NHC YAPEWA KIPAUMBELE BAJETI YA ARDHI

Na, Emmanuel Charles

Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt. Angelline Mabula amesema katika mwaka 2021/22, Shirika la Nyumba la Taifa NHC lilipanga kukamilisha Mradi wa Morocco Square Jijini Dar es Salaam. ambapo hadi tarehe 15 Mei, 2022, utekelezaji wa Mradi umefikia asilimia 93.

Akisoma Hotuba ya Bajeti ya Makadirio ya Mapato na Matumizi Wizara ya Ardhi, Nyumba na, Maendeleo ya Makazi Mhe Dkt. Mabula amesema Hatua hii imetokana na Serikali kuruhusu Shirika kukopa shilingi bilioni 173.9 ili kukamilisha Mradi huu na miradi mingine iliyokuwa imesimama tangu mwaka 2018 kwa kukosa fedha.

“Mpaka sasa Shirika limekopa shilingi bilioni 44.7 kati ya fedha hizo kwa ajili ya kukamilisha Miradi ya Morocco Square na Kiwanja Na. 300 Regent Estate.

Amesema kuwa, katika mwaka 2021/22, Shirika lilipanga kuanza ujenzi wa nyumba za gharama nafuu katika Halmashauri za Sumbawanga pamoja na kuendeleza Miji midogo ndani ya Mji Mkubwa (Satellite Towns) ya Uvumba (Kigamboni), Kawe (Kinondoni), Burka/Matevesi (Arusha Jiji) na eneo la Usa River (Meru).

“Napenda kuliarifu Bunge lako kuwa Shirika liko katika hatua za ukamilishaji wa taratibu za umiliki na upembuzi yakinifu katika eneo la Luguruni. Aidha, uendelezaji wa Miji Midogo ndani ya Miji Mikubwa uko katika hatua mbalimbali ambapo kwa eneo la Kawe, uandaaji wa michoro ya ujenzi wa nyumba za gharama nafuu unaendelea. Vilevile, upembuzi yakinifu unaendelea ili kuanza utekelezaji wa Mpango Kabambe wa eneo la Uvumba. Katika eneo la Burka/Mateves uandaaji wa Mpango Kabambe umekamilika na uuzaji wa viwanja katika sehemu ya eneo hilo unaendelea. Aidha, Mpango wa ujenzi wa nyumba za awali unaendelea katika eneo la Usa River.”

Ameongeza kuwa, katika mwaka 2021/22, Shirika lilipanga kuendelea na ujenzi wa nyumba katika Halmashauri ya Wilaya ya Chamwino (101) na Jiji la Dodoma (Iyumbu – 303) kwa ajili ya kupangisha na kuuza ikiwa ni utekelezaji wa mradi wa nyumba 1,000.  Napenda kuliarifu Bunge lako kuwa hadi tarehe 15 Mei, 2022, ujenzi wa nyumba 100 na jengo la maduka katika Wilaya ya Chamwino umekamilika kwa asilimia 80 na ujenzi wa nyumba 300 na majengo matatu (3) ya huduma za kijamii katika Jiji la Dodoma (Iyumbu) umekamilika kwa asilimia 90.

“Shirika lilipanga kuendelea na ujenzi wa majengo ya biashara katika Halmashauri za Manispaa za Lindi na Bukoba pamoja na kutekeleza miradi ya ukandarasi katika maeneo mbalimbali nchini. Hadi tarehe 15 Mei, 2022, usanifu wa jengo la biashara katika Halmashauri ya Manispaa ya Lindi umekamilika na marekebisho ya michoro yanaendelea kufanyika ili kuendana na taarifa ya uchunguzi wa udongo.”

Aidha, usanifu wa jengo la biashara katika Halmashauri ya Manispaa ya Bukoba umefanyika na taratibu za ununuzi kwa ajili ya kumpata mkandarasi zinaendelea.

Kuhusu utekelezaji wa Miradi ya ukandarasi, Mhe. Mabula amesema Mradi wa Ujenzi wa Hospitali ya Rufaa Mwalimu Nyerere (Mara) Awamu ya IV umekamilika kwa asilimia 96 na Mradi wa ujenzi wa Soko la Kimataifa la Mifugo la Buzirayombo (Geita) umekamilika kwa asilimia 94. Vilevile, Shirika linaendelea na mradi wa Ujenzi wa Ofisi ya Rais, Muungano na Mazingira kama Mshauri Elekezi.

Pia, mapitio ya michoro na gharama za Mradi wa ujenzi wa majengo ya Wizara ya Fedha na Mipango katika eneo la Mji wa Serikali – Mtumba yamefanyika.

  • sambamba na utekelezaji wa miradi mbalimbali, katika mwaka 2021/22, Shirika lilipanga kuandaa mipango ya uendelezaji wa maeneo mbalimbali nchini pamoja na kutekeleza Mpango wa Uendelezaji wa maeneo ya Chuo Kikuu cha Dodoma (Institutional master plan) ambao unahusisha utekelezaji wa Muundo Jumuishi (Integrated System) wa TEHAMA. Hadi tarehe 15 Mei, 2022, Shirika lilishiriki katika uandaaji wa Mipango Kabambe ya Uendelezaji wa maeneo ya Kwala (Pwani) na Mji wa Tanzanite wa Mirerani (Manyara). Aidha, uandaaji wa Mpangokina kwa ajili ya uendelezaji wa maeneo ya Chuo Kikuu cha Dodoma unaendelea.

Ujenzi wa Viwanda vya Vifaa vya Ujenzi 

  • Mheshimiwa Spika, ili kutimiza azma ya kujenga nyumba za gharama nafuu nchini hususan kwa ajili ya wananchi wa kipato cha chini, Shirika limeanza kutekeleza mpango wa kuwekeza katika ujenzi wa viwanda vya kutengeneza vifaa vya ujenzi hususan kokoto, matofali na mabati. Hadi tarehe 15 Mei, 2022, Shirika limenunua maeneo kwa ajili ya uchimbaji mchanga na uzalishaji wa kokoto pamoja na kufanya upembuzi yakinifu kwa ajili ya kupata idhini ya utekelezaji wa miradi hiyo.  Mpango wa Shirika ni kuhakikisha viwanda vya uzalishaji wa vifaa vya ujenzi vinaanza kufanya kazi mwaka 2022/23.

Ukusanyaji wa Mapato

  • Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2021/22, Shirika lilipanga kukusanya shilingi bilioni 105.6 kutokana na kodi ya pango. Hadi tarehe 15 Mei, 2022, Shirika limekusanya shilingi bilioni 76.22 sawa na asilimia 72.1 ya lengo.

Matarajio ya Shirika ni kufikia lengo hilo ifikapo Juni, 2022.

Ukarabati wa Nyumba

  1. Mheshimiwa Spika, sambamba na utekelezaji wa miradi ya ujenzi, Shirika limeendelea kufanya ukarabati wa nyumba zake kupitia Mpango wa Ukarabati unaoendelea kutekelezwa katika mikoa mbalimbali nchini. Ili kuhakikisha kwamba kazi hii inatekelezwa kwa ufanisi, katika mwaka 2021/22, Shirika lilitenga shilingi bilioninane(8) kwa ajili ya ukarabati wa nyumba 350. Hadi tarehe 15 Mei, 2022, shilingi bilioni tatu (3) zimetumika kukarabati nyumba 53 katika mikoa ya Kilimanjaro, Dar es Salaam na Katavi. Katika mwaka 2022/23, Shirika litakarabati nyumba 180 katika mikoa ya Dar es Salaam, Iringa, Tabora, Arusha, Kigoma, Morogoro, Lindi, Tanga, Mbeya, Mwanza, Singida na Kagera kwa gharama ya shilingi bilioni nane (8).

Akisoma Hotuba yake ameendelea kueleza kuwa

  • Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2022/23, Shirika limepanga kutekeleza kazi zifuatazo: –
  • Kukusanya shilingi bilioni 268.03 kutoka kwenye vyanzo mbalimbali vya mapato;
  • Kuendelea kukamilisha mradi wa ujenzi wa nyumba 300 kati ya nyumba 1,000 za gharama nafuu Jijini Dodoma kwa ajili ya kuuza na kupangisha;
  • Kukamilisha  ujenzi wa Mradi wa Morocco square na kuendelea na Miradi katika Kiwanja Na. 711 Kawe, Golden Premier (GPRProject) na ujenzi wa nyumba 500 katika eneo la Kawe kwa ajili ya wananchi wa kipato cha kati cha chini ambapo nyumba 360 zitajengwa awamu ya kwanza na nyumba

140 zitajengwa awamu ya pili; iv) Kufanya upembuzi yakinifu na usanifu wa michoro katika miji ya pembezoni (Satellite Cities) ya Kwala – Ruvu, Mbezi One Riffle

Range (Dar es Salaam) na Kawe;

v) Kuendelea na ujenzi wa majengo ya biashara katika maeneo mbalimbali nchini ikiwemo Bukoba, Mwanza, Dodoma, Kahama,

Morogoro, Masasi na Lindi; vi) Kuandaa Mpango Kabambe wa matumizi ya ardhi katika maeneo ya Iwambi na Mwashiwawala – Mbeya, Uvumba – Dar es

Salaam na Mafuru Village – Morogoro; vii) Kuendelea na utekelezaji wa miradi ya ukandarasi ikiwemo ujenzi wa Majengo ya Ofisi za Wizara nane (8) Jijini Dodoma,  ujenzi wa Jengo la Shule ya Uchumi ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Ujenzi wa majengo matano (5) ya  Wakala wa Ununuzi wa Serikali (GPSA), ujenzi wa jengo la TANZANITE Mirerani, ujenzi  wa Jengo la Kitengo cha Moyo cha Jakaya Kikwete (JKCI) na miradi mingine itakayojitokeza;

viii)     Kuendelea   na     usimamizi wa     miradi mbalimbali ya kimkakati ikiwemo Soko la 

Kariakoo; ix) Kuendelea kutekeleza Mpango wa miaka mitano wa ukarabati wa nyumba za Shirika unaoishia mwaka 2027; 

  • Kununua ardhi ekari 400 katika maeneo mbalimbali ya kimkakati kwa ajili ya ujenzi wa nyumba na akiba ya ardhi; 
  • Kuanza utekelezaji wa Sera ya Ubia itakayoruhusu Sekta Binafsi kushiriki katika uendelezaji wa maeneo ya Shirika; 
  • Kuendelea na ujenzi wa viwanda vya kuzalisha vifaa vya ujenzi hususan kokoto na matofali; na
  • Kuendelea kutoa elimu kwa umma kuhusu masuala ya nyumba na kulitangaza Shirika na Sekta ya Milki nchini kupitia vyombo vya habari.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *