
Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salam, Amos Makala amesema kuwa Operesheni ya kutokomeza Panya Road ni endelevu na bado inaendelea.
Mh. Makalla amesema hayo wakati akizungumza kwenye kikao Maalum na Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa ambapo amewatoa hofu Wananchi kuwa mji uko salama.
“Kwa Panya road wowote wale ambao wanadhani Operesheni hii ni ya nguvu ya soda wamekaa kwenye mashimo wakisikilizia nawaonya waache mipango hiyo hii ni Operesheni kabambe, Polisi wameongezwa, vikundi shirikishi wameongezwa, kwa hiyo wakafanye kazi nyingine” alisema
Mkuu huyo ambaye ni Mwenyekiti wa Kamanti ya Ulinzi na Usalama Dar es Salaam amewaonya wateja wa vifaa vinavyoibwa na vijana hao kuwa Operesheni nyingine iko mbioni kuwabaini wanunuzi wa vifaa vya wizi.

Amesisitiza kuacha mara moja ununuzi wa bidhaa hizo kwa ajili ya usalama wao.
Awali Kamanda wa Kanda Maalum Dar es Salaam, Muliro J Muliro amesema vijana 86 wamefikishwa kwenye Mahakama ya Wilaya ya Ilala Kinyerezi ili kusomewa mashtaka yao.
Amesema Operesheni ya kutokomeza vikundi hivyo vya Kihalifu ilifanikisha kupatikana kwa vifaa mbalimbali vilivyoibwa ikiwemo Televisheni.
Alifafanua kuwa Operesheni hiyo bado inaendelea kwa kuhusisha kitengo cha Intelijensia cha Polisi ili kubaini vijana hao ambao wengi ni vijana wadogo kiumri.
