MPANGO WA KUKABILI MAAFA WAZINDULIWA

Mwandishi wetu- Pwani

Kamati za uratibu wa Maafa Halmashauri ya Wilaya ya Rufiji zimetakiwa kutekeleza majukumu yake kikamilifu katika kuzuia, kupunguza vihatarishi na kuwa tayari kukabiliana na maafa ili kuleta maendeleo endelevu kwa Wananchi.

Hayo yamesemwa na Mkurugenzi wa Idara ya Menejimenti ya maafa Ofisi ya Waziri Mkuu Meja Jenerali Michael Mumanga kwa niaba ya Katibu Mkuu Dkt. John Jingu wakati wa hafla ya kushuhudia utiaji saini na kukabidhi Mkakati wa kupunguza vihatarishi vya maafa pamoja na Mpango wa kujiandaa na kukabiliana na maafa iliyofanyika katika Halmashauri Wilayani Rufiji moani Pwani.

Mkurugenzi wa Idara ya Menejimenti ya maafa Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu) Meja Jenerali Michael Mumanga ( wa kwanza kushoto) akikabidhi nakala ya Mpango wa kukabili maafa kwa Mwenyekiti wa Kamati ya Ulinzi na Usalama ambaye ni Mkuu wa Wilaya ya Rufiji mkoani Pwani Meja. Edward Gowele ili kuanza kwa utekelezaji wake.

Alisema kuwa jamii ya Rufiji imekuwa ikihitaji muitikio mkubwa wa Serikali na wadau katika usimamizi kutokana uwepo wa majanga ya maafuriko, migogoro kati ya wakulima na wafugaji, ukame, magonjwa ya mlipuko, wanyama pori pamoja na wadudu waharibifu.

“Ni lazima tuchukue hatua za makusudi za kuzuia na kupunguza vihatarishi na kuwa tayari muda wote katika kukabili maafa yale ambayo hayazuiliki kwa kuwa ni mpango madhubuti ili kuleta maendeleo endelevu,” Alisema Mkurugenzi huyo.

Pia alitoa shukurani kwa Shirika la kuhudumia watoto Duniani (UNICEF) kwa ufadhili wa kuchangia jitihada za Serikali katika kuandaa mpango wa kujiandaa kukabiliana na maafa katika bajeti kwa Halmashauri mbalimbali Nchini.

Mkurugenzi wa Idara ya Menejimenti ya maafa Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu) Meja Jenerali Michael Mumanga ( wa kwanza kushoto) akikabidhi nakala ya Mpango wa kukabili maafa kwa Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Rufiji mkoani Pwani Bwa. John Kayombo.

Awali akisoma taarifa ya utekelezaji Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Rufiji Bwa. John Kayombo alibainisha kuwa Halmashauri ya Wilaya ya Rufiji imechukua hatua za kuandaa mpango wa kujiandaa na kukabili maafa baada ya kufanikiwa kufanya tathimini ya vihatarishi.

“Halmashauri inashirikiana na Ofisi ya Waziri Mkuu na imechukua hatua mbalimbali zikiwemo kuandaa mpango wa kijiandaa na kukabili maafa wa Wilaya kama ambavyo tumekuwa tukishuhudia madhara hivyo mpango huu utasaidia kuongeza ufanisi ii tuokoe maisha ya wananchi na mali zao,” alieleza Bwa. Kayombo.

Mkurugenzi wa Idara ya Menejimenti ya maafa Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu) Meja Jenerali Michael Mumanga ( wa tatu kushoto aliyekaa) akiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya wajumbe wa Kamati ya Ulinzi na Usalama Halmashauri ya Wilaya ya Rufiji mkoani Pwani.

Aidha Mkuu wa Wilaya ya Halmashauri ya Wilaya ya Rufiji ambaye ndiye Mwenyekiti wa Kamati ya Ulinzi na Usalama Meja Edward Gowele aliahidi kutekeleza mpango huo kwa kushirikiana na kamati, kusimamia na kuufanyia kazi mpango huo.

Mkurugenzi wa Idara ya Menejimenti ya maafa Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu) Meja Jenerali Michael Mumanga ( wa tatu kulia) akiwa katika picha ya pamoja na Kamati ya Ulinzi na Usalama Wilaya ya Rufiji baada ya kukabidhiwa nakala za Mpango wa kukabiliana na maafa wilayani humo.
Mwenyekiti wa Kamati ya Ulinzi na Usalama ambaye ni Mkuu wa Wilaya ya Rufiji mkoani Pwani Meja Edward Gowele pamoja na Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Rufiji Bwa. John Kayombo wakitia saini Mpango wa kukabili maafa.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *