujio wa watalii 4,500 kutoka Israel. Ujio wa watalii hao ni matokeo ya juhudi kubwa zilizofanywa na Serikali kwa kushirikiana na wadau wa utalii wa kutoka Israel na hapa nchini.
4.2.4 Ushirikiano wa Tanzania na Nchi za Ulaya
na Amerika
- Mheshimiwa Spika, mwezi Aprili, 2022, Wizara iliratibu na kufanikisha ziara ya
Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania nchini Marekani. Akiwa nchini humo, Mheshimiwa Rais alizindua filamu maalum ya kutangaza utalii wa Tanzania iliyopewa jina la “Royal Tour” ambayo yeye mwenyewe alishiriki katika uandaaji wake. Tanzania inakuwa nchi ya tisa duniani na ya pili Afrika kuandaa filamu kama hiyo. Aidha, filamu hiyo inatarajiwa kuwa chachu katika kuvutia wawekezaji na watalii wengi zaidi kutoka sehemu mbalimbali duniani.
- Mheshimiwa Spika, wakati wa ziara hiyo, Wizara iliratibu na kufanikisha mazungumzo baina ya Mheshimiwa Rais na Mheshimiwa Kamala Harris, Makamu wa Rais wa Marekani yaliyofanyika katika Ikulu ya Marekani. Viongozi hawa wakuu walikubaliana kuendelea kuimarisha uhusiano kati ya nchi hizi mbili uliodumu kwa miaka 60.
- Mheshimiwa Spika, vilevile, wakati wa ziara hiyo, Wizara iliratibu na kufanikisha kusainiwa kwa hati za makubaliano saba ya uwekezaji yenye thamani ya Dola za Marekani bilioni 5.04. Utekelezaji wa mikataba hiyo unatarajiwa kuzalisha ajira zipatazo 301,110 hapa nchini katika sekta mbalimbali zikiwemo sekta za kilimo, utalii na biashara. Mikataba iliyosainiwa ni kama ifuatavyo: Mkataba kati ya Kampuni ya Taifa Group na Kampuni ya Northern Feed ya Marekani kukuza kilimo cha umwagiliaji cha mazao ya soya, alizeti na miwa; Shirikisho la Wenye Viwanda Tanzania na Corporate Council on Africa kukuza ushirikiano wa kuwajengea uwezo wajasiriamali wadogo na wa kati.
- Mheshimiwa Spika, Mikataba mingine ni kati ya Wizara ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara na Kampuni ya Daaya Group Ltd kuwekeza katika mnyororo wa thamani wa sekta ya utalii; Mamlaka ya Maendeleo ya Biashara Tanzania na Chama cha Wafanyabiashara cha Marekani kuimarisha biashara na uwekezaji kati ya Tanzania na Marekani; Tanzania Mercantile Exchange (TMX) na
STONEX Financial Inc. kwa kushirikiana na Kampuni ya SJS Ltd na Tanzania Electronic Market Exchange kuimarisha uwezo wa TMX; Wizara ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara na FE Jordan & Associates kuendeleza maeneo maalum ya uzalishaji; na Wizara ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara na Kampuni ya WABI International Ltd kuendeleza uwekezaji katika sekta ya nyumba na huduma za malazi.
- Mheshimiwa Spika, mwezi Februari 2022, Wizara iliratibu na kufanikisha ziara ya
Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania nchini Ufaransa. Akiwa nchini humo, Mheshimiwa Rais alishiriki katika Mkutano wa Wakuu wa Nchi na Serikali kuhusu Bahari Kuu (One Ocean Summit) uliofanyika nchini Ufaransa. Mheshimiwa Rais Samia pia alifanya mazungumzo na Jumuiya ya Wafanyabiashara wa Ufaransa (MEDEF) kwa lengo la kuwahamasisha kuwekeza hapa nchini katika sekta mbalimbali na kuitangaza vema Tanzania nchini mwao. Aidha, Tanzania na Ufaransa zilisaini tamko la pamoja la dhamira kuhusu kushirikiana katika eneo la uchumi wa buluu na usalama wa bahari.
- Mheshimiwa Spika, ninayo furaha kulifahamisha Bunge hili Tukufu kuwa, kufuatia ziara hiyo ya Mheshimiwa Rais, ujumbe wa wafanyabiashara na wawekezaji kutoka kampuni zipatazo 41 wanachama wa Jumuiya MEDEF na Business France ulifanya ziara nchini mwezi Mei 2022. Ziara hiyo ililenga kuangalia fursa za biashara na uwekezaji katika sekta za ujenzi, kilimo, afya, maji; nishati; TEHAMA na uchukuzi. Ninamshukuru kwa dhati Mhe. Rais Samia kwa kutenga muda wake na kukutana na ujumbe huo. Pia, ninapenda kuwashukuru Mhe. Mwigulu Lameck Nchemba (Mb), Waziri Fedha na Mipango,
Mhe. Ashatu K. Kijaji (Mb), Waziri wa Uwekezaji,
Viwanda na Biashara, Mhe. Mudrick Soragha, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Kazi, Uchumi na Uwekezaji, Mhe. Dkt. Khalid S. Mohamed, Waziri wa Ujenzi, Mawasiliano na Uchukuzi, Mhe. Suleiman Masoud Makame, Waziri wa Uchumi wa Buluu na Uvuvi na Mhe. Atupele Fredy Mwakibete (Mb), Naibu Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi kwa kukutana na kufanya mazungumzo na ujumbe huo wa wafanyabiashara na wawekezaji wa MEDEF na Business France.
- Mheshimiwa Spika, vilevile, kufuatia ziara hiyo, Benki ya Maendeleo ya Kilimo (TADB) na Serikali ya Ufaransa zilisaini Mkataba wa Ushirikiano ambapo TADB itapata Euro 80,000,000 kwa ajili ya kuendeleza sekta ya kilimo pamoja na kutoa mikopo yenye riba nafuu kwa wakulima. Serikali ya Ufaransa pia imeahidi kutoa fedha kiasi cha Euro milioni 178 kwa ajili ya utekelezaji wa Awamu ya 5 ya Mradi wa Ujenzi wa Barabara za Mabasi Yaendayo Kasi (Bus Rapid Transit Phase 5 – BRT) jijini Dar es Salaam. Kadhalika, Mamlaka ya Viwanja vya Ndege
Tanzania na Kampuni ya Kimataifa ya Bouygues Bàtiment (BBI) zilisaini Hati ya Makubaliano ya ukarabati wa Jengo la Pili la abiria katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere jijini Dar es Salaam.
- Mheshimiwa Spika, Wizara iliratibu na kufanikisha majadiliano kati ya Serikali ya Ufaransa na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar kuhusu kuendeleza ushirikiano katika sekta ya uchumi wa buluu. Serikali ya Ufaransa imeahidi kutoa msaada wa kitaalamu na fedha kwa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar ili kuimarisha doria na uvuvi katika bahari kuu. Ushirikiano huo ni chachu ya utekelezaji wa sera ya uchumi wa buluu ambayo inalenga kukuza kipato cha wananchi na kupunguza umaskini.
- Mheshimiwa Spika, mwezi Februari 2022, Wizara iliratibu na kufanikisha ziara ya
Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania nchini Ubelgiji na Makao Makuu ya Umoja wa Ulaya. Kufuatia ziara hiyo, Umoja wa Ulaya uliahidi kuipatia Tanzania kiasi cha Euro milioni 425 kwa ajili ya utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo kwa kipindi cha miaka mitatu kuanzia mwaka wa fedha 2021/2022. Aidha, Benki ya Uwekezaji ya Ulaya imeahidi kuipatia Tanzania mkopo wa masharti nafuu wa Euro milioni 50 kwa ajili kuboresha viwanja vya ndege vya Tabora, Kigoma, Shinyanga na Sumbawanga. Benki hiyo pia imeahidi kutoa mikopo ya masharti nafuu kwa wajasiriamali na wakulima wadogo wa Tanzania kupitia benki za biashara nchini. Vilevile, Serikali ya Ubelgiji imeahidi kutoa nyongeza ya kiasi cha Euro milioni 25 kwa ajili ya kutekeleza Programu ya Ushirikiano kati ya Tanzania na Ubelgiji kwa kipindi cha miaka mitano kuanzia 2023 hadi 2027. Programu hiyo inatarajiwa kuendeleza sekta ya elimu, maendeleo ya jinsia na kukuza ujasiriamali kwa watanzania.
- Mheshimiwa Spika, vilevile katika ziara hiyo,
Wizara iliratibu na kufanikisha Kongamano la
Biashara na Uwekezaji kati ya Tanzania na Ubelgiji lililohudhuriwa na wafanyabiashara 150 kutoka nchi hizi mbili. Kupitia kongamano hilo, kampuni nne za Ubelgiji na kampuni Dar-Lyon Investments Ltd ya Tanzania zilisaini makubaliano ya kibiashara, ambayo yataiwezesha kampuni hiyo ya Tanzania kuingiza nchini Ubelgiji bidhaa za dagaa, samaki, viungo, mchele, maharage ya njano na pilipili. Aidha, Chama cha Biashara, Viwanda na Kilimo Tanzania na Chama cha Biashara, Viwanda na Kilimo cha Ubelgiji na Luxembourg vilisaini Hati ya Makubaliano ya kuanzisha ushirikiano wa kibiashara.
- Mheshimiwa Spika, sambamba na hayo,
Wizara imefanikisha upatikanaji wa soko la bidhaa za Tanzania hususan dagaa, samaki na mchele nchini Ubelgiji na Umoja wa Ulaya kufuatia jitihada za kutafuta masoko ya bidhaa tunazozalisha nchini. Hadi sasa, tani 4 za dagaa kutoka Kigoma na tani 25 za mchele kutoka Mbeya zimeuzwa nchini humo. Aidha, wastani wa tani 50 za minofu ya samaki kutoka Ziwa Victoria huuzwa kila wiki nchini Ubelgiji.
- Mheshimiwa Spika, ninayo furaha kulieleza
Bunge lako tukufu kuwa, Wizara ilifanikisha Tanzania kuchaguliwa kuwa miongoni mwa nchi nne za Jumuiya ya Nchi za Afrika, Karibiani na Pasifiki (OACPS) zitakazonufaika na utekelezaji wa Awamu ya Pili ya Programu ya Maendeleo ya Sekta ya Madini inayotekelezwa kwa ubia kati ya OACPS na Umoja wa Ulaya. Programu hiyo inatekelezwa kwa kipindi cha miaka mitatu kuanzia mwaka 2022 hadi 2024 kwa ufadhili wa Euro milioni 11.1 kutoka Umoja wa Ulaya. Kupitia programu hiyo, sekta ya madini hapa nchini itanufaika na miradi ya kuendeleza wachimbaji wadogo hususan vijana na wanawake hivyo kuchochea ukuaji wa uchumi na maendeleo. Nchi nyingine zitakazonufaika na programu hiyo ni Suriname, Burkina Faso na DRC.
- Mheshimiwa Spika, mwezi Januari 2022, Wizara iliratibu na kufanikisha kusainiwa kwa mkataba kati ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Serikali ya Shirikisho la Ujerumani wa ushirikiano wa maendeleo katika sekta za afya, maji na michezo. Katika utekelezaji wa makubaliano ya ushirikiano huo, mwezi Aprili 2022 Ujerumani kupitia Benki ya Maendeleo ya Ujerumani (KfW) iliipatia Zanzibar Euro 660,000 kwa ajili ya kufanya upembuzi yakinifu wa mahitaji ya maji Zanzibar. Aidha, Ujerumani imeahidi kuipatia Zanzibar Euro milioni 1,000,000 kwa ajili ya kuendeleza sekta ya michezo.
- Mheshimiwa Spika, mwezi Desemba 2021, Wizara iliratibu na kufanikisha Jukwaa la Biashara kati ya Tanzania na Italia lililofanyika jijini Rome, Italia na kuwakutanisha
wafanyabiashara 250 kutoka katika sekta za utalii, madini, anga, kilimo na ujenzi. Kupitia jukwaa hilo Shirika la Taifa la Madini (STAMICO) lilisaini mkataba wa makubaliano ya awali na kampuni ya SUNESS Limited ya Italia kwa ajili kuendeleza mradi wa kuchimba madini ya shaba mkoani
Kilimanjaro.
- Mheshimiwa Spika, mwezi Novemba 2021, Wizara iliratibu na kufanikisha Kongamano la kwanza la Biashara kati ya Tanzania na Uingereza lililofanyika jijini Dar es Salaam. Kongamano hilo lilihudhuriwa na washiriki 1,100 kutoka sekta za umma na binafsi ambao walijadili na kuweka mikakati endelevu ya kukuza biashara kati ya Tanzania na Uingereza hususan kwenye uwekezaji na miradi ya maendeleo. Aidha, nchi hizi mbili zilisaini mpango kazi wa kutekeleza maeneo ya ushirikiano kwenye sekta ya biashara na uwekezaji.
- Mheshimiwa Spika, mwezi Oktoba 2021, Wizara iliratibu na kufanikisha majadiliano ya ushirikiano wa maendeleo baina ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Shirikisho la Ujerumani yaliyofanyika jijini Dar es Salaam. Kufuatia majadiliano hayo, Serikali ya Ujerumani imeridhia kutoa msaada wenye thamani ya Euro milioni 71 kwa ajili ya uendelezaji wa sekta ya maliasili na utalii hususan uhifadhi wa mbuga za taifa; sekta ya maji; utawala bora; na afya ya mama na mtoto.
- Mheshimiwa Spika, mwezi Oktoba 2021, Wizara iliratibu na kufanikisha majadiliano ya kisiasa kati ya Tanzania na Umoja wa Ulaya. Majadiliano hayo yalilenga kuimarisha uhusiano wa muda mrefu na kukuza ushirikiano kwenye maeneo ya biashara na uwekezaji, miradi ya maendeleo, masuala ya kikanda na kimataifa. Aidha, mara baada ya kukamilika kwa majadiliano hayo, pande mbili zilisaini Tamko la Pamoja kuthibitisha utayari wa kutekeleza makubaliano yaliyofikiwa.
- Mheshimiwa Spika, vilevile, Wizara iliratibu na kufanikisha majadiliano kati ya Tanzania na Umoja wa Ulaya ambapo Umoja huo uliahidi kuipatia Tanzania Euro milioni 703 kwa kipindi cha miaka 7 kuanzia mwaka wa fedha 2021/2022. Utekelezaji wa makubaliano hayo umeanza ambapo mwezi Machi 2022 Tanzania na Umoja wa Ulaya zilisaini mikataba mitatu ya ufadhili wa miradi yenye thamani ya Euro milioni 180 ambazo zitatolewa katika maeneo ya maendeleo ya jinsia, TEHAMA na maendeleo ya miji. Upatikanaji wa fedha hizo utachangia katika juhudi za Serikali za kuleta maendeleo na kusogeza huduma karibu na wananchi.
- Mheshimiwa Spika, mwezi Julai 2021, Wizara iliratibu na kufanikisha kuanza kwa safari za moja kwa moja za shirika la ndege la Eurowings kutoka Frankfurt, Ujerumani hadi Zanzibar. Majadiliano kuhusu shirika hilo kuanzisha safari za moja kwa moja kwenda Kilimanjaro yanaendelea. Kadhalika, mwezi Oktoba 2021, Wizara iliratibu na kufanikisha kuanzishwa kwa safari za moja kwa moja za Shirika la Ndege la Ufaransa (Air France) kutoka Paris, Ufaransa hadi Zanzibar.
- Mheshimiwa Spika, vilevile Wizara inaendelea kuratibu majadiliano ya kurejesha safari za moja kwa moja za kampuni ya TUI Fly ya Ubelgiji kutoka Brussels kwenda Zanzibar na pia kuanzisha safari za kwenda Kilimanjaro. Kuanza kwa safari hizo kutapunguza gharama za usafiri kwa watalii na wafanyabiashara kutoka barani Ulaya na hivyo kuchochea ukuaji wa sekta ya utalii na biashara nchini.
- Mheshimiwa Spika, ninapenda kukujulisha kuwa, Wizara iliratibu kwa mafanikio zoezi la kuwaondoa watanzania 289 kati yao 273 ni wanafunzi waliokuwa Ukraine kufuatia vita kati ya Urusi nchini hiyo. Hadi kufikia mwezi Mei 2022, wanafunzi 219 wamesharejea nchini na wengine wapo kwenye nchi mbalimbali walizofikia zikiwemo Poland (11), Hungary (02), Ujerumani (23), Uholanzi (03) wakiendelea kutafuta nafasi ya kuendeleza masomo katika vyuo kwenye nchi hizo. Wizara inaendelea kushirikiana na Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia kutoa ushauri na miongozo kuhusu hatma ya masomo ya wanafunzi hao baada ya kurejea nchini. Halikadhalika, Balozi zetu katika nchi za Sweden, Urusi na Ujerumani zinaendelea kuratibu upatikanaji wa nafasi za masomo katika vyuo vya nchi za jirani na Ukraine na kuwashauri wanafunzi waliobaki katika nchi hizo ipasavyo. Wizara pia imeratibu na kufanikisha kuondolewa kwa watalii wapatao 1,000 kutoka Ukraine waliokwama Zanzibar kufuatia vita hiyo kwenda nchini Poland.
Mapambano Dhidi ya UVIKO-19 kupitia
Ushirikiano wa Kimataifa
- Mheshimiwa Spika, Wizara iliratibu na kufanikisha upatikanaji wa msaada wa chanjo dhidi ya UVIKO-19, ambapo Tanzania imepokea msaada wa dozi 4,900,000 za chanjo kutoka Marekani; dozi 2,300,000 kutoka China; dozi 115,200 kutoka Ubelgiji; dozi 1,000,000 kutoka Uturuki; na dozi 150,000 kutoka Mauritius na dozi 1,024,564 kutoka Rwanda. Aidha, mwezi Februari na Mei 2022, Wizara iliratibu na kufanikisha upatikanaji wa vifaa tiba kutoka nchi za Ufaransa na Austria mtawalia kwa ajili ya kukabiliana na UVIKO-19.
- Mheshimiwa Spika, mwezi Septemba 2021, Wizara iliratibu na kufanikisha mkutano kati ya Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Bi. Kristalina Georgieva, Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF). Kufuatia mkutano huo, IMF imeipatia Tanzania mkopo wa masharti nafuu wenye thamani Dola za Marekani milioni 567.25 sawa na Shilingi trilioni 1.3 kwa ajili ya kukabiliana na athari za kiuchumi na kijamii zilizosababishwa na UVIKO-19. Sekta zilizonufaika na mkopo huo ni afya, elimu, utalii, maji, pamoja na makundi maalum ikiwemo kaya maskini, vijana, wanawake na wenye ulemavu.
4.3Kuratibu Masuala ya Ushirikiano wa Kikanda na Kimataifa
4.3.1 Jumuiya ya Afrika Mashariki
107. Mheshimiwa Spika, Wizara imeendelea kuratibu ushiriki wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika utekelezaji wa hatua za mtangamano za Jumuiya ya Afrika Mashariki kwa kuzingatia maslahi mapana ya Taifa kama ifuatavyo:
Mkutano wa Wakuu wa Nchi Wanachama wa
Jumuiya ya Afrika Mashariki
- Mheshimiwa Spika, mwezi Machi 2022, Wizara iliratibu na kufanikisha ushiriki wa Tanzania kwenye Mkutano wa 19 wa Wakuu wa
Nchi Wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki. Katika mkutano huo, nchi wanachama ziliridhia ombi la Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) kujiunga na Jumuiya, hatua inayoifanya Jumuiya kuwa na wanachama saba. Tarehe 08 Aprili, 2022 Mheshimiwa Uhuru Muigai Kenyatta, Rais wa Jamhuri ya Kenya na Mwenyekiti wa Jumuiya kwa niaba ya Jumuiya ya Afrika Mashariki alisaini pamoja na Mheshimiwa Félix-Antoine Tshisekedi Tshilombo, Rais wa DRC mkataba wa kuiwezesha nchi hiyo kujiunga na Jumuiya ya Afrika
Mashariki.
- Mheshimiwa Spika, hivi sasa DRC inaendelea na taratibu za ndani za kikatiba za kuridhia mkataba huo na inatarajiwa kuwasilisha kwa Katibu Mkuu wa Jumuiya hati ya kuridhia kujiunga ifikapo tarehe 29 Septemba, 2022 ili kuwa mwanachama kamili. Kujiunga kwa nchi hiyo ni kiashiria cha kuendelea kukua kwa Jumuiya na kuongezeka kwa fursa za kiuchumi na kijamii katika Jumuiya.
Umoja wa Forodha wa Afrika Mashariki![]()
- Mheshimiwa Spika, nchi wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki zimeendelea kutekeleza Itifaki ya Umoja wa Forodha wa Afrika Mashariki inayolenga kukuza biashara ya bidhaa na uwekezaji ndani ya Jumuiya. Uchambuzi wa mwenendo wa biashara kwa mujibu wa Taarifa ya Biashara na Uwekezaji ya EAC mwaka 2020, unaonesha kuwa thamani ya mauzo ya bidhaa miongoni mwa nchi wanachama ilipungua kwa asilimia 7.37 kutoka Dola za Marekani Milioni 3,162.80 mwaka 2019 hadi Dola za Marekani Milioni 2,929.6 mwaka 2020. Aidha, thamani ya manunuzi ya bidhaa miongoni mwa nchi wanachama ilishuka kwa asilimia 3.71 kutoka Dola za Marekani Milioni 3,175.80 mwaka 2019 hadi Dola za Marekani Milioni 3,058 mwaka 2020. Kushuka kwa biashara katika mwaka 2020 kulitokana na kuendelea kuwepo kwa vikwazo vya kibiashara baina ya nchi wanachama na athari za UVIKO-19.
- Mheshimiwa Spika, pamoja na kushuka kwa biashara ndani ya Jumuiya ya Afrika Mashariki, thamani ya mauzo ya bidhaa za
Tanzania ndani ya Jumuiya iliongezeka kutoka Dola za Marekani milioni 674.4 mwaka 2019 hadi Dola za Marekani milioni 812.5 mwaka 2020 na thamani ya manunuzi ya bidhaa za Tanzania ndani ya Jumuiya ilipungua kutoka Dola za Marekani milioni 329.2 mwaka 2019 hadi Dola za Marekani milioni 324.3 mwaka 2020. Taarifa za awali zinaonesha kuwa mauzo ya Tanzania katika nchi nyingine wanachama yalikuwa Dola za Marekani milioni 1,161.2 mwaka 2021 na manunuzi ya Tanzania kutoka nchi nyingine wanachama yalikuwa Dola za Marekani milioni 525.4 mwaka 2021. Kukua kwa biashara na thamani ya mauzo kwa nchi yetu katika kipindi hicho kumetokana na juhudi za Serikali kuendelea kuboresha mazingira ya biashara na uwekezaji nchini.
- Mheshimiwa Spika, nchi wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki zimeendelea kutekeleza Mfumo wa Himaya Moja ya Forodha ambao unalenga kupunguza gharama za ufanyaji biashara ndani ya Jumuiya. Mfumo huo umeweka utaratibu wa mizigo kulipiwa kodi kabla ya kuondoka kituo cha kwanza cha forodha mzigo huo ulipoingilia (bandarini, kiwanja cha ndege au mpakani) kusafirishwa kwenda nchi husika. Utekelezaji wa mfumo wa himaya moja ya forodha umepunguza gharama na muda wa kusafirisha shehena za mizigo ndani ya Jumuiya. Mathalan, muda wa kusafirisha mzigo toka bandari ya Dar es Salaam kwenda Kigali, Bujumbura na Kampala umepungua kutoka wastani wa zaidi ya siku 8 mwaka 2013 hadi kufikia siku 4 mwaka 2019. Hata hivyo, kutokana na athari za UVIKO-19 muda huo umeongezeka hadi kufikia wastani wa siku 6. Mafanikio hayo pia yametokana na Tanzania kupunguza idadi ya vituo vya kupima uzito wa magari yanayosafirisha mizigo kwenda nje na matumizi ya vituo vya kutoa huduma pamoja mpakani (OSBP).
- Mheshimiwa Spika, Wizara imeendelea kuratibu uondoaji wa vikwazo vya biashara visivyo vya kiforodha ndani ya nchi wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki. Kupitia kamati ya Kitaifa na Kikanda ya ufuatiliaji wa vikwazo vya biashara visivyo vya kiforodha, kuanzia mwaka 2007 hadi Oktoba, 2021 jumla ya vikwazo 232 viliondolewa na nchi wanachama.
- Mheshimiwa Spika, Wizara iliratibu mikutano ya uwili kati ya Tanzania na Kenya iliyofanyika katika kipindi cha Julai 2021 hadi Machi 2022. Kupitia mikutano hiyo vikwazo vya biashara visivyo vya kiforodha 56 kati ya 70 viliondolewa. Vikwazo 14 vilivyosalia vipo katika hatua mbalimbali za majadiliano ya kuviondoa. Miongoni mwa vikwazo visivyo vya kiforodha vilivyopatiwa ufumbuzi ni pamoja na ucheleweshaji wa kupitisha mizigo kutokana na utaratibu uliokuwepo wa matumizi ya mashine ya ukaguzi; ucheleweshaji wa kutoa vibali vya kuingiza bidhaa zitokanazo na maziwa kwa ajili ya kuuza nje; usumbufu wa taratibu za kiforodha uliokuwa unafanywa na Mamlaka ya Mapato Kenya; changamoto ambazo Taifa Gas Tanzania ilikuwa ikizipata ili kuweza kuwekeza Mombasa, Kenya; changamoto ya upatikanaji wa vibali vya kazi kwa wataalam wa Tanzania ili kuweza kufanya kazi Kenya; na watanzania kutakiwa kuwa na cheti cha chanjo ya UVIKO-19 wanaposafiri kwenda Kenya kwa njia ya anga.
- Mheshimiwa Spika, hatua ya kuondoa vikwazo vya kibiashara visivyo vya kiforodha imepunguza gharama za kufanya biashara ndani ya Jumuiya.
Utekelezaji wa Programu za Jumuiya katika
Sekta za Uzalishaji
Sekta ya Kilimo
116. Mheshimiwa Spika, mwezi Septemba 2021, Tanzania iliridhia Itifaki ya Jumuiya ya Afrika Mashariki ya Afya ya Mimea, Wanyama na usalama wa Chakula ya mwaka 2013. Kuridhiwa kwa Itifaki hiyo kutaiwezesha Tanzania kuuza bidhaa zitokanazo na mimea, wanyama na samaki ndani ya Jumuiya bila vikwazo ikizingatiwa kuwa nchi yetu inaongoza kwa uzalishaji wa bidhaa za kilimo na mifugo katika Jumuiya. Utekelezaji wa itifaki hii, utakuwa pia kichocheo cha kukuza biashara ya mimea, wanyama na samaki baina ya nchi wanachama wa Jumuiya na nchi nyingine nje ya Jumuiya.
Sekta ya Viwanda
117. Mheshimiwa Spika, mwezi Desemba,
2021 Wizara iliratibu na kufanikisha Maonesho ya 21 ya Nguvu Kazi Jua Kali ya Afrika Mashariki yaliyofanyika jijini Mwanza. Katika maonesho hayo wajasiriamali 1,089 kutoka nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki walishiriki. Kati ya hao, wajasiriamali 419 walitokea Tanzania Bara na 50 walitokea Zanzibar. Kufuatia maonesho hayo, wafanyabiashara wetu walifanikiwa kupata fursa ya kutangaza bidhaa zao, kubadilishana uzoefu, teknolojia pamoja na taarifa za kibiashara.
Sekta ya Utalii
- Mheshimiwa Spika, mwezi Oktoba 2021, Wizara iliratibu na kufanikisha kufanyika kwa Maonesho ya Kwanza ya Utalii ya Afrika Mashariki yaliyofanyika jijini Arusha. Maonesho hayo yalishirikisha kampuni za utalii 157, wanunuzi wa kimataifa wa bidhaa za utalii 41, vyombo vya habari kutoka ndani na nje ya Jumuiya ikiwemo Aljazeera na Shirika la Habari la China. Hatua hii ilitoa fursa ya kutangaza utalii wa Tanzania na hivyo kuchangia katika jitihada za serikali kukuza shughuli za kitalii zilizokuwa zimeathirika na UVIKO-19.
- Mheshimiwa Spika, Wizara kupitia balozi zetu inaendelea kuwahamasisha wanunuzi wa kimataifa wa bidhaa za utalii walioshiriki katika Maonesho hayo, ambao walipata fursa ya kutembelea vivutio vya nchi yetu ili kushirikiana nao katika kuhamashisha watalii wengi zaidi kutembelea vivutio vya utalii vya Tanzania.
Umoja wa Fedha wa Afrika Mashariki
- Mheshimiwa Spika, Itifaki ya Umoja wa Fedha wa Afrika Mashariki ilisainiwa na nchi wanachama mwaka 2013 na kuanza kutumika mwaka 2014. Itifaki hiyo imeweka misingi ya kufikia umoja wa sarafu ndani ya miaka 10, ambapo nchi wanachama zitatumia sarafu moja ya Afrika Mashariki. Ili kutekeleza azma hiyo, Jumuiya imeendelea kuratibu uanzishwaji wa taasisi zitakazosimamia utekelezaji wa Umoja wa Fedha wa Afrika Mashariki.
- Mheshimiwa Spika, Mkutano wa 41 wa Baraza la Mawaziri uliofanyika mwezi Novemba
2021 ulipitisha Muswada wa Sheria ya kuanzisha
Kamisheni ya Huduma za Fedha ya Afrika
Mashariki na Muswada wa Sheria ya kuazisha Kamisheni ya Usimamizi, Udhibiti na Ufuatiliaji wa utekelezaji wa Umoja wa Fedha. Miswada hiyo imewasilishwa katika Bunge la Afrika Mashariki kwa ajili ya kutunga sheria ya kuanzisha taasisi hizo.
Utekelezaji wa Miradi na Programu za Miundombinu ya Uchumi na Huduma za Jamii
122. Mheshimiwa Spika, katika Mkataba wa Uanzishwaji wa Jumuiya ya Afrika Mashariki, Nchi Wanachama zilikubaliana kutekeleza programu na miradi katika sekta mbalimbali ili kufikia malengo ya mtangamano. Katika kipindi hiki Wizara imeratibu kwa mafanikio ushiriki wa Tanzania katika majadiliano ya kikanda na utekelezaji wa programu na miradi ya Jumuiya kama ifuatavyo:
Sekta ya Barabara
- Mheshimiwa Spika, Wizara iliratibu na kufanikisha uwasilishwaji wa mapendekezo ya Tanzania kutekeleza Mradi wa Ujenzi wa Barabara ya Lusahunga – Rusumo / Kayonza – Kigali (km 162) ambao unatekelezwa kupitia Programu ya
Kuendeleza Mitandao ya Barabara kwa Nchi za
Jumuiya ya Afrika Mashariki kati ya Tanzania na
Rwanda. Mradi huo umepata ufadhili wa Benki ya Dunia wa Dola za Marekani milioni 72, na kukamilika kwake kutachochea ukuaji wa biashara kwa kuwa barabara hii ni kiungo muhimu kati ya Tanzania na nchi nyingine za Burundi, Rwanda na DRC.
- Mheshimiwa Spika, Wizara iliratibu na kufanikisha upatikanaji wa fedha kwa ajili ya ujenzi wa sehemu ya mradi wa Barabara ya Tanga – Bagamoyo/Malindi – Lunga Lunga (km 400) kutoka Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB). Kwa upande wa Tanzania, mradi unahusisha ujenzi wa barabara ya Tanga – Pangani – Makurunge yenye urefu wa kilometa 244, ambayo imegawanywa katika sehemu kuu nne. Sehemu ya kwanza ni kipande cha barabara ya Pangani – Tangani (km 50) ambayo inajengwa kwa kutumia fedha za ndani. Sehemu ya pili inahusisha ujenzi wa kipande cha barabara ya Pangani -Tungamaa (km 14.3); Daraja la Pangani (mita 525); Ushongo Spur (km 5.9); na Pangani Access (km 5.4). Sehemu ya tatu inahusisha kipande cha barabara ya Tungamaa – Mkwaja – Mkange (km 95.2) na Sehemu ya nne inahusisha kipande cha barabara ya Makurunge – Mkange (km 73.5).
- Mheshimiwa Spika, Serikali ya Tanzania na Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB) mwezi Agosti 2021 zimesaini Mkataba wa wa Dola za Marekani milioni 350 kwa ajili ya ujenzi wa sehemu ya Tatu ya mradi huo ambayo inahusisha kipande cha barabara ya Tungamaa – Mkwaja – Mkange (km 95.2). Mkandarasi yupo katika hatua ya maandalizi ya kuanza ujenzi.
Sekta ya Reli
126. Mheshimiwa Spika, Wizara imeendelea kuratibu ushiriki wa Tanzania katika utekelezaji wa Mpango Mkuu wa Reli wa Jumuiya ya Afrika Mashariki uliopitishwa mwaka 2009 na Baraza la
Mawaziri la Jumuiya ya Afrika Mashariki. Kupitia Mpango huo, Tanzania inatekeleza mradi wa kujenga reli ya kisasa (SGR) yenye urefu wa km 2,561. Reli hiyo itaunganisha mikoa ya Dar es Salaam, Morogoro, Dodoma, Singida, Tabora, Mwanza, Kigoma na nchi jirani za Rwanda, Burundi na DRC. Ujenzi wa reli hiyo nchini ina mtandao wa km 1,219 za njia kuu na utekelezaji wake umegawanyika katika Awamu Tano. Awamu zote tano ambazo ni Dar es Salaam – Morogoro (km 300), Morogoro – Makutopora (km 422), Makutupora – Tabora (km 294), Tabora – Isaka (km 130), na Isaka – Mwanza – (km 249) tayari zimepata fedha za ujenzi na wakandarasi wanaendelea na kazi. Reli hii pia, itaiunganisha nchi ya Rwanda kupitia Isaka kwenda Kigali ambapo kwa upande wa Rwanda (Isaka – Kigali; km 532) tayari kazi za usanifu wa kina na upembuzi yakinifu pamoja na matayarisho ya eneo itakapopita reli hiyo yamekamilika.
Vituo vya Huduma kwa Pamoja Mpakani
127. Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2021/2022, Wizara imeendelea kuratibu utekelezaji wa Mradi wa Ujenzi wa Kituo cha Huduma kwa Pamoja Mpakani (OSBP) cha
Manyovu/Mugina kilichopo katika mpaka wa
Tanzania na Burundi kwa mkopo wa Dola za Marekani milioni 24 kutoka AfDB. Fedha hizo, ni sehemu ya mkopo wa Dola za Marekani milioni 256.2 zilizotolewa na Benki hiyo kwa ajili ya Mradi wa Barabara ya Jumuiya ya Afrika Mashariki ya Kabingo – Kasulu – Manyovu/ Rumonge – Gitaza. Kituo hiki kinatarajiwa kuwa cha mfano (standard model design) katika Jumuiya ya Afrika Mashariki.
Sekta ya Nishati
- Mheshimiwa Spika, Wizara imeendelea kuratibu Mradi wa Kikanda wa Kufua Umeme wa Murongo/Kikagati unaotekelezwa kwa pamoja kati ya Tanzania na Uganda. Mradi huu unazalisha jumla ya Megawati 14 ambapo kutokana na Mkataba wa Mradi huo, Tanzania inapata
Megawati saba kama ilivyo kwa upande wa Uganda. Mradi huo ulianza uzalishaji mwezi Februari 2022. Umeme huo tayari umesambazwa katika Wilaya za Kyerwa na Karagwe mkoani Kagera ambapo awali zilikuwa zinatumia umeme kutoka gridi ya Uganda.
- Mheshimiwa Spika, Wizara imeratibu majadiliano ya utekelezaji wa Mradi wa Kikanda wa Kufua Umeme wa Nsongezi ambao utajengwa katika Mto Kagera kwa ushirikiano baina ya Tanzania, Uganda na Rwanda. Mradi huu unatarajiwa kuzalisha umeme wa Megawati 39 utakapokamilika ambazo zitagawanywa kwa nchi husika.
Sekta ya Afya
130. Mheshimiwa Spika, mwezi Desemba,
2021 Wizara iliratibu na kushiriki katika Mkutano wa 21 wa Baraza la Mawaziri la Kisekta la Afya la Jumuiya ya Afrika Mashariki uliofanyika Zanzibar.
Kupitia mkutano huo, nchi wanachama zilikubaliana kuimarisha mikakati ya pamoja ya kukabiliana na athari za UVIKO-19 ikiwemo kuandaa Hati ya Pamoja ya Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC Health Common Pass) itakayotumika kurahisisha huduma za usafiri na usafirishaji ndani ya Jumuiya. Aidha, Nchi Wanachama zilikubaliana kufanya uhakiki wa maabara zinazotumika kufanya vipimo vya UVIKO-19 kwa lengo la kuwezesha hati inayotolewa na nchi moja kutambuliwa kutumika katika nchi nyingine wanachama.
Usimamizi Endelevu wa Rasilimali za Maji katika Bonde la Ziwa Victoria
- Mheshimiwa Spika, Wizara imeratibu na kufanikisha upatikanaji wa Euro milioni 5.3 kupitia Programu ya Pamoja ya Usimamizi na Uendelezaji wa Rasilimali za Maji katika Bonde la
Ziwa Victoria inayoratibiwa na kamisheni ya Bonde la Ziwa Victoria ya Afrika Mashariki. Fedha hizi zitaiwezesha Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Mwanza kukarabati na kupanua mtandao wake wa majitaka kwa kilomita 14.4, kuunganisha kaya 1,600 kwenye mtandao huo na kununua vifaa.
- Mheshimiwa Spika, mwezi Aprili 2022, Wizara iliratibu na kufanikisha ushiriki wa
Tanzania kwenye Mkutano wa 17 wa Baraza la
Mawaziri la Kisekta la Elimu, Sayansi na Teknolojia, Utamaduni Sanaa na Michezo uliofanyika jijini Dar es salaam. Mkutano ulipitisha maazimio yanayohusu masuala ya elimu ikiwa ni pamoja na mashindano ya uandishi wa insha kwa shule za sekondari za Jumuiya kwa mwaka 2021 ambapo mwanafunzi wa Tanzania Godson Chrispin Obaga kutoka Shule ya
Sekondari Nyerere iliyopo Mwanga, Kilimanjaro alikuwa mshindi wa kwanza katika Jumuiya ya Afrika Mashariki. Washindi sita wa mwanzo mmoja kutoka kila nchi watazawadiwa na mkutano ujao wa Wakuu wa Nchi za Jumuiya ya
Afrika Mashariki.
Sekta ya Utamaduni na Michezo
133. Mheshimiwa Spika, Wizara kwa kushirikiana na Sekretarieti ya Jumuiya ya Afrika Mashariki na kampuni ya Camp Fire Logs Guilds ya nchini Uganda iliratibu Ziara ya Nne ya Waendesha Baiskeli wa Jumuiya ya Afrika Mashariki iliyoanzia jijini Dar es Salaam mwezi
Agosti 2021 na kuhitimishwa jijini Arusha mwezi Septemba 2021. Tukio hilo lililenga kutoa elimu kwa umma kuhusu Jumuiya na fursa zilizopo; kuhamasisha utalii wa ndani na kutoa elimu ya mazingira. Waendesha baiskeli hao walipita katika mikoa ya Pwani, Tanga, Kigoma, Tabora, Singida, Dodoma, Manyara na Arusha nchini Tanzania na majiji ya Nairobi, Kampala, Kigali na Bujumbura.
Ushirikiano wa Siasa, Ulinzi na Usalama
134. Mheshimiwa Spika, Wizara iliratibu na kufanikisha ushiriki wa Tanzania katika kuandaa mpango kazi wa namna ya kushirikisha Wanawake, Asasi za Kiraia na Vijana katika shughuli za amani na usalama za Jumuiya ya Afrika Mashariki. Lengo la Mpango Kazi huo, ni kuimarisha ushiriki wa wanawake katika kuzuia na kutatua migogoro pamoja na kujenga amani na usalama endelevu ndani ya Jumuiya. Mpango kazi huo utaimarisha ushiriki wa makundi haya katika kutekeleza mfumo wa utatuzi wa Migogoro wa Jumuiya ya Afrika Mashariki.
Bunge la Afrika Mashariki
135. Mheshimiwa Spika, Wizara iliendelea kuratibu na kufanikisha ushiriki wa Tanzania katika mikutano ya Bunge la Afrika Mashariki, ambalo ni chombo cha kutunga sheria za Jumuiya. Katika kipindi hiki, Bunge hilo lilipitisha muswada wa Sheria wa Kuzuia na Kupambana na Rushwa wa mwaka 2019. Madhumuni ya Muswada huu ni kusimamia uadilifu na maadili katika vyombo na taasisi za Jumuiya; kuimarisha mfumo wa kisheria kwa ajlli ya kuzuia na kupambana na rushwa katika Jumuiya na kutoa ushirikiano kupitia wakala wa kitaifa katika kupambana na vitendo vya rushwa.
Ajira katika Jumuiya ya Afrika Mashariki
136. Mheshimiwa Spika, ninapenda kulijulisha Bunge lako Tukufu kuwa Wizara iliratibu na kusimamia kikamilifu mchakato wa ajira katika Jumuiya ya Afrika Mashariki uliofanyika kuanzia mwezi Oktoba 2021 hadi Aprili 2022. Katika mchakato huo, Tanzania ilifanikiwa kupata nafasi 10 kati ya 37 zilizotangazwa kwa nchi wanachama sita za Jumuiya ya Afrika Mashariki. Wizara inaendelea kuratibu fursa za ajira katika jumuiya za kikanda na Mashirika ya Kimataifa.
4.3.2 Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika
(SADC)
- Mheshimiwa Spika, Wizara imeendelea kuratibu ushiriki wa Tanzania katika Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika, ambapo katika kipindi hiki Tanzania imechaguliwa kuwa mwenyeji wa Kituo cha SADC cha Kupambana na Ugaidi chenye makao makuu yake jijini Dar es Salaam. Kituo hiki kilichozinduliwa rasmi tarehe 28 Februari 2022, kitasaidia kuimarisha ushirikiano baina ya Serikali na Taasisi za Kikanda na Kimataifa zinazoratibu mapambano dhidi ya ugaidi. Aidha, kuanzia mwezi Agosti 2021 hadi Agosti 2022, Tanzania imeteuliwa kuwa Mwenyekiti wa Kamati ya Rasilimaliwatu na Utawala ya SADC na kutokana na uenyekiti huo, Tanzania imechangia kuboresha Sera za ajira katika Jumuiya.
- Mheshimiwa Spika, mwezi Agosti 2021, Wizara iliratibu na kufanikisha ushiriki wa
Tanzania katika Mkutano wa 41 wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa SADC uliofanyika jijini Lilongwe, Malawi. Ujumbe wa Tanzania uliongozwa na Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Katika
Mkutano huo, nchi wanachama ziliridhia ombi la
Tanzania kuongeza wigo wa matumizi ya lugha ya Kiswahili katika ngazi ya kamati za kisekta za mawaziri za Jumuiya. Nchi wanachama pia ziliridhia kiasi cha Dola za Marekani 73,518.20 kutumika kugharamia mchakato wa kutafsiri nyaraka muhimu za SADC kwa lugha ya Kiswahili zikiwemo Mkataba wa uanzishwaji wa SADC, itifaki na nyaraka za kisera.
- Mheshimiwa Spika, katika kipindi hiki Tanzania imeendelea kushiriki katika juhudi za SADC za kuimarisha hali ya ulinzi na usalama katika ukanda wa kusini mwa Afrika, hususan Msumbiji ambayo inakabiliwa na mapigano kati ya majeshi ya Serikali na vikundi vya kigaidi katika eneo la kaskazini mwa nchi hiyo. Ninapenda kulifahamisha bunge lako tukufu kuwa Tanzania imeshiriki kwa kuchangia askari katika Misheni ya SADC nchini Msumbiji (SAMIM) na bajeti ya uendeshaji wa SAMIM kwa mwaka 2021/2022.
- Mheshimiwa Spika, napenda kulifahamisha bunge lako tukufu kuwa, Tanzania imechaguliwa kuwa mwenyeji wa Kituo cha Kupambana na Ugaidi cha Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika. Makao Makuu ya Kituo hicho kilichozinduliwa rasmi tarehe 28 Februari 2022 yapo jijini Dar es Salaam. Uwepo wa kituo hicho hapa nchini utasaidia kuimarisha ushirikiano baina ya Serikali na taasisi mbalimbali za kikanda na kimataifa zinazoratibu mapambano dhidi ya ugaidi ikiwemo Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulikia Dawa za Kulevya na Uhalifu na Kituo cha Stadi na Utafiti cha Masuala ya Ugaidi cha Umoja wa Afrika. Vilevile, Tanzania inanufaika kupitia kubadilishana ujuzi, mafunzo, teknolojia na nafasi za ajira.
- Mheshimiwa Spika, mwezi Machi 2022, Wizara iliratibu na kufanikisha ushiriki wa Tanzania katika Mkutano wa Baraza la Mawaziri wa SADC uliofanyika jijini Lilongwe, Malawi. Katika mkutano huo, Baraza liliidhinisha jumla ya Dola za Marekani 455,006 kwa ajili ya kutasfiri machapisho tisa ya Hashim Mbita katika lugha ya Kiswahili na kutengeneza makala za video.
- Mheshimiwa Spika, ninapenda kulitaarifu bunge lako tukufu kuwa, kampuni ya Tanzania iitwayo Epitome Architects ilishinda zabuni ya ujenzi wa sanamu ya Hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere ambayo itawekwa katika Jengo la Usalama lililopo Makao Makuu ya Umoja wa Afrika Addis Ababa, Ethiopia. Mkataba kati ya Sekretarieti na kampuni hiyo unatarajiwa kusainiwa kabla ya kufika mwisho wa mwaka huu wa fedha.
- Mheshimiwa Spika, sambamba na hilo, mwaka 2018 Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ilisaini Hati ya Makubaliano na Sekretarieti ya SADC kwa ajili ya ununuzi wa pamoja wa dawa, vifaa tiba na vitendanishi vya maabara kwa nchi wanachama wa SADC. Tangu kusainiwa kwa mpango huo Bohari ya Dawa (MSD) imefanikiwa kununua dawa, vifaa tiba na vitendanishi vya maabara kwa niaba ya nchi za Comoro na Shelisheli na kuokoa gharama za manunuzi kwa zaidi ya asilimia 55. Nchi ambazo zimeonesha nia ya kuutumia mpango huo ni pamoja na Botswana, Malawi, na Msumbiji. Hata hivyo, mpango huo unakabiliwa na changamoto mbalimbali ikiwemo mwamko mdogo wa kuutumia mpango huo na tofauti ya taratibu za manunuzi. Hivyo, Mkutano wa Baraza la Mawaziri uliofanyika mwezi Machi 2022 uliiagiza Sekretarieti ya SADC kushirikiana na Bohari ya Dawa ya Tanzania kushughulikia changamoto hizo ili kuhakikisha Nchi Wanachama zinanufaika na mpango huo.
- Mheshimiwa Spika, napenda kulifahamisha Bunge lako kuwa Mheshimiwa Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, Rais wa Awamu ya Nne wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ameteuliwa kuwa Mwenyekiti wa Jopo la Wazee la SADC la Usuluhishi wa Migogoro kwa kipindi cha miaka minne (2021-2025). Kadhalika, Bi. Hellen Lwegasira ameteuliwa kuwa Makamu Mwenyekiti wa Timu ya Upatanishi ya SADC kwa kipindi cha miaka minne (2021-2025). Kuteuliwa kwa viongozi hawa ni ishara ya Tanzania kuendelea kuaminiwa katika usuluhishi wa migogoro.
4.3.3 Umoja wa Afrika
- Mheshimiwa Spika, mwezi Februari
2022, Wizara iliratibu na kufanikisha ushiriki wa
Tanzania katika mkutano wa 35 wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Umoja wa Afrika uliofanyika jijini Addis Ababa, Ethiopia. Pamoja na masuala mengine, Mkutano uliridhia pendekezo la Tanzania la Kiswahili kuwa lugha rasmi ya kazi ya Umoja huo. Aidha, katika mkutano huo Tanzania iliteuliwa kuwa mjumbe wa Baraza la Amani na Usalama la Umoja wa Afrika kwa kipindi cha miaka miwili kuanzia Aprili 2022 hadi Aprili 2024.
- Mheshimiwa Spika, nilimwakilisha Mheshimiwa Rais katika Mkutano wa 16 wa Dharura wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Umoja wa Afrika uliofanyika tarehe 27-28 Mei 2022 jijini Malabo, Equatorial Guinea. Mkutano huo ulijadili masuala ya Majanga na Huduma za Kibinadamu; na Ugaidi, Siasa na Itikadi Kali na Mabadiliko ya Serikali yasiyozingatia misingi ya katiba.
- Mheshimiwa Spika, Mkutano huo pamoja na masuala mengine, ulikubaliana yafuatayo: Kuunda Jeshi la Afrika (African Standby Force) na Brigedi za Kikanda; Kuimarisha ushirikiano na mshikamano; Kujenga uwezo wa nchi zetu kukabiliana na majanga mbalimbali ya asili na kushughulikia changamoto za katika ulinzi na usalama; Kuheshimu katiba na demokrasia; na Mpango wa Kujitathmini kwenye Masuala ya Utawala Bora (APRM).
Mkataba wa Eneo Huru la Biashara la Bara la Afrika (AfCFTA)
- Mheshimiwa Spika, mwezi Septemba 2021, Tanzania iliridhia Mkataba wa kuanzisha Eneo Huru la Biashara la Bara la Afrika. Kuridhiwa kwa Mkataba huu kunaongeza wigo wa fursa za kukuza soko la bidhaa na huduma za Tanzania katika soko la Afrika. Hatua hii pia itajibu kiu ya wafanyabiashara wa Tanzania kutaka kunufaika na fursa za masoko ya nchi nyingine za Afrika ambazo siyo wanachama wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika na Jumuiya ya Afrika Mashariki.
- Mheshimiwa Spika, mwezi Februari 2022, Mkutano wa 35 wa Wakuu wa Nchi na
Serikali wa Umoja wa Afrika uliofanyika Addis Ababa, Ethiopia ulielekeza nchi wanachama kufungua soko kwa asilimia 87.7 kati ya 90 zilizokubalika na kuendelea na majadiliano ya asilimia zilizobaki. Hadi sasa, nchi 29 kati ya 44 ikiwemo Tanzania zimewasilisha orodha ya bidhaa zitakazofunguliwa zinazokidhi vigezo vya mkataba huo.
4.3.4 Jumuiya ya Nchi za Ukanda wa Maziwa
Makuu (ICGLR)
150. Mheshimiwa Spika, mwezi Februari
2022, Wizara iliratibu na kufanikisha ushiriki wa
Tanzania katika Mkutano wa 10 wa Wakuu wa Nchi na Serikali zinazotekeleza Mpango wa Amani, Usalama na Ushirikiano nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) uliofanyika jijini Kinshasa, DRC. Mkutano huo ulijadili utekelezaji wa mpango wa kusitisha mapigano mashariki mwa DRC na maeneo mengine kwenye Ukanda wa Maziwa Makuu ili kuimarisha hali ya ulinzi na usalama katika ukanda huo.
4.3.5 Ushirikiano wa Kimataifa
151. Mheshimiwa Spika, mwezi Mei 2022, Wizara iliratibu na kufanikisha uzinduzi wa Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Miaka Mitano
2022 – 2027 wa ushirikiano kati ya Tanzania na Umoja wa Mataifa nchini. Mpango huo, unachukua nafasi ya Mpango wa Pili unaofikia tamati mwezi Juni 2022. Kupitia Mpango huo, Tanzania na Umoja wa Mataifa zitashirikiana kutekeleza maeneo ya vipaumbele ya Ajenda 2030.
- tarehe 25, Mei 2022 wakati wa Mkutano wa 48 wa mwaka wa Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB) uliofanyika Accra, Ghana, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan alipokea nishani ijulikanayo kama 2022 Super Prize Great Builder – Trophée Boubacar Ndiaye inayofadhiliwa na AfDB na kutolewa na Africa Road Builders (ARB). Tuzo hii ni kutambua mchango wa Mhe. Rais kwenye mafanikio ya ujenzi wa mtandao wa barabara na reli hapa nchini pamoja na uongozi wake kwenye usimamizi wa fedha nyingi zilizoingia kwenye ujenzi wa miundombinu.
- Mheshimiwa Spika, mwezi Machi 2022, Wizara iliratibu na kufanikisha mkutano wa ngazi ya juu kati ya Serikali na Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulikia Masuala ya Wakimbizi (UNHCR) uliofanyika jijini Dar es salaam. Mkutano huo ulikuwa na lengo kujadili masuala mbalimbali kuhusu uendeshaji wa shughuli za wakimbizi nchini, uratibu wa zoezi la kuwarudisha wakimbizi nchini mwao kwa hiari pamoja na haki na kinga za kidiplomasia wanazopata watumishi wa Shirika hilo nchini. Wakati wa mkutano huo, pande mbili zilisaini andiko la makubaliano na mapendekezo ya pamoja ya kuongeza ushirikiano, uwazi na mawasiliano ya mara kwa mara katika utekelezaji wa majukumu ya UNHCR hapa nchini.
- Mheshimiwa Spika, mwezi Septemba
2021, Wizara iliratibu na kufanikisha ushiriki wa Tanzania kwenye Mkutano wa 76 wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa (UN) uliofanyika jijini New York, Marekani ambapo ujumbe wa Tanzania uliongozwa na Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Katika mkutano huo, Mheshimiwa Rais aliieleza jumuiya ya kimataifa kuhusu juhudi zinazofanywa na Serikali katika kukabiliana na athari za kiafya, kijamii na kiuchumi zilizosababishwa na mlipuko wa UVIKO-19 duniani. Aidha, Tanzania ilisisitiza umuhimu wa jumuiya ya kimataifa kutumia majukwaa ya diplomasia majumui kukabiliana na matatizo yanayoikabili dunia.
- Mheshimiwa Spika, mwezi Oktoba 2021, Wizara iliratibu na kufanikisha ushiriki wa Tanzania kwenye Mkutano wa 26 wa Nchi Wanachama za Mkataba wa Umoja wa Mataifa kuhusu Mabadiliko ya Tabianchi (COP26) uliofanyika jijini Glasgow, Scotland. Katika Mkutano huo, Tanzania ilielezea dhamira yake ya kupunguza kiwango cha uzalishaji wa hewa ukaa kwa asilimia 30 hadi 35 ifikapo mwaka 2030. Vilevile, Tanzania ilieleza namna inavyotekeleza sera, mikakati na programu za uhifadhi wa mazingira na kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi ikiwemo upandaji miti takriban milioni 270 kila mwaka kwa lengo la kupunguza athari za hewa ukaa inayozalishwa kutokana na shughuli za kijamii na kiuchumi. Tanzania ilizihimiza nchi zilizoendelea kutimiza ahadi ya kuchangia kiasi cha Dola za Marekani bilioni 100 kila mwaka kwa nchi zinazoendelea kwa ajili ya kuziwezesha kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi kama ilivyokubaliwa katika Mkataba wa Mabadiliko ya Tabianchi wa Paris wa mwaka 2015.
- Mheshimiwa Spika, ninapenda kulitaarifu Bunge lako tukufu kuwa, katika Mkutano Mkuu wa 41 wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Elimu, Sayansi na Utamaduni (UNESCO) uliofanyika jijini Paris, Ufaransa mwezi Novemba 2021 Tanzania ilichaguliwa kuwa mjumbe wa Bodi ya Shirika hilo kwa kipindi cha miaka minne (2021-2025). Vilevile, katika Mkutano huo tarehe 7 Julai ilitangazwa kuwa Siku ya Kiswahili Duniani. Kwa hatua hiyo lugha ya Kiswahili inakuwa ya kwanza Afrika na ya nane duniani kuwa na siku maalum ya kuadhimishwa. Lugha nyingine zenye siku maalum za kuadhimishwa ni: Kiarabu (18 Desemba); Kichina (20 Aprili); Kiingereza (23 Aprili); Kifaransa (20 Machi); Kirusi (06 Juni); Kihispania (23 Aprili); na Kireno (5 Mei). Wizara kupitia Balozi zetu inaendelea na Mikakati ya kuadhimisha siku hii kwa lengo la kukibidhahisha Kiswahili.
- Mheshimiwa Spika, aidha, katika
Mkutano Mkuu wa 27 wa UPU uliofanyika Abidjan, Côte d’Ivoire mwezi Agosti 2021 Tanzania ilichaguliwa kuwa Mjumbe wa Baraza la Utawala (CA) na Baraza la Uendeshaji (POC) la Umoja wa Posta Duniani (UPU) kwa kipindi cha miaka minne (2021-2025).
- Mheshimiwa Spika, kuanzia mwezi Januari 2022 Tanzania imekua ni miongoni wa wajumbe 54 wa Baraza la Uchumi na Jamii la
Umoja wa Mataifa. Tanzania itashikilia nafasi hiyo kwa kipindi cha miaka mitatu (2022-2024). Baraza hilo ndilo chombo muhimu kinachoratibu shughuli za kijamii na kiuchumi za Umoja wa Mataifa na mashirika yake yote. Vilevile, chombo hicho husimamia ajenda za maendeleo endelevu na miradi yote ya Umoja wa Mataifa kupitia mashirika yake kama vile UNDP, UNFPA na UNHCR.
- Mheshimiwa Spika, mafanikio haya ya Tanzania kuchaguliwa kuwa mjumbe kwenye vyombo mbalimbali vya maamuzi vya mashirika ya kimataifa ni ishara ya ukomavu wa diplomasia ya nchi yetu kimataifa. Aidha, ni fursa ya kusaidia kuwaongezea uwezo wa kiutendaji watalaam wetu watakaoshiriki katika shughuli za Mashirika hayo.
- Mheshimiwa Spika, mwezi Julai 2021, Wizara iliratibu na kufanikisha ushiriki wa Tanzania katika Jukwaa la Kizazi Chenye Usawa lililofanyika Paris, Ufaransa. Jukwaa hilo lilifanyika mahsusi kujadili tathmini ya miaka 25 ya utekelezaji wa Beijing Declaration and Platform for Action 1995 na kuweka mikakati ya kuimarisha utekelezaji wake. Katika jukwaa hilo, Tanzania ilikasimiwa jukumu la kutekeleza eneo la Usawa wa Kiuchumi na Haki ambalo ni kati ya maeneo sita yaliyoainishwa katika mpango wa miaka mitano (2021-2026).
- Mheshimiwa Spika, ninapenda kuarifu kuwa Wizara iliratibu ushiriki wa nchi kwenye Mkutano wa 66 wa Kamisheni ya Umoja wa Mataifa ya Hali ya Wanawake Duniani uliofanyika jijini New York, Marekani mwezi Machi 2022. Mkutano huo ulipitisha makubaliano ya pamoja yanayolenga kufikia usawa wa kijinsia na uwezeshaji wa wanawake na wasichana katika masuala ya mabadiliko ya tabianchi.
4.4 Kufuatilia na Kusimamia Utekelezaji wa Makubaliano za Ushirikiano
Mikataba ya Kimataifa na Hati za
162. Mheshimiwa Spika, Wizara iliratibu na kufanikisha kusainiwa kwa Mikataba na Hati za Makubaliano ya Ushirikiano zinazolenga kuimarisha uhusiano na ushirikiano uliopo kati ya Tanzania na nchi nyingine, jumuiya za kikanda na kimataifa. Wizara inaendelea kufuatilia utekelezaji wa Hati na Mikataba hiyo inayosimamiwa na Wizara, Taasisi na sekta binafsi kulingana na maudhui yake ili kuhakikisha nchi inanufaika. Orodha ya Mikataba na Hati hizo imeambatishwa kwenye kitabu cha Hotuba yangu.
4.5Kuratibu Masuala ya Itifaki, Uwakilishi na
Huduma za Kikonseli
- Mheshimiwa Spika, Wizara imeendelea kuratibu masuala ya haki na kinga kwa Jumuiya Wanadiplomasia hapa nchini kama ilivyoainishwa katika sheria za kimataifa hususan Mkataba wa Vienna kuhusu Uhusiano wa Kidiplomasia wa mwaka 1961 na Waraka Na. 2 wa Rais wa mwaka 1964 kuhusu Mawasiliano baina ya Taasisi za Serikali na Jumuiya Wanadiplomasia.
- Mheshimiwa Spika, katika kipindi hiki, Wizara imeratibu uwasilishaji wa Hati za Utambulisho kwa mabalozi wa nchi za Australia, Belarus, Chile, China, Colombia, India, Indonesia, Jamhuri ya Czech, Jamhuri ya Korea, Malawi, Morocco, Saudi Arabia, Ufaransa na Uholanzi. Aidha, katika kuimarisha uhusiano na Jumuiya ya Wanadiplomasia hapa nchini, Wizara imeimarisha utaratibu wa mashauriano kuhusu utekelezaji wa sera, mikakati na mipango ya maendeleo.
- Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kuongeza wigo wa uwakilishi nje ya nchi kwa kuzingatia maslahi mapana ya Taifa. Katika kipindi hiki, Ubalozi na Uwakilishi wa Kudumu wa Tanzania Umoja wa Mataifa Vienna, Austria; Ubalozi wa Tanzania Jakarta, Indonesia na Konseli Kuu mbili katika jiji la Lubumbashi, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, na jiji la Guangzhou, China zimefunguliwa. Hatua hiyo inaifanya Tanzania kuwa na jumla ya Balozi 45 na Konseli Kuu tano.
- Mheshimiwa Spika, Wizara imeendelea kutoa huduma za kiitifaki na kikonseli ikiwa ni pamoja na upatikanaji wa viza kwa maafisa na watendaji wa Serikali, viongozi wa vyama vya siasa na Waheshimiwa Wabunge. Aidha, Wizara imeendelea kutafuta ufumbuzi wa changamoto mbalimbali zinazowakabili Watanzania nje ya nchi kwa kushirikiana na wadau wengine na kulinda maslahi ya Watanzania wanaofanya kazi kwenye Balozi na Mashirika ya Kimataifa hapa nchini.
- Mheshimiwa Spika, Wizara iliratibu na kufanikisha ziara za kikazi na kitaifa za viongozi wakuu wa kitaifa katika nchi mbalimbali kama ifuatavyo:
- Ziara ya kikazi ya Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania nchini Ghana mwezi Mei 2022 kwenye Mkutano 48 wa Mwaka wa Benki ya
Maendeleo ya Afrika (AFDB);
- ya kitaifa ya Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania nchini Uganda kwa mwaliko wa Mheshimiwa Yoweri Kaguta Museveni, Rais wa Jamhuri ya Uganda, mwezi Mei 2022;
- Ziara ya kikazi ya Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania nchini Marekani kuzindua filamu maalum ya Tanzania Royal Tour, mwezi Aprili
2022; iv. Ziara ya kikazi ya Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika Umoja wa Falme za Kiarabu kushiriki Maonesho Kimataifa ya Dubai
(Dubai Expo 2020), mwezi Februari 2022;
v. Ziara ya kikazi ya Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania nchini Ubelgiji kushiriki Mkutano wa Sita wa Ushirikiano kati ya Umoja wa
Ulaya na Afrika, mwezi Februari 2022; vi. Ziara ya kikazi ya Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania nchini Ufaransa kushiriki Mkutano wa Wakuu wa Nchi na Serikali kuhusu
Bahari Kuu, mwezi Februari 2022; vii. Ziara ya kikazi ya Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania nchini Scotland kushiriki Mkutano wa 26 wa Nchi Wanachama za Mkataba wa Umoja wa Mataifa kuhusu Mabadiliko ya
Tabianchi, mwezi Novemba 2021;
viii. kitaifa Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania nchini Misri kwa mwaliko wa
Mheshimiwa Abdel Fattah el-Sisi, Rais wa Jamhuri ya Kiarabu ya Misri, mwezi Novemba
2021; ix. Ziara ya kikazi ya Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania nchini Marekani kushiriki Mkutano wa 76 wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa, mwezi Septemba 2021;
- Ziara ya kitaifa ya Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania nchini Rwanda kwa mwaliko wa Mheshimiwa Paul Kagame, Rais wa Jamhuri ya Rwanda, mwezi Agosti 2021;
- Ziara ya kikazi ya Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania nchini Malawi kushiriki Mkutano wa 41 wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa
SADC mwezi Agosti 2021; xii. Ziara ya Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania nchini Zambia kushiriki sherehe ya uapisho wa Mheshimiwa Hakainde Hichilema, Rais wa
Jamhuri ya Zambia, mwezi Agosti 2021; xiii. Ziara ya kitaifa ya Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania nchini Burundi kwa mwaliko wa Mheshimiwa Gen. Évariste Ndayishimiye, Rais wa Jamhuri ya Burundi, mwezi Julai 2021;
xiv. ya kikazi ya Mheshimiwa Philip Isdor Mpango, Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania nchini Ethiopia kushiriki Mkutano wa 35 wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Umoja wa Afrika mwezi Februari 2022, akimwakilisha Mheshimiwa
Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania; xv. Ziara ya kikazi ya Mheshimiwa Philip Isdor Mpango, Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania nchini Malawi kushiriki Mkutano wa Dharura wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Asasi ya Ushirikiano katika Masuala ya Siasa, Ulinzi na Usalama ya Jumuiya ya SADC mwezi Januari 2022, akimwakilisha Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan Rais wa Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania; xvi. Ziara ya kikazi ya Mheshimiwa Philip Isdor Mpango, Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania nchini Singapore kushiriki Mkutano wa Jukwaa la Majadiliano ya Kiuchumi mwezi Novemba 2021, akimwakilisha Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania; xvii. Ziara ya Kikazi ya Mheshimiwa Philip Isdor Mpango, Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania nchini Ufaransa kushiriki Jukwaa la Kizazi Chenye Usawa mwezi Julai 2021, akimwakilisha Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania;
xviii. kikazi Mheshimiwa Dkt. Hussein Ali Mwinyi, Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi katika Umoja wa
Falme za Kiarabu mwezi Januari 2022; xix. Ziara ya kikazi ya Mheshimiwa Dkt. Hussein Ali Mwinyi, Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi nchini Afrika Kusini kushiriki Mkutano wa Ufunguzi wa Maonesho ya Kimataifa ya Biashara kwa Nchi za Afrika mwezi Novemba 2021;
- Ziara za kikazi za Mheshimiwa Kassim Majaliwa Majaliwa (Mb), Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika nchi za Qatar na Jordan mwezi Machi 2022, akimwakilisha Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania;
- Ziara ya kikazi ya Mheshimiwa Kassim Majaliwa Majaliwa (Mb), Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania nchini
Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo kushiriki
Mkutano wa 10 wa Wakuu wa Nchi wa
Serikali zinazotekeleza Mpango wa Amani, Usalama na Ushirikiano nchini DRC na kwenye Ukanda wa Maziwa Makuu mwezi Julai 2021, akimwakilisha Mheshimiwa
Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania; xxii. Ziara ya kikazi ya Mheshimiwa Kassim Majaliwa Majaliwa (Mb), Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania nchini
Morocco mwezi Julai 2021; na
xxiii. ya kikazi ya Mheshimiwa Kassim Majaliwa Majaliwa (Mb), Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania nchini Burundi kushiriki sherehe za maadhimisho ya miaka 59 ya Uhuru wa nchi hiyo mwezi Julai 2021, akimwakilisha Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
168. Mheshimiwa Spika, vilevile, Wizara iliratibu na kufanikisha ziara za viongozi wa Serikali na mashirika ya kimataifa hapa nchini kama ifuatavyo:
i. Ziara ya kitaifa ya Mheshimiwa Uhuru Muigai Kenyatta, Rais wa Jamhuri ya Kenya mwezi
Desemba 2021; ii. Ziara ya kitaifa ya Mheshimiwa Paul Kagame, Rais wa Jamhuri ya Rwanda mwezi Desemba
2021; iii. Ziara ya Mjumbe Maalum Mhe. Ahmed Bin Abudlaziz Kattan, Mshauri wa Mahakama ya
Kifalme kutoka kwa Mtukufu Salman Bin Abdulaziz Al Saud, Mfalme wa Saudi Arabia na Msimamizi wa Misikiti miwili Mitukufu;
- Ziara ya kikazi ya Mhe. Lord John Walney, Mjumbe Maalum wa Mhe. Boris Johnson, Waziri Mkuu wa Uingereza katika masuala ya biashara mwezi Novemba 2021;
- Ziara ya kikazi ya Mhe. Patricia Scotland, Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Madola mwezi
Mei 2022;
- kikazi Mhe. Kamina Smith, Waziri wa Mambo ya Nje na Biashara wa Jamaica mwezi Mei 2022;
- Ziara ya kikazi ya Mhe. Katja Keul, Waziri wa Nchi kwenye Wizara ya Mambo ya Nje ya Shirikisho la Jamhuri ya Ujerumani mwezi
Aprili 2022; viii. Ziara ya Kikazi ya Mhe. Dominique Hasler, Waziri wa mambo ya Nje wa Liechtenstein mwezi Machi, 2022;
- Ziara ya Dkt. Akinwumi Adesina, Rais wa Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB) mwezi
Februari 2022;
- Ziara ya kikazi ya Dkt Sidi Ould Tah, Mkurugezi Mtendaji wa Benki ya Maendeleo ya Nchi za Kiarabu (BADEA) mwezi Oktoba
2021;
- Ziara ya kikazi ya Amina J. Mohammed, Naibu Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa mwezi Septemba 2021;
- Ziara ya kikazi ya Dkt. Hafez Ghanem, Makamu wa Rais wa Benki ya Dunia mwezi
Septemba 2021; xiii. Ziara ya Mheshimiwa Sheikh Shakboot Nahyan Al- Nahyan, Mjumbe Maalumu wa
Mrithi wa Ufalme wa Abu Dhabi na Naibu
Kamanda Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi ya
Umoja Falme za Kiarabu mwezi Julai 2021; xiv. Ziara ya kikazi ya Mhe. Balozi Victoria Nuland,
Naibu Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani
anayeshughulikia masuala ya siasa mwezi
Agosti 2021; na xv. Ziara ya kikazi ya Mhe. Jakub Kulhanek, Waziri wa Mambo ya Nje wa Jamhuri ya Czech mwezi Oktoba 2021.
169. Mheshimiwa Spika, ziara hizo zinaendelea kuifungua Tanzania kimataifa katika azma ya kukuza na kutekeleza diplomasia ya uchumi.
4.6Uratibu wa Watanzania Wanaoishi Nje ya
Nchi (Diaspora)
- Mheshimiwa Spika, Wizara imeendelea kuhamasisha Diaspora kuchangia maendeleo nchini. Kutokana na jitihada hizo, mchango wa Diaspora umeendelea kuongezeka, ambapo kwa mujibu wa takwimu za Benki ya Kuu ya Tanzania fedha zilizotumwa na Diaspora nchini (remittances) ziliongezeka kutoka Dola za Marekani takribani milioni 400 mwaka 2020 hadi kufikia Dola za Marekani milioni 569.3 mwaka 2021. Diaspora pia wamewekeza kiasi cha Shilingi bilioni 3.9 katika mfuko wa UTT AMIS na kununua nyumba zenye thamani ya Shilingi bilioni 2.3 za Shirika la Nyumba la Taifa na mradi wa Hamidu City Park uliopo Kigamboni, Dar es Salaam.
- Mheshimiwa Spika, kadhalika, Diaspora wameendelea kutoa michango ya kijamii ambapo mwezi Machi 2022 jumuiya inayowaunganisha pamoja watanzania waliopo katika sekta ya afya nchini Uingereza (Tanzania – UK Healthcare Diaspora Association-TUHEDA) ilitoa vifaa tiba vyenye thamani ya Shilingi milioni 100 kwa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar. TUHEDA imekuwa chachu ya kuimarisha ushirikiano kati ya Tanzania na Uingereza, ambapo kwa sasa majadiliano yanaendelea kuhusu kusainiwa kwa Hati ya Makubaliano baina ya nchi hizi mbili yatakayoiwezesha Tanzania kunufaika na ubadilishanaji wa ujuzi, upatikanaji wa vifaa tiba na mafunzo kwa wauguzi na madaktari. Vilevile, jumuiya ya watanzania wanaoishi Marekani (Tanzania Diaspora Hub) imepanga kuwekeza nchini takribani Shilingi milioni 400 katika sekta ya uvuvi na kilimo mikoa ya Tanga, Njombe na
Singida.
- Mheshimiwa Spika, mwezi Aprili 2022, Wizara iliratibu na kufanikisha ziara ya Diaspora mwekezaji anayeishi nchini Canada ambaye amepanga kuwekeza nchini Dola za Marekani milioni 15 katika ujenzi wa barabara kwa kutumia teknolojia ya ‘geopolymer’, ambayo inatumia mabaki ya migodini na viwandani, hususan viwanda vinavyotengeneza alumina na vioo. Teknolojia hiyo ni mbadala wa matumizi ya saruji katika ujenzi wa barabara hapa nchini. Ninapenda kutambua michango ya Diaspora wengine ambayo iliekezwa katika sekta nyingine za kijamii na kiuchumi ambayo imesaidia kuleta maendeleo nchini.
- Mheshimiwa Spika, Wizara iliratibu na kufanikisha mikutano baina ya Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Diaspora wakati wa ziara nchini Kenya, Burundi, Ufaransa, Ubelgiji, Umoja wa Falme za Kiarabu na Marekani. Aidha, iliratibu na kufanikisha mkutano kati ya Mheshimiwa Dkt. Philip Isdor Mpango, Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Diaspora waliopo Singapore.
- Mheshimiwa Spika , Wizara ilishiriki mkutano wa Mheshimiwa Dkt. Hussein Ali Mwinyi, Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi na Diaspora wanaoishi katika nchi mbalimbali uliofanyika kwa njia ya mtandao. Vilevile, kwa nyakati tofauti nilikutana na kufanya mazungumzo na Diaspora wanaoishi nchini Kenya, Italia, Saudi Arabia, Jamhuri ya Korea na
Marekani.
- Mheshimiwa Spika , mikutano hiyo ilitoa fursa kwa Diaspora kupata taarifa za uwekezaji, ufafanuzi wa sera na mipango mbalimbali ya maendeleo nchini.
- Mheshimiwa Spika, pamoja na mapendekezo ya Sera ya Mambo ya Nje kuzingatia tamko la kisera kwa masuala ya Diaspora, ninapenda kulijulisha Bunge lako Tukufu kuwa, Wizara kwa kushirikiana na wadau ndani na nje ya Serikali ikiwemo Diaspora wenyewe inakamilisha Andiko Mahsusi litakalotoa mwongozo wa kisera kwa masuala yanayowahusu Diaspora. Ni matumaini yangu kuwa Andiko hili Mahsusi litatoa suluhisho la mambo mengine ya kisera na kisheria yanayohusu hadhi ya Diaspora ambayo yamekuwa kikwazo katika kuwahusisha Diaspora kuchangia Uchumi wa Taifa lao.
- Mheshimiwa Spika, naomba nichukue nafasi hii, kutoa shukrani kwa Diaspora na jumuiya zao kwa kuendelea kuchangia maendeleo ya uchumi nchini.
4.7Elimu kwa Umma
- Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha mwaka wa fedha 2021/2022 Wizara iliendelea kutoa elimu kwa umma kupitia vyombo vya habari vya ndani na nje ya nchi vikiwemo televisheni, redio na magazeti. Vilevile, kupitia majarida na vipeperushi; maonesho ya ndani na nje ya nchi mathalan maonesho ya sabasaba; na tovuti na mitandao rasmi ya kijamii ya wizara. Kupitia njia hizo wananchi wamefahamishwa kuhusu matokeo ya ziara za viongozi, fursa za masoko, ajira, uwekezaji na nafasi za masomo nje ya nchi.
- Mheshimiwa Spika, ninayo furaha kuliarifu Bunge hili kuwa, kwa miaka mitano Wizara imekuwa ikichapisha jarida maalum lenye kuelezea utekelezaji wa diplomasia ya uchumi katika Balozi zetu. Kupitia matoleo ya jarida hilo, Wizara imeelezea pamoja na mambo mengine namna ambavyo Waheshimiwa Mabalozi wanavyo tafuta masoko ya bidhaa zinazozalishwa nchini, kuvutia uwekezaji kutoka nje kutangaza utalii wa Tanzania katika maeneo yao ya uwakilishi. Pia,
Wizara iliandaa makala maalum ya televisheni (documentary) kuhusu utekelezaji wa diplomasia ya uchumi katika kipindi cha mwaka mmoja wa Serikali ya Serikali ya Awamu ya Sita na kuirusha katika vyombo vya habari nchini na mitandao ya kijamii.
- Mheshimiwa Spika, mwezi Desemba
2021, Wizara iliratibu ushiriki wa vijana wa vyuo vikuu vya Tanzania kwenye Mdahalo wa Saba wa Wanafunzi wa Vyuo Vikuu vya Afrika Mashariki. Lengo la mdahalo huo lilikuwa ni kupata washindi wawili kutoka kila nchi wanachama wa Jumuiya ambao wanapewa ubalozi wa vijana katika nchi zao na kukasimiwa majukumu ya kuelimisha vijana kuhusu mtangamano wa Jumuiya ya Afrika Mashariki.
- Mheshimiwa Spika, katika Mdahalo huo, Bw. Eben Mnzava na Bi. Bernadette Massawe kutoka Chuo Kikuu cha Dar es Salaam walishinda nafasi za Balozi na Naibu Balozi mtawalia. Wizara itashirikiana na vijana hawa katika kutoa elimu kwa vijana ili waweze kunufaika na fursa zinazopatikana katika Jumuiya ya Afrika
Mashariki.
- Mheshimiwa Spika, Wizara imeendelea kutoa elimu kuhusu masuala ya kikanda na kimataifa kwa makundi mbalimbali ambapo mwezi Septemba 2021 Wizara iliendesha mafunzo kwa wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama kuhusu diplomasia na ushirikiano wa kimataifa yaliyofanyika jijini Dar es Salaam. Vilevile, mwezi Februari 2022 Wizara iliandaa semina kuhusu masuala ya mtangamano wa Jumuiya ya Afrika Mashariki na fursa zake kwa wanafunzi wa Shule za Sekondari ya Jamhuri na Al-Hijra zilizopo mkoani Dodoma. Aidha, Wizara imefanya mikutano minne ya kidiplomasia (diplomatic briefings) na mabalozi na wakuu wa mashirika ya kikanda na kimataifa waliopo nchini kwa lengo la kutoa elimu na ufafanuzi kwa jumuiya hiyo ya kibalozi kuhusu utekelezaji wa sera, mipango na mikakati ya kitaifa ambapo katika kipindi hiki.
4.8Utawala na Maendeleo ya Watumishi 183. Mheshimiwa Spika, Wizara imeendelea kusimamia masuala ya utawala na maendeleo ya watumishi kwa lengo la kuimarisha utendaji kazi na kufanikisha malengo ya utekelezaji wa dhamana na majukumu yake. Hivi sasa, Wizara ina jumla ya watumishi 530 wa kada mbalimbali, ambapo watumishi 216 wapo katika Balozi za Tanzania nje ya nchi na 314 wapo Makao Makuu ya Wizara. Kati ya watumishi waliopo balozini, watumishi 138 wa kada na vyeo mbalimbali walipelekwa balozini katika mwaka wa fedha 2021/2022 ili kuimarisha utendaji katika Balozi za Tanzania nje ya nchi. Watumishi 62 walihudhuria mafunzo ya muda mrefu na mfupi katika fani mbalimbali ndani na nje ya nchi ili kuwajengea uwezo.
- Mheshimiwa Spika, katika kipindi hiki, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania alifanya uteuzi wa mabalozi 19 kuiwakilisha Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika nchi za Austria,
Brazil, Comoros, Ethiopia, India, Indonesia, Italia,
Israel, Kuwait, Jamhuri ya Demokrasia ya Kongo,
Jamhuri ya Korea, Japan, Malawi, Marekani, Misri, Qatar Rwanda, Sweden na Urusi. Vilevile, Wizara imewathibitisha kwenye vyeo wakuu wa Idara sita na kuwateua wakurugenzi wasaidizi nane.
- Mheshimiwa Spika, Wizara imeajiri watumishi wapya 11, kati yao 10 ni Maafisa Mambo ya Nje Daraja la Pili na mtumishi mmoja ni Katibu Muhtasi Daraja la Tatu. Aidha, watumishi 70 walihamishiwa wizarani kutoka katika wizara na taasisi nyingine za Serikali, watumishi 170 wa kada mbalimbali walipandishwa vyeo na watumishi tisa walibadilishwa kada baada ya kujiendeleza kielimu katika fani mbalimbali.
- Mheshimiwa Spika, ninapenda kuliarifu Bunge lako tukufu kuwa, ili kuboresha utekelezaji wa majukumu na malengo yake, Wizara imehuisha muundo wake kwa kuanzisha Idara mpya ya Diplomasia ya Uchumi. Aidha, Wizara imenunua vitendea kazi mbalimbali ikiwemo magari mapya 20 kwa ajili ya Makao Makuu na 37 kwa ajili ya Balozi zetu nje ya nchi kwa lengo la kuboresha mazingira ya utendaji kazi.
- Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2021/22, Wizara imeendelea na jukumu la kusimamia matumizi ya fedha na mali za Serikali. Matokeo ya usimamizi huu yanaonekana katika taarifa za kaguzi mbalimbali zinazofanywa na Wizara kupitia Kitengo cha Ukaguzi wa Ndani,
Mdhibiti na Mkaguzi wa Hesabu za Serikali, Mamlaka ya Udhibiti wa Ununuzi wa Umma, na vyombo vingine vya Serikali vya usimamizi. Kupitia Kitengo cha Ukaguzi wa Ndani, katika kipindi husika jumla ya balozi 16 Idara na Vitengo ndani ya Wizara zilikaguliwa. Kaguzi hizi zimesaidia sana kurekebisha kasoro mbalimbali za kiutendaji na hivyo kuhakikisha kunakuwepo na matumizi yenye kuzingatia thamani.
Usimamizi wa Rasilimali Fedha
188. Mheshimiwa Spika, ninayo furaha kulitaarifu Bunge lako Tukufu kwamba, Wizara na Balozi zake imepata Hati Safi za ukaguzi kwa miaka miwili mfululizo (2019/20 na 2020/21).
Ninapenda kulihakikishia Bunge lako kuwa, Wizara inaendelea kuboresha mifumo yake ya fedha na utunzaji wa mali za Serikali kwa mujibu wa sheria, taratibu na kanuni.
4.9Kuratibu na Kusimamia Utekelezaji wa Miradi ya Maendeleo ya Wizara na Taasisi Zilizo Chini ya Wizara
Utekelezaji wa Miradi ya Maendeleo ya
Wizara
- Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2021/2022, Wizara ilitengewa bajeti ya maendeleo ya Shilingi 13,500,000,000 kwa ajili ya kutekeleza miradi ya maendeleo iliyopo ndani na nje ya nchi. Napenda kulifahamisha Bunge lako Tukufu kuwa Wizara imekamilisha taratibu za ununuzi za kuwapata Wakandarasi watakaotekeleza miradi ya ujenzi na ukarabati kwenye Balozi zetu nje ya nchi. Miradi hiyo ni Ujenzi wa jengo la Ubalozi na Kitega uchumi katika Ubalozi wa Tanzania Nairobi – mkandarasi aliyepatikana ni CRJE (East Africa) Limited; ujenzi wa jengo la ubalozi na kitega uchumi katika ubalozi wa Tanzania Kinshasa, mkandarasi ni China Railways Construction Engineering Group Limited (CRCEG); ujenzi wa makazi ya jengo la ubalozi na makazi ya Balozi katika ubalozi wa Tanzania Muscat – Mkandarasi aliyepatikana ni Arab Contractors (Osman Ahmed Osman and Co); ujenzi wa jengo la ubalozi na kitega uchumi katika ubalozi wa Tanzania Comoro – mkandarasi aliyepatika ni SUMAJKT Construction Co. Limited; mradi wa ukarabati wa Jengo la zamani la ubalozi (R-street) katika ubalozi wa Tanzania Washington; usanifu wa ujenzi wa makazi ya Balozi katika Ubalozi wa Tanzania Addis Ababa; na ujenzi wa vyumba vya mihadhara Miradi hii iko katika hatua ya mikataba na utekelezaji wake utaanza kabla ya mwisho wa mwaka wa fedha 2021/22.
- Mheshimiwa Spika, maandalizi ya miradi hiyo yaliyohusisha kazi ya usanifu na uandaaji wa michoro ya ujenzi yamefanyika kwa kutumia fedha zilizotengwa katika mwaka wa fedha 2020/21 na kutunzwa katika akaunti ya amana ya Wizara. Fedha hizo zinazofikia shilingi bilioni 4.1 zimetumika pia kusanifu na kuandaa michoro kwa miradi idadi. itakayotekelezwa miaka ijayo kwa kufuata Mpango wa Wizara wa Uendelezaji wa viwanja na majengo Balozini. Miradi iliyosanifiwa na kuandaliwa michoro kwa utekelezaji miaka ijayo ni: Ujenzi ya Jengo la Ubalozi na Makazi ya Balozi katika Ubalozi wa Tanzania Riyadh; Ujenzi wa Jengo la Kitega Uchumi katika Ubalozi wa Tanzania Maputo; Ujenzi wa Jengo la la Kitega Uchumi katika Ubalozi wa Tanzania Lilongwe; Ujenzi wa Jengo la Kitega Uchumi na Makazi ya Watumishi katika ubalozi wa Tanzania Kigali; Ujenzi wa Jengo la Ubalozi na Makazi ya Balozi katika Ubalozi wa Tanzania Kigali; Ujenzi ya Jengo la Kitega Uchumi na Makazi ya Watumishi katika Ubalozi wa Tanzania Bujumbura; na Ukarabati wa Makazi ya Balozi katika Ubalozi wa Tanzania Harare.
- Mheshimiwa Spika, Wizara imeweza pia kutumia fedha zilizotengwa katika bajeti ya mwaka 2020/21 kukarabati majengo matano (5) ya makazi ya watumishi katika Ubalozi wa Tanzania Lusaka (Zambia) uligharimu shilingi Milioni 600. Hatua hii imewezesha watumishi wote wa ubalozi katika ubalozi huo kukaa katika nyumba za serikali na kuiokolea serikali fedha za pango. Aidha, Wizara imeweza kutumia kiasi cha shililingi 341,941,115.00 kukarabati jengo la ofisi za Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika
Mashariki Zanzibar.
- Mheshimiwa Spika, vilevile, ipo miradi ya maendeleo ambayo utekelezaji wake uliendelea katika mwaka wa fedha 2021/2022 kwa kutumia fedha zilizotengwa miaka iliyopita na zilizokuwa kwenye akaunti za amana za balozi husika. Hatua iliyofikiwa katika utekelezaji wa miradi hiyo ni kukamilika kwa ukarabati wa jengo la Ubalozi wa Tanzania Stockholm (Sweden); kuendelea na ukarabati wa makazi ya balozi na nyumba moja ya afisa katika Ubalozi wa Tanzania Stockholm (Sweden); kuendelea na ukarabati wa majengo matatu (3) ya Ubalozi wa Tanzania Kampala (Uganda); kuendelea na ukarabati wa jengo la ofisi na makazi ya Balozi wa Tanzania Brussels (Ubelgiji); na kuendelea na ukarabati wa jengo la ofisi na makazi ya Balozi wa Tanzania Khartoum
(Sudan).
- Mheshimiwa Spika, pamoja na maelezo hayo, ninayo furaha kulifahamisha Bunge lako Tukufu kuwa Wizara inaendelea na majadiliano na Benki ya CRDB kuhusu kushirikiana na katika ujenzi wa majengo ya ofisi, vitega uchumi na makazi ya watumishi balozini. Aidha, Wizara itaendelea kufanya majadiliano na taasisi nyingine za fedha ili kufanikisha azma hiyo ikiwa ni utekelezaji wa maelekezo ya Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania aliyotoa wakati wa uzinduzi wa jengo la makao makuu ya CRDB jijini Dar es Salaam tarehe 05 Machi, 2022.
4.10 Taasisi Zilizo Chini ya Wizara
194. Mheshimiwa Spika, katika kipindi hiki, Wizara imeendelea kuzisimamia taasisi zilizo chini yake ambazo ni: Kituo cha Kimataifa cha Mikutano Arusha (AICC); Chuo cha Diplomasia (CFR); na Mpango wa Hiari wa Afrika wa
Kujitathmini katika Masuala ya Demokrasia na Utawala Bora (APRM) katika kutekeleza majukumu yao kama ifuatavyo:
4.11 Kituo cha Kimataifa cha Mikutano
Arusha (AICC)
- Mheshimiwa Spika, majukumu ya AICC ni kuendesha biashara ya mikutano na upangishaji wa nyumba na ofisi. Aidha, kituo kinatoa huduma ya afya kupitia hospitali yake.
- Mheshimiwa Spika, Kituo kinatekeleza majukumu yake kwa kuongozwa na Mpango
Mkakati wa miaka mitano (2022/23-2026/2027), unaoainisha dira na dhima ya kuitangaza nchi yetu katika nyanja ya utalii wa mikutano na matukio ambayo inajulikana kama ‘’MICE’’ (Meetings, Incentive travel, Conferences,
Exhibition/Events).
- Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2021/2022 Kituo kilipanga kukusanya mapato ya shilingi 16,202,606,216. Hadi mwezi Aprili 2022 Kituo kilikusanya mapato ya shilingi 10,351,041,115.15 sawa na asilimia 64 ya malengo. Lengo la makusanyo halikufikiwa kutokana na shughuli za kituo kuendelea kuathirika na UVIKO-19 ambao umechangia kupungua kwa idadi ya mikutano.
- Mheshimiwa Spika, mapato hayo
yalitokana na;
- Huduma za kumbi za mikutano (AICC na JNICC) – shilingi 4,242,707,034 kati ya lengo la shilingi 4,634,077,500;
- Upangishaji wa ofisi na nyumba za kuishi shilingi 2,938,029,855 kati ya lengo la shilingi 3,634,506,432; na
- Huduma za hospitali – shilingi 3,170,304,225 kati ya lengo la shilingi 3,883,370,730.
- Mheshimiwa Spika, vilevile katika kipindi hicho, kituo kilitekeleza yafuatayo:
- Kuhudumia mikutano 239 ya kitaifa na 12 ya kimataifa ambayo ilileta washiriki 52,072 wa kitaifa na kimataifa. Aidha, Kituo kilifanikisha uzinduzi wa filamu maalum ya kutangaza utalii wa Tanzania ya The Royal Tour uliofanyika tarehe 28 Aprili, 2022 ukumbi wa AICC jijini Arusha na tarehe 8 Mei, 2022 jijini Dar es Salaam katika ukumbi wa JNICC;
- Kukamilisha tathmini ya mazingira ikiwa ni utekelezaji wa hatua za awali za mradi wa Ujenzi wa Mount Kilimanjaro International
Convention Centre;
- Kutoa huduma mbalimbali za afya kwa wagonjwa wa nje 71,220 na waliolazwa 1,300;
- Kuandaa na kuratibu kongamano la Asasi za wataalam wa hapa nchini kwa lengo la kuibua na kuvutia mikutano ya kimataifa kufanyika hapa nchini;
- Kufanya maboresho ya mifumo ya menejimenti ya usimamizi wa taarifa katika nyanja za rasilimali watu, miliki na
uendeshaji wa hospitali;
- Kufanya ukarabati wa nyumba za makazi na ofisi za kituo zilizopo Arusha; na
- Kukamilisha mpango wa mafunzo na kukamilisha zoezi la kuhuisha muundo wa utumishi.
- Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha Julai 2021 hadi Machi 2022 kituo kilitoa Shilingi 100,000,000 ikiwa ni gawio la awali kwa Serikali.
4.11.1 Chuo cha Diplomasia
- Mheshimiwa Spika, Chuo cha
Diplomasia kimeendelea kutoa mafunzo mbalimbali katika maeneo ya uhusiano wa kimataifa, diplomasia, utatuzi wa migogoro na kuimarisha amani, stratejia, ulinzi na usalama na lugha za kigeni.
- Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha wa 2021/2022, Chuo kilipanga kukusanya na kutumia jumla ya shilingi 7,960,040,070. Kati ya hizo, shilingi 4,300,640,000 ni ruzuku kutoka Serikali kuu na shilingi 3,659,400,070 ni mapato kutoka vyanzo vya ndani. Katika fedha za ruzuku kutoka Serikali kuu, shilingi 2,300,640,000 ni ruzuku ya mishahara, shilingi 1,000,000,000 ni ruzuku ya Miradi ya Maendeleo na shilingi 1,000,000,000 ni ruzuku ya matumizi mengineyo.
- Mheshimiwa Spika, hadi kufikia mwezi Aprili 2022, Chuo kimepokea jumla ya shilingi 5,937,257,608.00 ambayo ni sawa asilimia 74.5 ya lengo. Katika fedha hizo, shilingi 2,794,099,075.00 ni kutoka vyanzo vya ndani, shilingi 2,162,390,130.00 ni ruzuku ya mishahara na shilingi 833,333,333.00 ni ruzuku ya matumizi mengineyo kutoka Serikali Kuu.
- Mheshimiwa Spika, kwa upande wa matumizi, hadi kufikia mwezi Aprili 2022 Chuo kimetumia jumla shilingi 5,783,383,323.00 sawa na asilimia 97.4 Kati ya fedha hizo, shilingi 2,941,534,145.00 ni kutoka vyanzo vya ndani, shilingi 2,162,390,130.00 ni ruzuku ya mishahara kutoka Serikali Kuu na shilingi 679,459,048.00 ni ruzuku ya matumizi mengineyo kutoka Serikali Kuu.
- Mheshimiwa Spika, hadi kufikia mwezi Machi 2022, Chuo kimedahili jumla ya wanafunzi 1,617 katika ngazi mbalimbali za astashahada, stashahada, shahada na stashahada ya uzamili. Kati ya wanafunzi hao wanawake ni 790 na wanaume ni 827. Aidha, Chuo kimeendelea kutoa mafunzo ya muda mfupi kwa watumishi wa wizara mbalimbali, taasisi na mashirika ya umma, taasisi binafsi, waambata na mabalozi walioteuliwa kuiwakilisha Tanzania katika nchi mbalimbali. Ninapenda kulifahamisha kBunge hili kuwa Chuo kwa kushirikiana na Wizara kilitoa mafunzo kwa waheshimiwa wabunge ambao ni wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama yaliyofanyika mwezi Septemba 2021 jijini Dar es Salaam.
- Mheshimiwa Spika, chuo kimeendelea kuboresha miundombinu ya kufundisha na kujifunzia kwa kukarabati miundombinu iliyoharibika na ununuzi wa vifaa na vitendea kazi.
Kadhalika chuo kimeendelea kuwajengea uwezo watumishi wake kitaaluma ambapo kwa mwaka wa fedha 2021/2022 watumishi 25 wamehudhuria mafunzo ya muda mrefu. Kati ya hao watumishi 2 wamehitimu masomo ya ngazi ya Shahada ya Uzamili na watumishi 23 wanaendelea na mafunzo.
4.11.2 Mpango wa Hiari wa Afrika wa Kujitathmini katika Masuala ya Demokrasia na Utawala Bora
- Mheshimiwa Spika, Mpango wa Hiari wa
Afrika wa Kujitathmini katika Masuala ya
Demokrasia na Utawala Bora (APRM) ni Wakala Maalum wa Umoja wa Afrika ulioanzishwa mwaka 2003. Lengo la Mpango huo ni kufanya tathmini za mara kwa mara za utawala bora zenye nia ya kuimarisha maeneo ambayo nchi inafanya vizuri, kuibua changamoto za utawala bora na kutoa mapendekezo ya namna ya kuzitafutia ufumbuzi. Aidha, Mpango huo unawezesha nchi wanachama wa APRM kwa pamoja kubadilishana uzoefu katika masuala ya demokrasia na utawala bora.
- Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha Julai 2021 hadi Aprili 2022, APRM Tanzania ilitekeleza majukumu yake kulingana na malengo makuu yaliyoainishwa kwenye Mpango Mkakati wa APRM Tanzania (2017 – 2022) unaohuishwa kila mwaka, na kwa kuzingatia Mpango kazi na bajeti ya mwaka 2021/2022. Malengo yaliyotekelezwa kwa kipindi hiki ni kama ifuatavyo:
i. Kuimarisha uratibu wa utekelezaji wa
Mpango Kazi wa APRM Tanzania; ii. Kuimarisha uhamasishaji na mawasiliano kwa umma; na
iii. Kuhakikisha kuwa shughuli za APRM
Tanzania zinakuwa endelevu.
- Mheshimiwa Spika, bajeti iliyoidhinishwa na Bunge kwa ajili ya shughuli za APRM Tanzania kwa mwaka wa fedha 2021/2022 ni shilingi 800,000,000. Katika kipindi cha Julai 2021 hadi Aprili 2022, APRM Tanzania ilipokea jumla ya shilingi 492,503,239.85. Hadi kufikia mwezi Machi 2022 APRM Tanzania ilitumia kiasi cha shilingi 392,976,554.13 sawa na asilimia 95.3 ya fedha ilizopokea.
- Mheshimiwa Spika, katika kipindi hiki APRM Tanzania imekamilisha rasimu ya utekelezaji wa Mpango Kazi wa APRM. Rasimu hiyo inahusu hatua zilizochukuliwa katika kutatua changamoto za utawala bora zilizobainishwa katika tathmini iliyofanyika mwaka 2020 ambayo imeangazia maeneo manne ya tathmini: siasa na demokrasia, usimamizi wa uchumi, utendaji wa mashirika ya biashara na maendeleo ya jamii. Taarifa hiyo ina maelezo yaliyofanyiwa utafiti kwa kipindi cha mwaka 2014 hadi 2019.
- Mheshimiwa Spika, tathmini imeonesha kuwa Tanzania imepata mafanikio katika eneo la siasa na demokrasia kutokana na hatua zilizochukuliwa kutatua changamoto katika eneo hili. Baadhi ya mafanikio yaliyoainishwa ni utatuzi wa migogoro; kufanyiwa kazi kwa maeneo sita ya muungano; mageuzi katika utumishi wa umma; na uimarishaji wa taasisi za kuzuia na kupambana na rushwa. Aidha, haki za makundi ya wanawake, watoto, vijana na wakimbizi zimeendelea kulindwa kwa kuwekewa sera rafiki zinazosimamia maslahi ya makundi haya.
- Mheshimiwa Spika, katika eneo la usimamizi wa uchumi, tathmini imeonesha Tanzania imeendelea kutekeleza sera za uchumi mpana zinazolenga kupata maendeleo endelevu. Pia, katika eneo la usimamizi wa mashirika ya biashara, Serikali imeimarisha mfumo wa udhibiti wa mashirika ya biashara ili kuinua mchango wa mashirika hayo katika maendeleo ya Taifa. Vilevile, katika eneo la maendeleo ya jamii, Serikali imeendelea kuchukua hatua za kuimarisha ukusanyaji wa kodi kwa lengo la kuwa na uwezo wa kujitegemea na kuimarisha utoaji wa huduma mbalimbali za jamii.
- Mheshimiwa Spika, mwezi Februari 2022, APRM Tanzania ilishiriki katika mkutano wa Wakuu wa Nchi zilizojiunga na Mpango wa APRM. Katika mkutano huo, Tanzania ilieleza dhamira yake ya kuendelea kutekeleza Mpango huo kwa kuwa unatoa nafasi kwa Serikali kujitathmini na kuendelea kuimarisha na kuboresha maeneo yenye upungufu.
- Mheshimiwa Spika, katika kipindi hiki APRM Tanzania iliandaa Mwongozo wa Udhibiti wa Vihatarishi kama rejea mojawapo ya kuwezesha kuimarisha utawala bora ndani ya Taasisi na kutoa mchango wa kufikia malengo yake. Mwongozo huu ni dira ya kuzingatia katika utekelezaji wa shughuli za kila siku za Taasisi, kufanya maamuzi mbalimbali, mifumo, taratibu na kanuni ili kupata ufanisi na kufikia malengo yaliyokusudiwa.
- Mheshimiwa Spika, pia katika kipindi hiki Taasisi ilihuisha Mpango Mkakati wake wa mwaka 2016/2017 – 2021 utakaotekelezwa kwa kipindi cha miaka mitano ambayo ni 2021/2022 – 2025/2026. Mpango ulihuishwa kwa kushirikisha wadau mbalimbali wa APRM na pia umezingatia mahitaji ya Taasisi katika Awamu ya Pili ya tathmini pamoja na mabadiliko mengine yanayotazamiwa katika nyanja za uchumi, demokrasia, siasa na maendeleo kwa ujumla.
5.0 CHANGAMOTO NA HATUA ZILIZOCHUKULIWA
216. Mheshimiwa Spika, pamoja na kuwepo mafanikio ya kiutendaji katika kutekeleza bajeti ya mwaka wa fedha 2021/2022, Wizara ilikabiliwa na changamoto ya upungufu wa watumishi ikilinganishwa na wingi wa majukumu. Wizara imeendelea kuwasiliana na mamlaka ya ajira kwa ajili ya kupata vibali vya ajira mpya na ajira mbadala.
6.0 SHUKRANI
217. Mheshimiwa Spika, katika kufanikisha mipango mbalimbali ya maendeleo inayotekelezwa na Serikali yetu chini ya uongozi mahiri wa Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Serikali imeendelea kupata ushirikiano mzuri kutoka kwa wadau mbalimbali na washirika wa maendeleo kutoka nchi na asasi za kikanda na kimataifa. 218. Mheshimiwa Spika, kwa mkatadha huu, ninaomba nitumie fursa hii kuzishukuru nchi za Afrika Kusini, Algeria, Angola, Australia, Austria,
Bangladesh, Brazil, Botswana, Burundi, Canada,
China, Comoros, Cuba, Denmark, Ethiopia,
Eswatini, Finland, Hispania, Hungary, Italia, Iran,
Ireland, Indonesia, India, Israel, Jamhuri ya Czech,
Jamhuri ya Demokrasia ya Kongo, Jamhuri ya Korea, Japan, Kenya, Kuwait, Lesotho,
Madagascar, Malawi, Malaysia, Marekani,
Mauritius, Mexico, Misri, Morocco, Msumbiji,
Namibia, New Zealand, Nigeria, Norway, Oman,
Pakistan, Poland, Qatar, Romania, Rwanda,
Singapore, Sri Lanka, Thailand, Tunisia, Ubelgiji,
Zambia, Zimbabwe, Uganda, Saudi Arabia,
Shelisheli, Sudan, Sudani ya Kusini, Sweden,
Ufaransa, Uholanzi, Uingereza, Ujerumani, Ukraine, Umoja wa Falme za Kiarabu, Ureno , Urusi, Uswisi, Uturuki, na Vietnam.
219. Mheshimiwa Spika, vilevile ninaomba kutoa shukrani kwa African Capacity Building Foundation (ACBF); Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB); Benki ya Dunia; Investment Climate Facility for Africa; Mfuko wa Kimataifa wa Maendeleo ya Kilimo (IFAD); Shirika la Maendeleo ya Kimataifa la Uingereza (DfID); Mfuko wa Maendeleo wa Abu Dhabi (ADFD); Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF); Mfuko wa Maendeleo wa Kuwait (Kuwait Fund); Shirika la Nguvu za
Atomiki Duniani (IAEA); Shirika la Maendeleo ya Kimataifa la Sweden (SIDA); Shirika la Kimataifa la Kuzuia Matumizi ya Silaha za Kemikali (OPCW); Ofisi ya Mwakilishi Mkazi wa Umoja wa Mataifa
(UN RCO); Mfuko wa Kukuza Mtaji wa Umoja wa
Mataifa (UNCDF); Programu ya Maendeleo ya
Umoja wa Mataifa (UNDP); Shirika la Umoja wa
Mataifa la Idadi ya Watu (UNFPA); Shirika la Umoja wa Mataifa la Kupambana na UKIMWI (UNAIDS); Shirika la Umoja wa Mataifa la Kilimo na Chakula (FAO); Shirika la Umoja wa Mataifa la Elimu, Sayansi na Utamaduni (UNESCO); Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulikia Wakimbizi (UNHCR); Shirika la Kazi Duniani (ILO); Shirika la
Umoja wa Mataifa la Uhamaji (IOM); Shirika la
Umoja wa Mataifa la Kuhudumia Watoto (UNICEF);
Shirika la Maendeleo la Kimataifa la Israel (MASHAV); Shirika la Kimataifa la Maendeleo la Japan (JICA); Shirika la Misaada la Marekani (USAID); Shirika la Kimataifa la Maendeleo la Korea (KOICA); na Shirika la Maendeleo ya Viwanda la Umoja wa Mataifa (UNIDO).
220. Mheshimiwa Spika, mashirika mengine ni Shirika la Umoja Mataifa linaloshughulikia Masuala ya Wanawake (UNWOMEN); Shirika la
Mazingira la Umoja wa Mataifa (UNEP); Shirika la Umoja wa Mataifa la Biashara na Maendeleo
(UNCTAD); Shirika la Umoja wa Mataifa Kuhusu Madawa ya Kulevya na Uhalifu (UNODC); Umoja wa Ulaya (EU); Shirika la Afya Duniani (WHO); na Shirika la Mpango wa Chakula Duniani (WFP). Vilevile, napenda kuwashukuru Benki ya Kiarabu kwa Maendeleo ya Kiuchumi ya Afrika (BADEA); Benki ya Uwekezaji ya Ulaya (EIB); Shirika la Ushirikiano wa Kimataifa la Ujerumani (GiZ); Global Fund; International Committee of the Red Cross; International Federation of the Red Cross and Red Crescent Societies; Sekretarieti ya Jumuiya ya Madola; Khalifa Fund for Enterprise
Development (Khalifa Fund); Medecins Sans Frontieres; Mfuko wa Dunia wa Wanyama Pori (WWF); The Association of European
Parliamentarians with Africa; The Bill and Melinda Gates Foundation;TradeMark East Africa (TMEA); Umoja wa Posta Duniani (UPU); Umoja wa Posta Afrika (PAPU) pamoja na Mifuko na Mashirika mbalimbali ya Misaada. Ni dhahiri kuwa ushirikiano wao umekuwa na mchango mkubwa katika kufanikisha malengo ya Wizara, na Serikali kwa ujumla.
221. Mheshimiwa Spika, kwa dhati kabisa napenda kuwashukuru watendaji na watumishi wa Wizara na Taasisi zake kwa kuniwezesha kutekeleza majukumu yangu ya kulinda na kutetea maslahi ya Taifa letu ndani na nje ya nchi. Kwa namna ya pekee, ninapenda kumshukuru Mhe. Balozi Mbarouk Nassor Mbarouk (Mb), Naibu
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika
Mashariki; Balozi Joseph Edward Sokoine, Katibu
Mkuu; Balozi Fatma Mohammed Rajab, Naibu
Katibu Mkuu; Waheshimiwa Mabalozi wa Tanzania; Wakuu wa Idara na Vitengo; Wakuu wa Taasisi zilizo chini ya Wizara; na watumishi wote kwa kufanya kazi kwa umahiri, weledi, ufanisi, moyo wa uzalendo na kujitoa kulinda na kutetea maslahi ya Taifa letu.
7.0 MALENGO YA WIZARA KWA MWAKA WA
FEDHA 2022/2023
222. Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2022/2023, Wizara imeweka kipaumbele katika kutekeleza majukumu yafuatayo:
- Kuendelea kulinda na kutetea misingi ya Taifa letu ndani na nje ya nchi;
- Kuendelea kutekeleza diplomasia ya uchumi ikiwa ni pamoja na kuwezesha Balozi zetu kuwa kiungo muhimu katika kuvutia uwekezaji; kutafuta masoko ya bidhaa na huduma zinazozalishwa nchini; kutafuta misaada na mikopo yenye masharti nafuu; na kutafuta fursa za ajira na masomo kwa
watanzania nje ya nchi;
- Kuendelea kuimarisha uhusiano na nchi nyingine na jumuiya ya kimataifa;
- Kuendelea kutangaza na kuhamasisha matumizi ya lugha ya Kiswahili nje ya nchi;
- Kuendelea kuweka mazingira wezeshi na kuhamasisha ushiriki wa Watanzania wanaoishi nje katika kuchangia maendeleo ya nchi;
- Kuendelea kushiriki katika juhudi za kulinda na kuimarisha amani duniani na maendeleo kupitia Umoja wa Mataifa;
- Kuendela kushiriki kikamilifu katika kuimarisha mtangamamo wa Jumuiya ya Afrika Mashariki na Jumuiya ya Maendeleo
Kusini mwa Afrika; viii. Kuendelea kutoa elimu kwa umma kuhusu utekelezaji wa majukumu ya Wizara, masuala ya uhusiano wa kimataifa na mtangamano wa kikanda;
- Kuendelea kusimamia utekelezaji wa majukumu ya taasisi zilizopo chini ya Wizara;
- Kuendeleza viwanja vinavyomilikiwa na Serikali nje ya nchi na kukarabati majengo ya Balozi zetu ili kupunguza gharama na
kuchangia mapato ya Serikali;
- Kuendelea kubaini maeneo mapya kimkakati kwa lengo la kunufaika na fursa zilizopo kwa maslahi mapana ya Taifa; na
- Kuendelea kusimamia rasilimaliwatu na fedha makao makuu ya wizara na balozini.
8.0 MALENGO YA TAASISI ZILIZO CHINI YA
WIZARA KWA MWAKA WA FEDHA
2022/2023
Kituo cha Kimataifa cha Mikutano Arusha (AICC)
- Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha Mwaka wa Fedha 2022/2023, Kituo kimepanga kukusanya mapato ya shilingi 16,737,049,856 kutokana na vyanzo vya ndani. Mapato hayo yatatumika kugharamia uendeshaji wa kituo, mishahara na ununuzi wa vifaa tiba na mradi ya maendeleo ya ujenzi wa jengo la wagonjwa wa nje katika Hospitali ya AICC.
- Mheshimiwa Spika, Kituo kitaendelea kuvutia mikutano ya kimataifa kwa lengo la kuongeza mapato yake na kuitangaza nchi kama kitovu cha diplomasia ya mikutano. Ninayo furaha kulijulisha Bunge hili kuwa Kituo kinategemea kuwa mwenyeji wa mikutano ya kimataifa ikiwemo kikao cha Shirikisho la Soka Barani Afrika (CAF) na African Women in Leadership itakayofanyika ukumbi wa AICC jijini Arusha mwaka wa fedha ujao.
- Mheshimiwa Spika, Kituo kinakamilisha taratibu za kuanza ujenzi wa Kituo cha mikutano kitakachoitwa Mount Kilimanjaro International Convention Centre jijini Arusha. Kituo hicho kitaimarisha na kuongeza kasi ya utekelezaji wa diplomasia ya mikutano na maonesho hapa nchini.
Chuo cha Diplomasia
226. Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2022/2023 chuo kimepanga kukusanya shilingi 3,601,210,000 kutoka katika vyanzo vya ndani. Aidha, chuo kinatarajia kutekeleza majukumu yafuatayo:
- Kuendelea kutoa mafunzo ya uhusiano wa kimataifa, lugha ya Kiswahili kwa wageni, na mbinu za kidiplomasia;
- Kuendelea kutafiti maeneo ya uhusiano wa kimataifa na mbinu za kidiplomasia;
- Kuendelea kuboresha miundombinu ya kufundisha na kujifunzia;
- Kuendelea kuwajengea uwezo wa kitaaluma watumishi wa chuo;
- Kuendelea kutoa ushauri na huduma za kitaalamu kwa Serikali na taasisi zake; na
- Kuendelea kukitangaza chuo kitaifa na kimataifa.
Mpango wa Hiari wa Afrika wa Kujitathmini katika Masuala ya Demokrasia na Utawala Bora (APRM)
227. Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha mwaka wa fedha 2022/2023, APRM inatarajia kutekeleza majukumu yafuatayo:
- Kuendelea kufanya tathmini katika masuala ya demokrasia na siasa, usimamizi wa uchumi, uendeshaji wa mashirika ya biashara na utoaji wa huduma za jamii;
- Kuhuisha mbinu za utafiti kwa kupitia upya hojaji ya APRM, kuboresha viashiria vya utafiti, kuzingatia matumizi ya teknolojia katika utekelezaji wa mpango na kupanua wigo wa zana zinazotumika katika utafiti;
- Kuratibu utekelezaji wa mpango kazi wa APRM kwa kushirikiana na wizara, idara na wakala wa Serikali katika kuandaa taarifa ya mwaka na kuweka mfumo madhubuti wa ufuatiliaji; na
- Kuimarisha mawasiliano na utoaji taarifa kuhusu mpango wa APRM kwa kuzingatia Mpango wa Mawasiliano wa Miaka Mitano 2021/2022–2025/2026.
9.0 MAKADIRIO YA MAPATO NA MATUMIZI YA
WIZARA KWA MWAKA WA FEDHA 2022/2023
- Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2022/2023, Wizara inatarajia kukusanya kiasi cha shilingi 1,559,879,000 ikiwa ni mapato ya Serikali yatakayopatikana kutokana na vyanzo vilivyopo Makao Makuu ya Wizara na Balozi za Tanzania ambavyo ni pango la nyumba za Serikali zilizopo nje ya nchi na kuthibitisha nyaraka.
- Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2022/2023, Wizara imetengewa bajeti ya kiasi cha shilingi 208,366,964,000. Kati ya fedha hizo shilingi 203,666,964,000 ni kwa ajili ya matumizi ya kawaida, zinazojumuisha shilingi 188,937,219,000 kwa ajili ya matumizi mengineyo na shilingi 14,729,745,000 kwa ajili ya mishahara. shilingi 4,700,000,000 ni kwa ajili ya miradi ya maendeleo.
- Mheshimiwa Spika, kati ya fedha za bajeti ya matumizi mengineyo ya wizara, shilingi 500,000,000 ni kwa ajili ya Mpango wa Hiari wa
Afrika wa Kujitathmini katika Masuala ya Demokrasia na Utawala Bora, shilingi 1,000,000,000 ni kwa ajili ya Chuo cha
Diplomasia, shilingi 1,243,661,150 ni kwa ajili ya Mahakama ya Afrika ya Haki za Binadamu na Watu na shilingi 170,000,000 ni kwa ajili ya Bodi ya Ushauri wa Masuala ya Rushwa ya Umoja wa
Afrika. Aidha, kati ya fedha zilizotengwa kwa ajili ya mishahara, shilingi 2,833,778,000 ni kwa ajili ya mishahara ya Chuo cha Diplomasia.
- Mheshimiwa Spika, kati ya shilingi 4,700,000,000 zilizotengwa kwa ajili ya kutekeleza miradi ya maendeleo, shilingi 4,000,000,000 ni kwa ajili ya kuanza ujenzi wa
Makao Makuu ya Mahakama ya Afrika ya Haki za Binadamu na Watu iliyopo jijini Arusha na shilingi 700,000,000 ni kwa ajili ya ukarabati wa majengo ya ofisi na makazi ya watumishi katika Ubalozi wa Tanzania Pretoria, Afrika Kusini.
10.0 HITIMISHO
- Mheshimiwa Spika, ili kuweza kutekeleza kikamilifu majukumu ya Wizara kwa mwaka wa fedha 2022/2023, ninaomba Bunge lako Tukufu liidhinishe jumla ya shilingi 208,366,964,000. Kati ya fedha hizo shilingi 203,666,964,000 ni kwa ajili ya matumizi ya kawaida na shilingi 4,700,000,000 ni kwa ajili ya Bajeti ya Maendeleo.
- Mheshimiwa Spika, ninaomba kuhitimisha kwa kukushukuru tena wewe binafsi, Mheshimiwa Naibu Spika na Waheshimiwa Wabunge kwa kunisikiliza.
- Mheshimiwa Spika, ninaomba kutoa hoja.
KIAMBATISHO
ORODHA YA MIKATABA NA HATI ZA
MAKUBALIANO YA USHIRIKIANO
ILIYOSAINIWA KATIKA MWAKA WA FEDHA 2021/2022
- Hati ya Makubaliano kati ya Wizara ya
Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika
Mashariki ya Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania na Wizara ya Mambo ya Nje na
Maendeleo ya Kimataifa ya Jamhuri ya
Burundi kuhusu Ushirikiano katika Mashauriano ya Kisiasa na Kidiplomasia iliyosainiwa tarehe 16 Julai, 2021
Bujumbura, Burundi;
- Hati ya Makubaliano kati ya Serikali ya
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na
Serikali ya Jamhuri ya Burundi kuhusu Ushirikiano katika Sekta ya Uvuvi, iliyosainiwa tarehe 16 Julai, 2021
Bujumbura, Burundi;
- Hati ya Makubaliano kati ya Serikali ya
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na
Serikali ya Jamhuri ya Burundi kuhusu Ushirikiano katika Sekta ya Madini, iliyosainiwa tarehe 16 Julai, 2021 Bujumbura, Burundi
- Hati ya Makubaliano kati ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na
Serikali ya Jamhuri ya Burundi
Ushirikiano katika Sekta ya Afya,
iliyosainiwa tarehe16 Julai, 2021 Bujumbura, Burundi;
- Hati ya Makubaliano kati ya Serikali ya
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Jamhuri ya Burundi kufundisha Lugha ya Kiswahili nchini Burundi na Kufundisha Lugha ya Kifaransa nchini
Tanzania, iliyosainiwa tarehe 16 Julai,2021, Bujumbura, Burundi;
- Hati ya Makubaliano kati ya Serikali ya
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na
Serikali ya Jamhuri ya Burundi kuhusu Ushirikiano katika Sekta ya Nishati; iliyosainiwa tarehe 16 Julai, 2021 Bujumbura, Burundi
- Hati ya Makubaliano kati ya Serikali ya
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na
Serikali ya Jamhuri ya Burundi kuhusu Ushirikiano katika Sekta ya Kilimo, iliyosainiwa tarehe 16 Julai, 2021
Bujumbura, Burundi;
- Hati ya Makubaliano kati ya Serikali ya
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Jamhuri ya Burundi Kuhamisha Wafungwa, iliyosainiwa tarehe 16 Julai, 2021
Bujumbura, Burundi;
- Hati ya Makubaliano kati ya Serikali ya
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na
Serikali ya Jamhuri ya Rwanda kuhusu Ushirikiano katika Sekta ya Habari na TEHAMA, iliyosainiwa tarehe 2 Agosti, 2021 Kigali, Rwanda;
- Hati ya Makubaliano kati ya Serikali ya
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na
Serikali ya Jamhuri ya Rwanda kuhusu Ushirikiano katika Sekta ya Elimu, iliyosainiwa tarehe 2 Agosti, 2021 Kigali, Rwanda;
- Hati ya Makubaliano kati ya Serikali ya
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na
Serikali ya Jamhuri ya Rwanda kuhusu Ushirikiano katika Sekta ya Uhamiaji, iliyosainiwa tarehe 2 Agosti, 2021 Kigali, Rwanda;
- Hati ya Makubaliano kati ya Serikali ya
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na
Serikali ya Jamhuri ya Rwanda kuhusu Ushirikiano katika Udhibiti wa Vifaa tiba, iliyosaniwa tarehe 2 Agosti, 2021 Kigali, Rwanda;
- Hati ya Makubaliano kati ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ikiwakilishwa na Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TIC) na Serikali ya Jamhuri ya Kiarabu ya Misri ikiwakilishwa na Mamlaka ya Uwekezaji na kanda Huru ya Uwekezaji (GAFI) Kuwezesha Ushirikiano wa Pamoja katika Uwekezaji, iliyosainiwa tarehe 11 Novemba, 2021 Cairo, Misri;
- Hati ya Makubaliano kati ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ikiwakilishwa na Wizara ya Sanaa, Utamaduni na Michezo na Serikali ya Jamhuri ya Kiarabu ya Misri ikiwakilishwa
na Wizara ya Sanaa na Michezo
Ushirikiano katika Sekta ya Michezo, iliyosainiwa tarehe 10 Novemba, 2021, Cairo, Misri;
- Hati ya Makubaliano kati ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ikiwakilishwa na Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia na Serikali ya Jamhuri ya Kiarabu ya Misri ikiwakilishwa na Wizara ya
Elimu na Elimu ya Ufundi kuhusu ushirikiano katika Sekta ya Elimu, iliyosainiwa tarehe 10 Novemba, 2021 Cairo,
Misri;
- Hati ya Makubaliano kati ya Serikali ya
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Jamhuri ya Kiarabu ya Misri kuhusu Ushirikiano katika Sekta ya Elimu ya Juu kwa miaka 2021-2026 iliyosainiwa tarehe 10 Novemba, 2021 Cairo, Misri;
- Mkataba kati ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Falme ya Ubelgiji kuhusu huduma ya Usafiri wa Anga uliosainiwa tarehe 3 Novemba, 2021 Dodoma, Tanzania;
- Hati ya Makubaliano kati ya Serikali ya
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Jamhuri ya Kenya kuhusu ushirikiano katika sekta ya Uhamiaji, iliyosainiwa tarehe 10 Desemba, 2021 Dar es Salaam, Tanzania;
- Hati ya Makubaliano kati ya Serikali ya
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na
Serikali ya Jamhuri ya Kenya kuhusu Ushirikiano katika Sekta ya Afya, iliyosainiwa tarehe 10 Desemba, 2021 Dar es Salaam, Tanzania.
- Hati ya Makubaliano kati ya Kituo cha
Uwekezaji Tanzania na Mamlaka ya
Uwekezaji Kenya, iliyosainiwa, tarehe 10
Desemba, 2021 Dar es Salaam, Tanzania;
- Hati ya Makubaliano kati ya Serikali ya
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na
Serikali ya Jamhuri ya Kenya kuhusu Ushirikiano wa Pamoja kuzuia na kudhibiti magonjwa ya Wanyama yanayovuka Mipaka na Magonjwa ya Wanyama Yanayoambukiza Binadamu., iliyowekwa saini tarehe 10 Desemba, 2021 jijini Dar es Salaam,
Tanzania;
- Mkataba wa Kubadilishana Wafungwa kati ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Jamhuri ya Kenya uliosainiwa tarehe 10 Desemba, 2021 jijini Dar es Salaam, Tanzania;
- Hati ya Makubaliano kati ya Serikali ya
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na
Serikali ya Jamhuri ya Kenya kuhusu
Ushirikiano katika Makazi na Maendeleo ya Miji, iliyosainiwa tarehe 10 Desemba, 2021 jijini Dar es Salaam, Tanzania;
- Hati ya Makubaliano kati ya Serikali ya
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na
Serikali ya Jamhuri ya Kenya kuhusu Ushirikiano katika Masuala ya Magereza iliyowekwa saini tarehe 10 Desemba, 2021 Dar es Salaam.
- Mkataba wa Jumla kati ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Jamhuri ya Ufaransa ushirikiano katika Sekta za Fedha,
Maendeleo na Vipaumbele katika Utekelezaji wa Miradi ya Kimkakati nchini Tanzania uliosainiwa tarehe 12 Februari 2022 Brest, Ufaransa.
- Hati ya Makubaliano kati ya Serikali ya
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na
Serikali ya Jamhuri ya Ufaransa kuhusu
Ushirikiano katika Sekta ya Uchumi wa Buluu na Usalama wa Bahari iliyosainiwa tarehe 12 Februari 2022 Brest, Ufaransa.
- Hati ya Makubaliano kati ya Serikali ya
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na
Serikali ya Jamhuri ya Ufaransa kuhusu Ushirikiano katika Sekta ya Miundombinu ya Usafiri na Maendeleo Endelevu nchini Tanzania, iliyosainiwa tarehe 12 Februari 2022 Best, Ufaransa.
- Mkataba kati ya Serikali ya Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania na Shirika la
Maendeleo la Ufaransa (AFD) kuhusu Ushirikiano katika Kuboresha Upatikanaji wa Fedha za Kilimo uliosainiwa tarehe 12 Februari 2022 Brest, Ufaransa.
- Mkataba kati ya Benki ya Maendeleo ya Kilimo ya Tanzania na Shirika la Maendeleo la Ufaransa (AFD) kuhusu Ushirikiano katika Kuboresha Upatikanaji wa Fedha za Kilimo uliosainiwa tarehe 12 Februari 2022 Brest, Ufaransa.
- Mkataba kati ya Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania na Jamhuri ya Ufaransa kuhusu Ushirikiano katika Utekelezaji wa Awamu ya Tano ya Mradi wa Usafiri wa Mabasi yaendayo kasi uliosainiwa we tarehe 12 Februari 2022 Brest, Ufaransa.
- Hati ya Makubaliano ya Ushirikiano kati ya
Mamlaka ya Viwanja vya Ndege ya Tanzania
(TAA) na Kampuni ya Kimataifa ya Bouygues Batiment International ya Ufaransa kwa ajili ya kufanya Upembuzi Yakinifu na Ukarabati wa Terminal Two katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere iliyosainiwa tarehe 14 Februari 2022 jijiniParis, Ufaransa.
- Hati ya Makubaliano ya kati ya Wizara ya
Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika
Mashariki ya Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania na Wizara ya Mambo ya Nje ya
Umoja wa Falme za Kiarabu kuhusu
Ushirikiano katika Mashauriano ya Kisiasa na Kidiplomasia iliyosainiwa tarehe 26 Februari 2022 Dubai, Umoja wa Falme za
Kiarabu.
WIMBO WA AFRIKA MASHARIKI
1. Ee Mungu twaomba ulinde Jumuiya Afrika Mashariki
Tuwezeshe kuishi kwa amani Tutimize na malengo yetu.
Chorus
Jumuiya Yetu sote tuilinde
Tuwajibike tuimarike
Umoja wetu ni nguzo yetu Idumu Jumuiya yetu.
- Uzalendo pia mshikamano
Viwe msingi wa Umoja wetu Uhuru na Amani
Mila zetu na desturi zetu.
- Viwandani na hata mashambani
Tufanye kazi sote kwa makini Tujitoe kwa hali na mali Tuijenge Jumuiya bora.
